CCM inavyojimaliza yenyewe

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,906
22,049
Date::9/13/2008
Nape aendelea kukingiwa kifua, adai Nchimbi ana ajenda binafsi
Na Kizitto Noya
Mwananchi

SIKU moja baada ya Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Dk Emmanuel Nchimbi, kutoa taarifa kwenye vyombo vya habari kuwa Nape Nnauye amevuliwa uanachama kwa kosa la kusema uongo na si kuukosoa mkataba wa jengo la umoja huo, Nape amedai kuwa hali hiyo inaonyesha kuwa kiongozi huyo ana ajenda binafsi.

Nape aliiambia Mwananchi Jumapili kuwa, mjadala kuhusu adhabu yake umekwisha, hivyo hoja zinazoendelea kutolewa na UVCCM kuhusu suala hilo hazina msingi vinginevyo ni agenda binafsi za baadhi ya watendaji wa umoja huo.

''Uamuzi wa CC (Kamati Kuu) na NEC kutaka mkataba huo ukaboreshwe kwa kuwa una kasoro, unatosha kumaliza mjadala huo na kuthibitisha nani mkweli na nani mwongo, haya maelezo mengine ni ajenda binafsi za watu,'' alisema.

Alisema ajenda iliyoelezwa na Dk Nchimbi juzi kwamba, Baraza Kuu limemvua uanachama Nape kwa kosa la kusema uongo, haina mantiki kwani tayari vikao hivyo vya juu vya chama vimeshatoa taswira ya ukweli kuhusu suala hilo.

''Kimsingi vikao vya CC na NEC vimeshamaliza mjadala huo na hayo yanayoendelezwa sasa hayana maana, kwa kuwa tayari mwongo na mkweli wamejulikana,'' alisisitiza.

Alisema tangazo la Dk Nchimbi kwenye baadhi ya magazeti jana kwamba CC na NEC vimepitisha mkataba huo isipokuwa vimetaka nyongeza za vitu vichache, inapotosha kwani hiyo anayoita nyongeza ndizo kasoro alizokuwa (Nape) akizipigia kelele tangu awali.

Alibainisha kuwa kelele zake kuhusu mkataba huo hazikulenga kuwaharibia watu fulani ndani ya UVCCM bali kutetea haki kwa maslahi ya jumuiya yenyewe, hivyo si sahihi kwa baadhi ya watendaji kumwona kama ana chuki nao.

Juzi, Nchimbi alitoa taarifa kwa vyombo vya habari akieleza kuwa Nape amevuliwa uanachama wa UVCCM si kwa sababu ya kuukosoa mradi wa UVCCM bali kuudanganya umma na kukipaka matope chama kwa kusema uongo.

Alisema Nape alionekana kwenye televisheni akitoa tuhuma hizo kuwa, hakukuwa na vikao halali vilivyopitisha mkataba huo, wajumbe wa Baraza Kuu waliridhika kuwa aliwadanganya kwa kukana maneno hayo.

''Baraza Kuu liliridhika kuwa vikao vyote vya UV-CCM vinavyohusika na mchakato huo vilihusika kikamilifu, ikiwamo Baraza Kuu la tarehe 4/8/2007 na kikao kilichopitisha muhtasari wa Baraza Kuu cha tarehe 9/2/2008 ambacho Nape alishiriki,'' ameeleza Nchimbi katika taarifa yake.

Hata hivyo, Nchimbi anaonyesha katika maelezo yake kuwa uamuzi wa Baraza Kuu ulikuwa mkubwa kuliko mapendekezo yaliyotolewa na Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM, ambayo ilitaka Nape asimamishwe kushiriki vikao vya umoja huo na CCM imchukulie hatua za kinidhamu kwa mujibu wa taratibu zake.

Badala yake Baraza hilo lilimvua uanachama na kupendekeza kwa CCM avuliwe nyadhifa zake zote.

Katika taarifa hiyo Nchimbi alisema mapendekezo ya kumvua Nape nyadhifa zake zote ndani ya CCM ameshayawasilisha kwa Katibu Mkuu wa chama hicho tawala na kuwa "Uamuzi wa chama katika suala hilo utakuwa wa mwisho.

Katika hatua nyingine, wakati Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), ukitoa taarifa rasmi inayoeleza sababu za kumvua Nape Nnauye uanachama, kada na mwanzilishi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Peter Kisumo amesema, anachoona katika adhabu hiyo ni utoto na hasira za vijana.

Kisumo aliliambia Mwananchi Jumapili kuwa haoni sababu za Nape ambaye ni Mjumbe wa Baraza Kuu la UVCCM na Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) kuvuliwa uanachama kwa kusema uongo wakati hakuna ushahidi wa kutosha kuthibitisha hilo.

''Mimi ninachoona katika adhabu hiyo ni utoto na hasira za vijana na naamini busara haikutumika,'' alisema.

Alisema UVCCM inatakiwa kupinga hoja za Nape kwa ushahidi utakaoonyesha kuwa, mkataba wa uendelezaji wa jengo la UVCCM hauna harufu ya rushwa badala ya kumwadhibu Nape kwa tuhuma za kusema uongo.

''Hata kama Nape amesema uongo, adhabu ya kumvua uanachama bado ni kubwa na naamini adhabu hiyo imetolewa kwa ushawishi wa watu wenye hasira na jazba kuliko busara,'' alisema Kisumo na kuongeza:

''Nasema busara haikutumika kwani ingekuwapo wangetafuta adhabu nyingine inayolingana na kosa, tena baada ya kuthibitisha kosa lake kwa ushahidi badala ya kufukuzana.

Kwa mujibu wa Kisumo, adhabu ya kumvua mtu uanachama ni kubwa na haina tofauti na kumfukuza mtu uraia wa nchi yake na siku zote CCM imekuwa ikikwepa kutumia adhabu hiyo kwa kuwa inakidhalilisha chama.

Lengo la kulinda heshima yake na mwanachama anayeadhibiwa.''Kama Nape kasema ukweli au uongo, nasema adhabu hiyo sio mwafaka. UVCCM wanatakiwa kuleta ushahidi kutetea hoja zao badala ya kutumia adhabu hiyo ambayo inakidhalilisha chama na wanachama,'' alisema na kuongeza:

''Kama Nape alisema ukweli lakini ukweli huo kasemea nje ya vikao sioni sababu za kumwadhibu.''

Kisumo alisema haoni sababu ya mwanasiasa huyo chipukizi kuvuliwa uanachama wa UVCCM kama tuhuma kwamba, mkataba wa jengo la UVCCM hauna maslahi ni za kweli.

Alisema CCM inatakiwa kuweka mikakati kudhibiti jumuiya zake kuwafukuza wanachama ili kulinda heshima yake na wanachama ambao uzoefu umeonyesha kuwa wengi waliopata adhabu hiyo wanakihama.

Katika hutua nyingine Mzee Kisumo alisema Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba amekosea kulishawishi Baraza Kuu la UVCCM kumfukuza Nape uanachama kwa tuhuma za kusema uongo.

Alieleza kuwa Makamba aliteleza kwenda kuzungumza na vijana kwa lengo la kuwashawishi kufikia uamuzi huo kwa kuwa hii sio kazi yake.

''Kazi ya Katibu Mkuu ni kushauri na sio kushawishi na hatua ya Makamba kuzungumza na vijana ilikuwa ushawishi na sio ushauri hivyo ni makosa,'' alisema.

Alisema CCM imejengwa katika misingi ya kila jumuiya yake kujiongoza hivyo kitendo cha viongozi hao kuingilia mambo ya vijana ni kinyume na misingi hiyo na kinakiuka kanuni.

Kauli ya Mzee Kisumo imekuja huku tuhuma alizotoa Nape dhidi ya mkataba huo zikionekana kuwa na nguvu baada ya Kamati Kuu kuunda timu ya watu watatu kupitia upya mkataba huo uli kuondoa kasoro na kuufanya uwe na maslahi ya UVCCM

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuchukua fomu za kugombea uenyekiti wa UVCCM Julai 15, Nape, ambaye ni mtoto wa mwanasiasa aliyekuwa na heshima ndani ya CCM, Moses Nnauye, alidai kuwa mkataba huo unanuka rushwa na kumshambulia Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini la vijana, Edward Lowassa, mwenyekiti wa wake Dk Emmanuel Nchimbi na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Vijana, Amos Makalla kuwa walihusika.

Katika hatua nyingine, wakati UVCCM na CCM kupitia vikao vyao vya juu wanazidi kusisitiza kuwa mkataba wa jengo unaolalamikiwa haujasainiwa, mwekezaji katika eneo hilo anaendelea na ujenzi.

Mwananchi Jumapili jana lilishuhudia mafundi wa mwekezaji huyo wakifanya kazi kama mchwa licha ya kwamba mkataba wa uwekezaji huo unadaiwa haujatiwa saini.
 
Kama Roman Empire ilianguka sidhani mnyonge kama SISIEMU atahimili.

Labda ushauri zaidi kwa wanazuoni wa siasa UDSM tuambieni historia ya miliki na himaya zilizoanguka how they got fallen ili SISIEMU wabuni strategy za kuzuia zuia walu miaka miwili mitatu kwani na sasa tulipange hatutaki mwanachama kutoka SISIEMU na hata akija hatumpi madaraka yoyote zaidi ya mfagizi wa ofisi za chama. Tusifanye kosa wakaja huku side yetu tukajifi** tukawapokea tena itakuwa noma ileile.

We need to observe consistency and persistency
 
Back
Top Bottom