CCM na changamoto za siasa za umoja

abdulahsaf

JF-Expert Member
Aug 31, 2010
858
130
[h=1]
img_72301.jpg
[/h]
IMG_0724.jpg


Na Ahmed Rajab

KUNA zama ambapo Zanzibar ilikuwa haikugawika kisiasa. Bila ya shaka kulikuwa na matabaka ya kijamii na watu walikuwa na tofauti zao za kimaisha, lakini kwa jumla Wazanzibari wote wakijihisi kuwa ni watu wamoja, kitu kimoja.
Hizo zilikuwa nyakati kabla ya kuzuka kwa siasa za vyama vyama ambavyo baadhi yao vilitumiwa na watawala wa kikoloni wa Kingereza kuwagawa Wazanzibari.
Zama hizo, badala ya vyama vya kisiasa, Wazanzibari wakijishughulisha na vyama vingine kama vile vya densi, ngoma, muziki na michezo ikiwemo soka. Badala ya kuwako ushindani wa vyama vya kisiasa kulikuwako na ushindani wa vyama vya burdani.
Siku hizo Zanzibar ilikuwa ni nchi iliyojaa amani na utulivu. Si siasa wala si dini zilizowagawa Wazanzibari. Ndiyo pakazuka ule usemi wa ‘Zanzibar ni njema atakaye naaje.’ Nadhani hiyo hali ya amani, utulivu na umoja uliokuwapo ndiyo iliyosababisha Zanzibar ya siku hizo kubandikwa lakabu ya ‘Visiwa vya Peponi.’
Nakumbuka utotoni mwangu wakati timu ya soka ya Zanzibar ilipokuwa ikishiriki katika mechi za Afrika ya Mashariki kama zile za kuwania Kombe la Gossage, Wazanzibari wote walikuwa pamoja wakiishangiria timu yao ya taifa. Uzalendo waliokuwa nao ulikuwa wa hali ya juu.
Kwa bahati mbaya uzalendo huo ulitoweka Visiwani kwa muda wa takriban miaka 50 iliyopita. Uzalendo huo umeibuka tena hivi karibuni tu baada ya kuanza mchakato wa kuitunga upya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.
Kuna sababu kwa nini uzalendo huo ufufuke sasa. Na sababu yenyewe ni kwamba hili suala muhimu la katiba limewafanya Wazanzibari kwa jumla waamke na wawe tena wamoja, kitu kimoja, wakizicheza ‘Siasa za Umoja.’ Hizi ni siasa za kuwa na vuguvugu la umoja. Si siasa za vyama bali ni siasa zinazowaunganisha wazalendo walio wafuasi wa vyama vyote na hata wasio wafuasi wa vyama kwa lengo au malengo fulani.
Kile ambacho wengi wa Wazanzibari wanachokifanya wakati huu ni kuyapa kipaumbele maslahi ya kitaifa na kuyapa kisogo maslahi ya kichama. Ni wazi kuwa Wazanzibari hao wametanabahi kwamba cha kufikiriwa kwanza na cha kupewa uzito wakati wa kutoa maoni yao juu ya katiba mpya ni nchi yao na si chama cha kisiasa kinachotawala au cha upinzani. Cha kupiganiwa ni matilaba ya nchi na si sera za chama. Kwa hilo hawakwenda kombo wala hawajapoteza dira kwani mtu kuitakia kheri nchi yake ni sehemu ya imani ya mtu hata ya kidini.
Kuna sababu nyingine nzito zilizowafanya Wazanzibari wazikumbatie hizo Siasa za Umoja. Kwa kweli siasa za aina hiyo ndiyo dawa mujarab kwa jamii iliyokuwa imegawika kama ya Zanzibar na iliyokuwa na ugonjwa wa kisiasa kama iliokuwa nao hadi hivi karibuni.
Hii ni jamii ambayo kwa muda mrefu sana iligawika kisiasa nusu kwa nusu na hivyo kuwafanya Wazanzibari wasiweze kukubaliana kuhusu masuala nyeti yanayohusu mustakbali wao na wa vizazi vyao vijavyo.
Ule mzozano wa kisiasa baina ya vyama vya ZNP (Hizbu) na ASP uliopamba moto tangu 1957 hadi 1964 uliweza kuzimwa kwa kuanzishwa mfumo wa kuwa na chama kimoja tu cha kisiasa hatua ambayo iliikandamiza migawanyiko ya kisiasa.
Hata hivyo, mzozano huo ulifufuka uliporuhusiwa tena mfumo wa vyama vingi vya siasa na ulisababisha uhasama mkubwa na hata vifo vya kisiasa katika jamii. Mzozano na mgogoro huo wa kisiasa uliendelea hadi 2010 pale Amani Karume na Seif Sharif Hamadi walipopiga mbizi katika bahari iliyochafuka ya kisiasa kwa niaba ya vyama vyao (CCM na CUF) na wakaibuka na yale yaitwayo Maridhiano.
Maridhiano yaliukomesha kwa kiasi kikubwa ule uhasama mkongwe wa kisiasa nchini Zanzibar. Kadhalika Maridhiano yalisababisha kupatikana kwa umoja. Huu umoja wa Wazanzibari ulioimarika sasa ulianzia huko kwenye Maridhiano na ni umoja wa wale wenye matumaini mema kuhusu mustakbali wa nchi yao.
Kwa kuchomoza kwa Ajenda ya Zanzibar katika muktadha wa Siasa za Umoja Wazanzibari hao hii leo wanaamini kwamba wataweza kuupata muradi wao ilimradi waendelee kuwa na umoja na watumie njia za amani na za kikatiba kulifikia lengo lao. Lengo hilo si siri tena; ni la kutaka nchi yao irejeshewe tena mamlaka yake kamili, uhuru wake na adhama yake.
Yote hayo yasingaliwezekana bila ya kuwako siasa zinazowaunganisha wengi. Hii dhana au fikra ya Siasa za Umoja si ngeni. Haikuanza leo na wala si kwamba inatumika Zanzibar pekee. Imekwishatumiwa zamani na itaendelea kutumiwa na mataifa mengi yanayokabiliwa na upeo wa matatizo ya kisiasa, kiuchumi na kijamii. Aghalabu migawanyiko ya kisiasa isiyo na maana ndiyo huyazidisha matatizo kama hayo.
Kingine kinachoyapalilia moto hayo matatizo ni uadui baina ya vyama vya kisiasa. Na si viongozi tu wa vyama tofauti vya kisiasa wanaohasimiana bali uhasama unakuwako hata miongoni mwa wanachama wa kawaida wa vyama hivyo. Huku kwetu ilifika hadi ya wanaojiita viongozi kuamini kuwa mpinzani wa kisiasa ni adui ambaye lazima anyamazishwe, akandamizwe na hatimaye auawe.
Hii leo mazingira ya kisiasa ya Zanzibar ni tofauti kabisa na yale ya kipindi cha takriban nusu karne iliyopita. Tofauti hiyo inajidhihirisha wazi hasa tunapowaangalia wenye kutaka pafanywe mageuzi makubwa katika mahusiano kati ya Tanganyika na Zanzibar na wenye kupendekeza kwamba mahusiano hayo yawe juu ya msingi wa Mkataba.
Watu hao hawatoki kwenye chama kimoja tu cha kisiasa, si watu wa rika moja tu na wala si wa jinsia moja. Hawa ni watu wanaotoka katika makundi yote ya Zanzibar, ni wanachama wa vyama vyote vya kisiasa, wamo kwenye jumuiya za kidini na za vijana na wengine ni watu binafsi wasiojihusisha na jumuiya zozote au vyama vyovyote.
Si hayo tu bali Wazanzibari hao wanaungwa mkono na viongozi wa ngazi za juu wa sasa na wa zamani kutoka vyama vyote vikuu vya huko na si kutoka chama kimoja tu cha kisiasa.
Miongoni mwa hao waliojitokeza wazi hadi sasa kuunga mkono Muungano wa Mkataba ni Seif Sharif Hamadi, Hassan Nassor Moyo, Mansur Yusuf Himidi, Hamza Hassan Juma na Ismail Jussa Ladhu. Huu ni mseto wa aina ya pekee; mchanganyiko maalumu wa wakongwe na vijana. Unadhihirisha kuchomoza kwa vuguvugu la umoja wa kizalendo, vuguvugu lisilojali itikadi za kichama pale mstakabali wa nchi unapojadiliwa.
Tunapoyachambua maoni ya Wazanzibari kuhusu fikra mbalimbali zinazotolewa kuhusu mustakbali wa Muungano hitimisho tunalolipata ni kwamba wengi wa Wazanzibari hawautaki muundo wa sasa wa Muungano. Wao wanasema kwamba wanataka mabadiliko na wanatoa hoja mbalimbali za kuunga mkono matakwa yao ya kutaka Muungano huu uwe wa Mkataba baina ya nchi mbili zilizo huru, yaani Tanganyika na Zanzibar, na nchi zozote nyingine zitazotaka baadaye kujiunga na Muungano huo.
Kama nilivyowishadokeza wiki za hivi karibuni Tume ya Katiba inatazamiwa kurudi Zanzibar mwezi huu na kuanza tena mchakato wake wa kukusanya maoni ya wananchi wa mikoa ya Kaskazini Unguja na Kaskazini Pemba. Tume hiyo imekwishakusanya maoni mikoa ya Kusini Unguja na Kusini Pemba ilipozuru Zanzibar mara ya kwanza. Nadhani safari hii ya pili maoni ya Wazanzibari wanaotaka Muungano wa Mkataba yatazidi kuongezeka na hoja watazozitoa Wazanzibari hao zitazidishwa nguvu na umoja wao utaimarika zaidi.
Juu ya yote hayo kuna haja ya vyama vyote vya kisiasa kuendesha shughuli zao kwa uangalifu mkubwa na hadhari kuu. Vyama hivyo lazima viwe vivumilivu na visijaribu kuwakandamiza wanachama wao wenye kwenda kinyume na misimamo rasmi ya chama kuhusu Muungano, misimamo ambayo hivi sasa imepitwa na wakati na haiwavutii tena wengi wa Wazanzibari.
Nafikiri chama cha CCM kinahitaji kupewa indhari mahsusi. Chama hicho kina wajibu wa kuhakikisha kwamba hakitochafuliwa jina kwa kulaumiwa kwamba kinaziminya haki za binadamu kwa kuwanyima wanachama wake haki yao ya kimsingi ya uhuru wa kusema na wa kueleza imani zao za kisiasa.
Itakuwa ni aibu kubwa endapo chama hicho kitawakaba roho wanachama wake wasiweze kujieleza bila ya pingamizi zozote hasa kwa vile kuna jukwaa la hadhara kama la Tume ya Katiba lenye kuwahimiza wananchi wawe huru wanapotoa maoni yao kuhusu mustakbali wa nchi yao.
Labda chama cha CCM kiuigize mfano wa CUF ambacho sasa kimeitupilia mbali ile sera yake kuhusu Muungano iliyo kwenye ilani yake rasmi. Sera hiyo ikitaka pawepo ‘Muungano wa Serikali Tatu.’ Sasa chama hicho kinasema kinataka ‘Muungano utaokubaliwa na wananchi’ na viongozi wake wawili Seif Sharif Hamadi na Ismail Jussa Ladhu wamekwishatamka kwamba wao wanapendelea pawepo Muungano wa Mkataba. Kuna ushahidi kwamba hilo ndilo chaguo la wananchi wengi wa Zanzibar.
Kelele za Wazanzibari wanaouhiari muundo huo wa Muungano zimepaa na kusikika kote lakini kelele hizo hazitoshi. Ni muhimu pia kwamba Wazanzibari wajitokeze kwa wingi katika shehia zao na wajieleze bila ya pingamizi zozote, wakiongozwa tu na maslahi ya nchi yao na ya vizazi vijavyo. Wajiepushe kuwafuata wale wachache wanaoziona ‘amri za chama’ kuwa ni adhimu kushinda uzalendo na maslahi ya nchi.
 
Back
Top Bottom