CCM wadaiwa kuingiza udini vurugu za Arusha

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
Mwananchi wetu
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Arusha, kinatuhumiwa kuanza mchezo mchafu wa kuufanya mgogoro wa uchaguzi wa Meya wa jiji la Arusha uliosababisha vifo vya watu watatu, kuwa wa kidini.

Habari za uhakika kutoka ndani ya chama hicho, zimebainisha kuwa katika kufanikisha njama hiyo, baadhi ya viongozi wamefanikiwa kuwashawishi baadhi ya masheikh jijini Arusha, kutoa tamko la kulaani vurugu na kupinga kile wanachodai kuwa ni viongozi wa dini kujiingiza katika siasa.


Mpango wa kuwatumia baadhi ya Waislamu kuingilia mgogoro huo ulianza tangu juzi, siku moja baada ya umoja wa viongozi wa dini ya kikristo, kutoa tamko la kutomtambua Meya ya jiji hilo kwa tiketi ya CCM, Gaudence Lyimo.

Maaskofu hao pia waliaani kitendo cha polisi kutumia nguvu kubwa kupita kiasi kuvunja maandamano yaliyoandaliwa na Chadema kupinga mchakato wa uchaguzi huo.

Juzi jioni baadhi ya wanaCCM waonekana wakiwa kwenye harakati za kuwaalika waandishi wa habari kuhudhuria mkutano wa mashekhe uliofanyika jana mchana jijini Arusha, kulaani tamko la maaskofu.

"Kesho mashekh wanatoa tamko....Huu ni mgogoro wa kidini, maaskofu hawamtaki Kikwete ndio sababu wanampinga hadi Meya...Hali hii itatufikisha pabaya,"alisema kiongozi mmoja wa CCM (jina tunalo).

Kama ilivyodokezwa na viongozi hao wa CCM juzi, jana baadhi ya masheikh wa Msikiti Mkuu wa Arusha, waliitisha mkutano na waandishi wa habari na kutoa tamko la kulaani vurugu, ghasia na uvunjifu wa amani uliotokea wakati wa maandamano ya Chadema.

Katika tamko hilo ambalo nakala imesambazwa kwa jeshi la polisi, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Usalama wa Taifa, Mkuu wa wilaya ya Arusha, Ofisi ya Mbunge wa Arusha Mjini, Ofisi ya Meya wa Arusha na Ofisi ya Mkurugenzi, lililosomwa na Imamu wa msikiti huo, Mohamed Hambali Waislamu hao walisema tukio hilo liliwaathiri sana.

"Tumeshindwa kufanya ibada zetu msikitini kwa amani na utulivu, uharibifu wa mali ikiwa pamoja na kuchomwa moto majengo, kutupiwa mawe msikitini na watoto na wazee kuathirika,"inasomeka sehemu ya tamko hilo.

Tamko hilo, pia lilisomeka" Sisi viongozi wa dini ya Kiislamu tunawakumbusha wenzetu kwamba hatupaswi kuingilia maswala ya kisiasa kwa kutoa matamko ambayo yatapelekea uvunjifu wa amani."

Kauli hiyo, ambayo inaungana na kauli ya Katibu wa CCM mkoa wa Arusha, Mary Chatanda, aliyoitoa juzi, inaaminika kuwa ililenga kuwasema maaskofu ambao walitoa tamko la kutomtambua Meya wa CCM kutokana na kuchaguliwa bila kufuata utaratibu.

Tamko hilo, liliendelea kusema, " sisi viongozi tunatakiwa tuwe washauri wa kiroho na kusisitiza amani iliyopo. Ni vyema watu wakafuata kanuni na sheria za nchi kama inavyosomeka katika katiba ya nchi.

Taarifa hiyo, ilinukuu ibara ya 19(2) inayosomeka,"Kazi ya kutangaza dini kufanya ibada na kueneza dini itakuwa ni huru na jambo la hiari la mtu binafsi na shughuli za uendeshaji wa jumuiya za dini zitakuwa nje ya mamlaka ya nchi"

Tamko hilo la kwanza la aina yake kwa Waislamu wa Arusha ambao kwa miaka mingi wamekuwa na misuguano na serikali ilieleza kuwa, waislamu watatii mamlaka iliyochaguliwa kwa mujibu na kanuni za nchi .

"Tunatambua ibara 107(1) mamlaka yenye kauli ya mwisho ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, itakuwa ni Mahakama." ilisomeka taarifa hiyo.

Mwisho taarifa hiyo, ilitoa pole kwa wote walioathirika katika maandamano hayo yaliyofanyika juma iliyopita jiji Arusha ikiwamo familia za watu waliofariki dunia kwa kupigwa risasi za moto.

Hata hivyo mwenyekiti wa Kamati ya Msikiti Mkuu wa Arusha, Abdulaziz Mkindi, alikanusha tamko hilo kutolewa kwa shinikizo la CCM.

"Hili ni tamko letu sisi hatutumiwi na CCM wala serikali....Sisi waislamu wa Arusha Mjini tumeathirika sana na hizo vurugu na tunataka amani,"alisema Mkindi ambaye alikuwa pamoja na Imamu Hambali.

CCM wadaiwa kuingiza udini vurugu za Arusha
 
Back
Top Bottom