ccm watumia kombora la udini kuvichafua vyama

abdulahsaf

JF-Expert Member
Aug 31, 2010
858
130
ansbert.jpg


Ansbert Ngurumo

WIKI mbili zilizopita nilizungumzia magonjwa kadhaa ya CCM ambayo nilionya wana CHADEMA wajihadhari nayo.
Nilizungumzia sumu ya makundi hasimu, na matumizi mabaya ya pesa kutafuta uongozi; nikataja udini, ukabila na ueneo. Kwa kuwa nilijadili yale mawili ya kwanza, na katika muktadha wa hisia za ubaguzi na machafuko ya kidini yanayonukia sasa, nimeona vema leo nijadili haya mawili ya mwisho – udini na ueneo.
Naanza kwa kusisitiza kwamba dini ni uhusiano kati ya mtu na Mungu wake. Nasema pia, kama alivyowahi kusema, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kama Mungu angependa watu wote tuwe katika dini moja, asingeshindwa. Lakini haielekei kwamba ndivyo alivyopenda.
Kama dini ni uhusiano wa binadamu na Mungu, na kama Mungu huyo huyo hajalazimisha binadamu hao kuwa katika dini moja, kwanini binadamu tulazimishane dini? Kwanini tushindane kwa dini zetu? Kwanini tudharauliane kwa dini zetu?
Kama Mungu amevulimia watu na dini zao mbalimbali; kama amevumilia hata wanaodiriki kutamka na kusisitiza kwamba “Mungu hayupo,” kwanini sisi binadamau tushindwe kuvumiliana katika tofauti za dini zetu mbalimbali?
Na dini zote ninazojua zinafundisha na kusisitiza kwamba Mungu ni mweza wa yote. Hakuna linalomshinda. Yeye ndiye asili ya nguvu zote. Hana mwanzo, hana mwisho. Yeye ni mwanzo na mwisho wa yote.
Kama ndivyo ilivyo, inakuwaje binadamu huyu dhaifu anathubutu kupambana na binadamu mwenzake, eti anampigania Mungu wake aliyetukanwa au aliyedhalilishwa?
Mungu wetu amekuwa dhaifu kiasi kwamba tunadhani nguvu zetu ndizo zinazoweza kumnusuru? Hivi, kumpigania Mungi si sawa na kumdhihaki? Si sawa na kutangaza hadharani kwamba Mungu wetu ni dhaifu kama sisi?
Na nani aliyesema kuna dini (madhehebu) bora kuliko nyingine? Hivi kama kila muumini wa dini husika angezingatia vema mafundisho makuu ya dini yake, binadamu tungepigania tofauti za kidini?
Labda hayo yote yanajadilika kutokana na misingi ya malezi ya mtu kidini. Labda kuna watu walioaminishwa tangu utotoni kwamba dini yao ni bora, na nyingine ni mbaya. Labda wapo walioaminishwa tangu utotoni kwamba mapambano ya kidini yanampendeza Mungu.
Lakini lipo swali jingine tunalopaswa kujiuliza. Hivi dini ya mtu ni mafanikio ya kujivunia mbele ya wengine?
Mimi najua fika kwamba, kwa mfano, hakuna mtu anayezaliwa katika dini fulani. Mkristo hupata Ukristo wake kwa kubatizwa, na Mwislamu kwa kusilimishwa. Na ni wachache wanaochagua dini ukubwani.
Kwa hiyo, wengi wetu tumejikuta na imani tulizonazo kwa sababu wazazi wetu walituchagulia, wakatuingiza. Nao walituingiza katika imani ambazo walikuwa nazo wakati wanatuzaa.
Maana yake ni kwamba kama mimi ningezaliwa katika familia ya Kiislamu, ningekuwa Mwislamu. Kama ningezaliwa kwenye familia ya Kihindu, ningekuwa Mhindu. Kama ningezaliwa kwenye familia ya Kiyahudi, ningekuwa Myuda. Kama ningezaliwa kwenye familia ya Kisabato ningekuwa Msabato!
Halikuwa chaguo langu, kwa mfano, kuwa Mkatoliki. Ni ajali ya kihistoria kwamba nilizaliwa kwenye familia ya Wakatoliki, nikabatizwa na kulelewa Kikatoliki.
Kwa mantiki hiyo, imani yangu si jambo nililohangaikia na kufukuzia hadi nikalipata. Si zao la jasho au bidii ya aina yoyote. Ni matokeo ya mfumo nilioukuta baada ya kuzaliwa. Nina haki ya kubadili dini wakati wowote, au kubaki na ile ile niliyopewa na wazazi wangu.
Kwa maana hiyo, ni ukosefu wa maarifa kwa mtu yeyote kutumia dini kama mafanikio binafsi anayojivunia, na ambayo anayatumia kukejeli wengine ambao si wa imani yake.
Ni ukosefu wa busara kwa mtu yeyote kutumia dini yake kama kigezo cha ubora wake dhidi ya wengine. Ni ujinga uliopitiliza kwa mtu yeyote kudhani kwamba ataipata mbingu kwa kushambulia, kulazimisha, kudharau na kuumiza wenzake kwa ajili ya tofauti za kidini.
Ndiyo maana tunawaonya hata wanasiasa wanaodiriki kutumia dini kama kigezo cha kujitafutia umaarufu. Umaarufu unaopatikana kwa misingi ya chuki za kidini, ni umaarufu unaomwelekeza mwenye nao kwenye shimo la uharibifu. Ni umaarufu wenye harufu ya mauti.
Ni umaarufu wenye madhara kwa mtu mwenyewe na kwa taasisi aliyomo. Ndiyo maana baadhi yetu tuliwakemea kwa nguvu wanasiasa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) walipodiriki kukichafua Chama cha Wananchi (CUF) miaka ya 2000 hadi 2005 kwamba ni chama cha kidini.
Walijua dhambi waliyokuwa wanatenda, lakini walidhani kwa kuwa chama chao kipo madarakani wangeweza kujinusuru na matokeo ya dhambi hiyo. Lengo lao lilikuwa kukishambulia na kukimaliza nguvu CUF mbele ya macho ya umma.
Walitumia vibaya ajali ya kihistoria ya CUF kuwa na wanachama wengi kutoka Zanzibar ambako asilimia kubwa ya wakazi wake ni Waislamu; na wana utamaduni unaofanana kijamii na kidini.
Walitumia vibaya udhaifu wa CUF kwenye idara ya uenezi na propaganda. Wakawashibisha Watanzania uchafu huu, na baadhi ya wananchi, kwa kutazama tu ajali za kihistoria, wakakubaliana na uongo wa CCM kwamba CUF ni chama cha kidini.
Dhambi hii ya CCM imewatafuna CUF kwa bahati mbaya. Imewasaidia CCM kwa kiwango fulani kushusha haiba ya CUF mbele ya umma. Ikichanganywa na udhaifu wa kimkakati ndani ya CUF, imekinyima chama hicho fursa ya kukua upande wa Tanzania Bara.
Lakini haijakiacha salama CCM. Kila mara CCM wanapoguswa pabaya, wanatafuta kombora la kurushwa kwa washindani wao. Kama walivyotumia kombora la udini dhidi ya CUF miaka ya 2000 – 2005, ndivyo wamethubutu kutumia kete hiyo hiyo mwaka 2010 dhidi ya CHADEMA.
Kwa kutumia nguvu ya dola, waliweza kuingilia hata mitambo ya simu na kutengeneza meseji za chuki ya kidini na kuzisambaza, wakidai zinatoka kwa viongozi, mashabiki na makada wa CHADEMA.
Lakini sote tunajua kwamba wenye uwezo wa kitaasisi wa kufanya hayo ni wao wenye vyombo vya dola na mfumo wa kitaasisi unaoingilia mifumo ya utendaji ya vyombo vingine. Kwa Kiingereza dhana hii inaitwa spoofing.
Hadi sasa imeshindwa kukisaidia CCM kukimaliza CHADEMA kwa kuwa imekuja wakati nchi imeshaanza kukua kuelekea demokrasia ya kweli. Wamefanya makosa yale yale ya nyuma ambayo yalishatumika kama somo kwa wengine.
CCM wamefanya mambo haya wakati jamii imeshawachoka. Haiko tayari kuamini propaganda zao chafu dhidi ya CHADEMA. Wamefanya hivyo huku wakijua kuwa kwa sasa ni rahisi kwa jamii kuamini uongo wa CHADEMA kuliko ukweli wa CCM.
Maana yake ni kwamba wananchi wa leo wapo tayari kwa mabadiliko. Na mabadiliko ya kwanza wanayowazia sasa ni kuiondoa CCM madarakani.
Hivyo, ili CCM kiweze kuaminika na kukubalika tena, lazima kifanye jitihada mpya na za kisasa. Kibadilike kimfumo na kimwenendo. Nani miongoni mwao ataweza kazi hiyo?
Hata hivyo, ingawa CHADEMA hadi sasa kimeweza kuonesha dalili za kuvuka kihunzi hiki za shutuma za udini, mtihani haujaisha. Bado hakijashinda.
Naziona jitihada za CCM kupandikiza udini ndani ya CHADEMA. Naona baadhi ya wana CHADEMA wakishindwa kubaini asili ya jitihada hizi. Wengine wanajikuta wamenaswa na propaganda za CCM.
Nimewaona baadhi yao wakithubutu kutumia kauli zile zile za udini zinazorushwa kwao na CCM. Nimeona baadhi ya wana CCM wakihamia CHADEMA na ajenda za udini, na kujaribu kutumia imani zao kujenga makundi ya wafuasi.
Ama wanafanya hivyo kwa imani binafsi au wana ajenda yao kwa ajili ya kuivuruga CHADEMA na kuinusuru CCM.
Lakini naweza kutabiri kwamba jitihada zozote za kufanya siasa kwa kutumia mwavuli wa dini zitaleta maangamizi makubwa kwa wanaoshambuliwa na wanaoshambulia. Zitabomoa vyama, jamii na taifa zima.
Matokeo ya siasa za kidini ndiyo yamezaa baadhi ya hisia hizi tunazoanza kushuhudia zikihatarisha mustakabali wa taifa letu.
Haya ni matokeo ya malezi mabaya ya baadhi ya wanasiasa na watawala ndani ya CCM. Ni matokeo ya ombwe la uongozi ambao tumekuwa tukilijadili kwa muda sasa.
Ndiyo maana Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kwamba wanasiasa wanapoanza kufilisika kisiasa, huanza kujihalalisha kwa ukabila na udini.
Udini na ukabila ni maeneo nyeti ambayo yanapoguswa tu, wapo watu walio tayari kuyapigania hadi tone la mwisho la damu yao, kwa sababu ya mazingira na malezi yale yale ya kudhani kwamba ni heshima kwao kuumiza binadamu wenzao kwa heshima na utukufu wa Mungu!
Bahati mbaya haya nayo yamekuwa magonjwa sugu na silaha za maangamizi za CCM dhidi ya wapinzani wao. Walifanikiwa kwa CUF. Je, watafanikiwa kwa CHADEMA pia? Je, CHADEMA watakuwa wazembe kiasi hicho?


 
Ni kosa la kijiografia kilichoiponza Cuf,na inawezekana hata baadhi ya kauli za viongozi na wafuasi wa cuf ziliwapa nafasi ccm.Kutokana na kuwa na ngome Zanzibar hususan Pemba ilikuwa rahisi,elimu nayo imechangia,mwaka2005 nilikuwa wakala wa cuf katika uchaguzi kituo cha chuo kikuu,cuf ilishunwa vibaya mmoja wa viongozi tukiwa tunazungumzia hali hii akadfiriki kusema kwa sababu huku wakristo wako wengi,baada ya hapo nikawakimbia kwani mi ni mkristu,na ukristu wangu haukuwa sababu ya mimi kuwa wakala wa cuf.
Tulimsikia naibu katibu mkuu cuf Zanzibar akitamka wameshindwa uchaguzi kwa sababu wakristu na wababra wako wengi kwenye jimbo husika.
Aidha propaganda zimewaingia au kukosa elimu,na mbinu hizi hata wakiamua kuzitumia kwa cdm haitowezekana kwa sababu imeenea kutoka Dar hadi Mbeya.kutoka Mwanza hadi Mtwara,au tuseme unabii umefika wakati wa ukombozi ni sasa si ule wa ndugu yangtu mtikila aliwahi sanan
 
Wamegunduliwa udini sasa wanabaki na fitina ya chama cha ukanda.alivyokuwa bob makani msukuma haikuwa ya ukanda kuwa mbowe na silaa imekuwa ya ukanda.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom