CCM kuwabana Mnyika, Kafulila bungeni

RealMan

JF-Expert Member
Nov 9, 2010
2,367
1,388
WAKATI mkutano wa 11 wa Bunge ukitarajiwa kuanza keshokutwa mjini Dodoma, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinahaha kuzizuia hoja binafsi za wabunge wa upinzani zisijadiliwe bungeni ili kulinda masilahi ya kisiasa ya chama hicho na serikali yake, Tanzania Daima Jumapili limeelezwa.
Hoja hizo ni ile ya Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), inayotaka Bunge lijadili na kutoa mwongozo utakaoweka mchakato utakaowezesha kuandikwa na kuridhiwa upya kwa Katiba ya nchi.
Nyingine ni ile ya Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi) inayoitaka serikali itoe maelezo nchi imefikishwaje mpaka ikashindwa na Kampuni ya Dowans ambayo ilirithi mkataba ‘hewa’ kutoka kwa Kampuni ya Richmond.
Tayari wabunge hao kwa nyakati tofauti kila mmoja ameshawasilisha kwenye ofisi ya Bunge taarifa ya kutaka kuwasilisha hoja yake binafsi katika mkutano wa Bunge unaoanza keshokutwa.
Taarifa kutoka ndani ya CCM na ofisi ya Bunge zinasema chama hicho kwa kumtumia spika wa bunge, Anne Makinda ambaye ni mwananchama wake mtiifu, kimepanga kuizuia hoja ya Mnyika kuhusu katiba kwa kutumia njia kuu mbili; moja ni serikali kuwasilisha bungeni muswada wa sheria ya kuweka mchakato wa katiba na tume ya kuusimami na pili ni kuwatumia wabunge wake wawasilishe hoja ya Katiba kama Mnyika.
“Spika atasema hoja ya Mnyika haiwezi kujadiliwa kwa sababu analotaka kuliwasilisha tayari anaweza kulichangia katika muswada utakaowasilishwa na serikali bungeni kuhusu tume na mchakato wa katiba.
“Pili, watasema kuna wabunge wengine pia waliowasilisha hoja kama yake, sasa tumpe yupi, tumuache yupi….na muda hautoshi kujadili hoja zote na wala kanuni haziruhusu kujadili suala hilo hilo moja kwa hoja nyingi tofauti,” alifafanua kigogo mmoja wa CCM kwa sharti la kutotajwa jina lake.
Kuhusu hoja ya Kafulila itakavyozuiwa, taarifa kutoka ndani ya chama hicho zinasema, watatumia kisingizio cha suala la Dowans kuwa mahakamani ili kuzuia lisijadiliwe bungeni.
“Watasema Bunge haliwezi kujadili suala linaloshughulikiwa na mhimili mwingine wa dola (Mahakama)”, alisema mtoa taarifa wetu.
Hata hivyo, akizungumza na Tanzania Daima Jumapili, Kafulila, alisema msingi wa hoja yake ni kutaka kuangalia namna serikali ilivyoshindwa katika kesi hiyo wakati mkataba iliourithi Dowans una utata mkubwa wa kisheria na kwamba suala hilo haliwezi kwa namna yoyote ile kuingilia uhuru wa mahakama.
Alisema kuwa mazingira ya kesi yenyewe yanaonyesha kuwa hujuma zimefanywa katika uendeshaji huo ndiyo maana yeye amejipanga kuwasilisha hoja hiyo ili Bunge lijadili na kujua kwa kina kilichotokea kwenye kesi hiyo.
Alibainisha kuwa Tanzania ilishawahi kuvunja mkataba kibabe na Kampuni ya City Water ambayo ilipokwenda ICC ilishindwa pia lakini katika kesi ya Dowans inaonekana kuna mazingira yenye utata zaidi.
Alibainisha kuwa Rais Kikwete amekiri Richmond ilikuwa haina uwezo wa kuzalisha umeme hivyo mkataba wake ukawa batili hivyo katika mazingira hayo kampuni hiyo haiwezi kuirithisha kampuni nyingine mkataba usio halali.
“Hebu niambie Ndugu yangu kuna mwizi ameingia ndani na kuiba vitu, ukamuona na kuanza kumkimbiza, wakati ukikaribia kumkamata anaubwaga mzigo aliouiba, je, hutakwenda kumshitaki kwa sababu ya kuwa hukumshika na mzigo?” alihoji Kafulila.
Aliongeza kuwa hivyo ndivyo inavyofanya serikali ya CCM ambayo sasa imebanwa katika sakata la Dowans na inaamua kuuacha mzigo huo ili isikamatwe.
“CCM wamekwama kwa sababu wananchi, wanasiasa tumelipigia kelele suala wa malipo haya ya Dowans, sasa wanatafuta pa kutokea, Kikwete na watendaji wake hawawezi kukwepa kuwajibika.
Wajiuzulu ili tutafute viongozi na watendaji wengine ambao watakuwa mstari wa mbele kujali matatizo ya wananchi na kuyapatia ufumbuzi,” alisema.
Kuhusu hoja binafsi hiyo kupitishwa na Bunge linaloanza kesho kutwa, Kafulila alisema huu ndiyo mtihani mkubwa kwa Spika Anne Makinda na wabunge wa chama tawala kwa sababu hoja hiyo inagusa masilahi ya taifa.
Alisema kama Makinda atatumia ufundi wa kanuni kuzuia hoja hiyo basi ajue hasira za wananchi zitakuwa kubwa kwa chama tawala na pia tatizo la umeme halitaweza kupatiwa ufumbuzi wa kudumu.
“Ninachokifanya mimi ni kuangalia namna tutakavyotoka kwenye matatizo ya nishati ya umeme ambayo tuna mikataba mibovu pamoja na kutokuwa na umeme wa uhakika, wakifanya hila wataumia.
Alibanisha kuwa Kanuni ya 150 ya bunge, inaweka wazi kuwa Bunge linaweza kuvunja kanuni yoyote kwa ajili ya lengo la kutimiza jambo fulani lenye maslahi ya umma.
Kama kuna kanuni itakayozuia mjadala wa Dowans itabidi ivunjwe ili kuruhusu hoja hiyo kinyume na hapo mambo yatakuwa mabaya zaidi kwa CCM.
Alibainisha kuwa sekta nzima ya umeme ina upungufu, hivyo ni wakati mufaka kuweka mfumo utakaoliwezesha taifa kusonga mbele badala ya wajanja wachache kutumia matatizo ya wananchi kujinufaisha.
“Dowans ni sehemu ya hoja, mambo mengi yanapasawa kufanyiwa kazi, huu ndiyo mwanzo wa kujua mambo mengi,” alisema.


Source: Tz Daima
 
Kwa niwajuavyo CCM hawachelewi kulikoroga maana kifaa chao cha kupima joto kilishakufa.
Hawawezi kujua joto la kisiasa likoje nchini, watakurupuka kama walivyomfungia Zitto lakini baadae ikala kwao.
 
Back
Top Bottom