Elections 2010 CCM sasa ni ya matajiri!?

asha ngedere

Member
Nov 6, 2009
92
11
CCM sasa ni ya matajiri, maskini wakafie mbele!

  • Wengi wakimbilia Ubunge, Udiwani kuficha maovu yao
  • Agizo la kutenganisha biashara na siasa lawekwa kapuni

Na Daniel Mbega

“CHEO ni dhamana, nitatumia cheo changu kwa faida ya wote.” Hii ni mojawapo ya Ahadi 10 za Mwana-TANU ambazo zilirithiwa na Chama cha Mapinduzi inayosisitiza kwamba mtu yeyote anayepewa uongozi hapaswi kuutumia kwa maslahi yake binafsi bali kwa maslahi ya wote.

Ahadi hii na nyinginezo zilikuwa zikiimbwa kila mahali kuanzia shule ya msingi, sekondari na vyuo vikuu ambako somo la Siasa lilianzishwa na serikali ya TANU na kuendelezwa na CCM kabla ya kufutwa mwanzoni mwa miaka ya 1990 kufuatia kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa.

Vijitabu vingi vya TANU na Azimio la Arusha vilikuwa vimesambazwa ambapo kila mjumbe wa nyumba kumi kumi alikuwa navyo vya kutosha kuwagawia wananchi wake ili waweze kuelewa wajibu wao na siasa kwa ujumla na kuhamasisha Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea ambayo sasa imezikwa na wajanja wachache walioamua kuukumbatia ubepari kwa kisingizio cha Soko Huria.

TANU (na baadaye CCM) iliamini binadamu wote ni sawa na kusisitiza raia wote kwa pamoja wamiliki utajiri wa asili wa nchi hii ukiwa kama dhamana kwa vizazi vyao; na Kwamba ni wajibu wa Serikali, ambayo ni watu wenyewe, kuingilia kati kwa vitendo maisha ya uchumi ya Taifa ili kuhakikisha usitawi wa raia wote na kuzuia mtu kumnyonya mtu mwingine au kikundi kimoja kunyonya kikundi kingine na kuzuia limbikizo la utajiri kufikia kiasi ambacho hakipatani na siasa ya watu wote kuwa sawa.

Tunaelezwa bayana kwamba TANU (sasa CCM) ni chama cha wakulima na wafanyakazi na ikasisitiza katika katiba yake kwamba, Serikali lazima itumie mali yote ya nchi yetu kwa kuondoshea umaskini;ujinga na maradhi;

Kuona kwamba Serikali inaondoa kila namna ya dhuluma, vitisho, ubaguzi, rushwa na upotofu; na Kuona kwamba Serikali ya nchi yetu inasimamia barabara njia kuu za kuzalisha mali na inafuata siasa ambayo itarahisisha njia ya kumiliki kwa jumla mali za nchi yetu.

Njia kuu za uchumi ambazo zinapaswa kuwa chini ya wakulima na wafanyakazi ni pamoja na ardhi, misitu, madini, maji, mafuta na nguvu za umeme;njia za habari, njia za usafirishaji; mabenki, na bima; biashara na nchi za kigeni na biashara za jumla; viwanda vya chuma, mashini, silaha, magari, simenti, mboleo; nguo, na kiwanda chochote kikubwa ambacho kinategemewa na sehemu kubwa ya watu katika kupata riziki zao au kinachotegemewa na viwanda vingine; mashamba makubwa na hasa yale yanayotoa mazao ya lazima katika viwanda vikubwa.

Suala la mgawanyo wa mali za umma limekuwa kitendawili kigumu kuteguliwa hasa baada ya kushuhudia namna viongozi wa chama na serikali wanavyojilimbikizia mali nyingi za umma, wakijali zaidi matumbo yao kuliko ya Watanzania licha ya kuwepo kwa maadili ya uongozi ambayo nayo yameendelea kubaki kwenye makaratasi na kufungiwa kabatini huku agizo la kutenganisha biashara na siasa likiwa limesahauliwa kitambo!

Viongozi hawa ambao wanaagizwa na chama kwamba ‘Cheo ni dhamana’, pamoja na kubadili mfumo wa siasa kutoka Ujamaa kuja kwenye Ubepari, bado wanashindwa kufuata maadili sahihi ya uongozi, yakiwemo kutojilimbikizia mali kwa kutumia vyeo vyao, kutaja mali zao kabla ya kuingia madarakani na baada ya kutoka, badala yake wanaendelea kuchota mali za umma kadiri wapendavyo huku wananchi wakiendelea kuogelea kwenye umaskini.

Kila kiongozi anayeingia madarakani kwa sasa huangalia kwanza tumbo lake, na kadiri siku zinavyosonga hupata tamaa ya kuchota zaidi na zaidi na mwishowe huona kwamba ni haki yake kuwa tajiri huku wengine wakiendelea kupiga miayo bila kuwa na uhakika hata wa kipande cha mhogo kushibisha tumbo kwa mlo mmoja.

Viongozi wa chama hiki ambacho tulitegemea kingeleta na kuendeleza mapinduzi ya kweli kwa kila Mtanzania, leo hii si chama cha wakulima na wafanyakazi kama tulivyoelezwa enzi zile za Mwalimu.

Tangu tulipopata uhuru wetu Desemba 9, 1961 Serikali ya Awamu ya Kwanza ilihimiza lazima kusiwe na tabaka mbili:tabaka ya chini ya watu wanaoishi kwa kufanya kazi, natabaka ya juu ya watu wanaoishi kwa kufanyiwa kazi.

Yale yaliyokatazwa, hasa ya kuweka matabaka baina ya matajiri na maskini, leo hii siyo jambo geni ndani ya CCM ambayo imefuta kabisa dhana ya mkulima na mfanyakazi kuwa muhimili wa chama.

CCM kimekuwa chama cha mabwanyenye ambao kila siku ama wanafikiria namna ya kuingia madarakani au jinsi ya kuendelea kuchota na kukalia madaraka hata kwa kuzivunja zile ahadi za chama, ikiwemo kutumia rushwa ingawa midomoni mwao wanaimba kuwa ‘rushwa ni adui wa haki’, tena wengine wanaongeza kwamba ‘ni dhambi’!

Ukitazama mchakato wa kura za maoni kwa mwaka 2010 ndani ya chama hicho utaamini kwamba CCM ni Chama cha Matajiri, si Chama cha Mapinduzi kama ambavyo tunaimba midomoni. Wengi ni wanafiki wakubwa na wameanza kuitumbua nchi mara tu baada ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, kufariki dunia mwaka 1999.

Ukiwachungulia baadhi ya walioshinda kura za maoni lazima utakutana na majina ya watu ambao wanasifika ndani ya jamii yetu kwa mambo maovu, yakiwemo ya ukwepaji wa kodi kwenye biashara zao nyingi zikiwa hazifahamiki sawasawa.

Kwa ujumla utakutana na wafanyabiashara wengi ambao wanatajwa kwamba wamepata nafasi hiyo kutokana na ‘mchango wao kwa chama’, hasa fedha, bila kujali misingi iliyounda chama hicho kikongwe zaidi barani Afrika, na pekee ambacho kinaendelea kusimama imara ingawa kwa sasa kinaelekea kuyumba.

Nakumbukwa wakati wa mchakato wa kumtafuta mgombea wa urais kupitia CCM mwaka 1995 walijitokeza wanachama wengi ambao wengi wao nilihudhuria hata mikutano yao ya kutangaza azma za kuwania nafasi hiyo.


Lakini kuibuka kwa wagombea wengi kiasi hicho kulimpagawisha sana Mwalimu Nyerere, ambaye aliamini kwamba hiyo haikuwa demokrasia tena bali chama kilikuwa kimevamiwa na kwamba kilikuwa na viongozi ‘wabaya’, ambao dhahiri aliwaona walikuwa na nguvu na wangeweza kupitishwa na chama kushika madaraka ya nchi.


Nyerere aliona kwamba chama kilikuwa kimevamiwa na watu wenye fedha, ambao walikuwa tayari kumsimika ‘mtu wao’ kwa kutumia fedha hizo ambazo Mwalimu Nyerere aliziita ‘fedha za bhangi’, akimaanisha kwamba zilikuwa fedha chafu ambazo hata upatikanaji wake ulikuwa wa njia zisizo halali ndiyo maana walikuwa tayari kuzitumiza watakavyo ili kulinda ‘maslahi’ yao.


Akawaponda wagombea wengine waliokuwa kwenye mchakato huo akisema; “Mnakimbilia Ikulu, Ikulu kuna biashara gani pale? Mnataka kwenda kufanya nini Ikulu? Ikulu ni mahali patakatifu, si mahali pa mchezo mchezo pale. Ni mahali pa kuheshimika!”


Hata hivyo, miaka michache baadaye wale aliodhani wangefuata falsafa yake wakawa wamekengeuka na kuamua kuitia najisi Ikulu, sehemu takatifu ambayo Nyerere alipigania kuhakikisha hakiingii kilicho ‘kichafu’.


Kusema ukweli, CCM ya sasa imebaki na katiba tu, ndani yake hakuna wanachama wenye katiba ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, kwa sababu misingi aliyoiacha imebomolewa na kuigeuza rushwa kuwa ni sehemu ya maamuzi ndani ya Chama hicho.


Watu wenye fedha haijalishi kama ni za halali au za ‘bhangi’ kama mwalimu Nyerere alivyopata kusema ndio wenye sauti kwenye chama na wanaweza kushinikiza jambo lolote kwa wananchi kwa kutumia pochi zao.


Kukosekana kwa kanuni madhubuti za kukiendesha ndiko kumefanya wakulima na wafanyakazi wasipate nafasi na badala yake kimevamiwa na wafanyabiashara na walanguzi wakubwa. Wafanyabiashara hawa ndio wenye sauti ndani ya chama, wanaweza kuamua lolote kwa nguvu ya fedha.


Kwa sasa mkulima, ambaye ni maskini wa mwisho ndani ya nchi hii kutokana na kutowezeshwa, anaonekana dhahiri hawezi kupata nafasi ya kuongoza ndani ya Chama hicho, zaidi ya kuwa shabiki wa vitendo viovu kama vile rushwa, ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka.


Wapo wanachama wengi wa CCM ambao wameelekea upinzani baada tu ya kura za maoni. Ingawa ni kawaida kwa mambo haya kutokea kila ifikapo kipindi cha uchaguzi, lakini kuondoka kwa makada wengi kunaonyesha dhahiri mambo si shwari.


Ni ukweli ulio wazi kuwa mchakato wa kura za maoni uligubikwa na vitendo vya hila, chuki na rushwa za waziwazi miongoni mwa wanachama na viongozi wa juu hawakukemea vitendo hivyo, licha ya kuwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ilijitahidi kudhibiti.


Yawezekana kuna ukweli ndani yake, lakini CCM inapaswa isiwakemee wale wanaoikosoa, badala yake ijichunguze kama imesimama sawasawa katika misingi iliyowekwa na waasisi wa Taifa hili.


Leo hii mtu akipata ujasiri wa kuhoji ni wapi matajiri hawa ‘wanaoisaidia CCM’ ataonekana katumwa ama anatumiwa. Kwa bahati nzuri, sisi tunapenda kuona Tanzania inaendelea na wananchi wananufaika na matunda ya rasilimali zao, hivyo hatuna budi kukikosoa chama ili kijirekebishe.


Inakuwaje watu ambao wanasifika kwa tabia za utapeli, ufisadi na ukwepaji wa kodi leo hii ndio wawe na nafasi kubwa ndani ya chama? CCM huwa hailioni jambo hili mapema ama huleweshwa na fedha wanazozitoa kukisaidia?


Tukiwachunguza hata hawa waliopitishwa kwenye ubunge na udiwani mwaka huu ndani ya CCM, hakika tutawakuta ‘waovu’ ambao wamejificha kwenye siasa kulinda maslahi yao. Kwamba wakiwa ndani ya ‘chama’ hakuna atakayewanyooshea kidole, hasa ikizingatiwa kwamba bado wanaendelea ‘kukisaidia’ chama.


Vijana wenzangu tuna wajibu wa kuwahoji watu hawa wamepata mali hizo kwa njia zipi hata kama watakuwa ni ndugu zetu wa karibu ama wazazi wetu. Jambo hili linawezekana tukipata ujasiri wa kuhoji wakati tunapoona rasilimali za nchi zinahodhiwa na watu wachache kwa maslahi yao binafsi.


SOURCE: DIRA YA MTANZANIA, AGOSTI 30, 2010


My Take:
Kweli misingi imekiukwa. anayejua data zaidi za wanaojificha ndani ya chama-dume (ccm) atuorozeshee matajiri wote na ma-tycoon + matapeli, majambazi, wauza unga wanaojificha huko. pengine tutakuwa makini nao hata uraiani.
 
Ehhh bwana weee, siyo Rostam Azziz, Lowassa, Kinana (muuza meno ya Tembo), Chenge, na akina ..................
Nilisahau kaka..kumbe tulitakiwa kutaja wa CCM peke yake... basi Pinda
 
Mbona hii si siri? watanzania wenzangu jamani kwani leo ndio linaonekana?
Mimi nimeshuhudia wengi waliofilisi mashirika ya umma na waliofirisi vyama vidogo na vikuu vya ushirika ndio wagombea wengi wa ubunge na udiwani. Halafu wanakubalika sana kwa sababu tu ya pesa ya wizi waliyonayo.
Kwa mfano huko Kagera yuko mama mmoja alihusika sana na wizi kwenye chama cha ushirika. Miaka michache tu baadaye aliibuka katika udiwani kupitia viti maalum sisi m. Baadaye mara huyo nikasikia ni katibu wa sisi m wa wilaya. Na sasa nasikia amepitishwa kati ya wabunge wa viti maalum sisi m.
Yupo mwingine ni mwanaume wa kata moja huko Katoro wilaya ya Bukoba naye amekuwa na visa vingi vya wizi kwenye chama cha ushirika na baadaye alijitokeza kwenye kugombea udiwani na akapata. Orodha ya namna hii ni ndefu.
Hili si siri. Msururu ni mrefu.
 
Back
Top Bottom