CCM hakukaliki; Makundi hasimu yazidi kukipasua chama

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
HALI ya mambo si shwari ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) hasa baada ya kuarifiwa kuwapo kwa mipango ya kuwang'oa vigogo wa chama hicho pamoja na kuisafisha Jumuiya ya Vijana (UVCCM).

Habari ambazo Tanzania Daima Jumapili imedokezwa ni kuwa baadhi ya viongozi wamekuwa wakiratibu mikutano ya siri pamoja na kutoa habari kwenye vyombo vya habari ili kuchochea harakati za kuwang'oa wenzao.

Harakati hizo zinadaiwa kuchagizwa zaidi na utashi wa kutaka Ridhiwan Kikwete, ambaye ni mtoto wa Rais Kikwete na waomuunga mkono wavuliwe uongozi kwenye baraza la utekelezaji la UVCCM, ambalo linadaiwa limekuwa likiendeshwa kwa matakwa ya kundi fulani.

Wakati hali ya mambo ikionekana kuwa si shwari kwa UVCCM, CCM nako vigogo wamekuwa wakituhumiana kuwindana na kuchafuana ili kujitafutia uungwaji mkono kwenye uchaguzi wa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) na Kamati Kuu (CC).

Mbio hizo zimeshamiri zaidi hivi sasa ikiwa ni ishara ya vigogo wa chama hicho kujiandalia mazingira ya kuwania nafasi ya urais mwaka 2015 au kuwasimamisha wagombea wanaowahitaji.


Harakati hizo hivi sasa zinaonekana kukiathiri zaidi chama hicho kwa kuwa hakuna kiongozi anayeweza kusimama na kuwakemea wenzake, hasa wale wanaoonekana kukiyumbisha chama.

Baadhi ya vigogo wa chama hicho ambao mara kwa mara wamekuwa mstari wa mbele kupinga hali ya mambo inavyoendeshwa ndani ya chama hicho wameweka wazi kuwa Rais Kikwete amekuwa sehemu ya kuyumba kwa chama hicho kutokana na kushindwa kuchukua hatua zinazostahili.

Hoja wanazozijenga vigogo hao ni kuwa Rais Kikwete anashindwa kuchukua uamuzi wa kuwafukuza au kuwaonya wanachama hao kutokana na ukaribu alionao huku wengine ikidaiwa ndio waliochangia kwa kiasi kikubwa ushindi wake mwaka 2005 na 2010.

Wakati hali ikionekana kutotulia ndani ya chama hicho, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT), Sofia Simba, amesema hivi sasa nchi ipo katika msukosuko wa kisiasa na kuwataka makada wenzake kutokaa kimya kujibu hoja na mashambulizi ya wapinzani.

Kauli hiyo aliitoa jana jijini Dar es Salaam, alipokuwa akifungua mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa, ambapo alisema hivi sasa nchi ipo katika kipindi cha mpito (msukosuko) ambacho anaamini serikali ya CCM itakivuka.
"Tunapita katika kipindi cha rasharasha, na si wakati mgumu, ila msukosuko wa kawaida wa kisiasa, ni lazima tujibu kila hoja yenye kupotosha ukweli, hasa zinapokuwa zinatolewa na vyama vya upinzani.

"CCM ndiyo mshindi katika uchaguzi wa mwaka jana na ndani ya miaka minne tunatakiwa kuhakikisha tunaweza kupata ushindi katika uchaguzi wa serikali za mitaa, kwa kuimarisha umoja wetu sisi wanawake ni imara katika nchi hii," alisema Simba.

Simba, alisema katu hatakaa kimya kwa kuogopa hoja na yupo tayari kujibu kila hoja zinazotolewa na viongozi wa vyama vya upinzani.

"Nipo imara na UWT ipo imara katu hatutishwi na chama chochote cha siasa na wala hatuogopi vitisho vyao, nami kiongozi wenu nitapambana kwa masilahi ya UWT na CCM kwa ujumla.

"Katu hatutatumia nguvu wala kufanya maandamano ila tutaimarisha umoja wetu ndani ya CCM, kwani hii ndiyo silaha kubwa ya ushindi katika uchaguzi wa mwaka 2015 ili CCM iendelee kutawala nchi," alisema Simba.

Mkoani Dodoma, Mwandishi Wetu, anaripoti kuwa Rais Kikwete amewaomba viongozi wa dini kuwa karibu na serikali katika kutatua migogoro mbalimbali ambayo inaweza kuleta mgawanyiko na machafuko katika nchi.

Kauli hiyo aliitoa alipokuwa akitoa salamu kwa viongozi wa dini na washirika walioshiriki katika sherehe za kumsimika Askofu wa Jimbo la Katoliki Dodoma, Gervas Nyaisonga, zilizofanyika katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo mjini hapa.

Kikwete alisema kuwa viongozi wa dini ndio pekee wanaoweza kunusuru nchi kwa kutoa elimu ya kutosha kwa waumini wao juu ya wanavyotakiwa kuishi, kuheshimu mamlaka zilizopo pamoja na kushirikiana nazo.

Alisema kuwa viongozi wa dini wana uwezo mkubwa na ushawishi wa kutosha katika kuisaidia serikali kwa kiasi kikubwa, kwa kuweza kuwaunganisha wanasiasa na kuweza kukaa meza moja na kuzungumzia mambo ambayo yana masilahi ya nchi badala ya kuendesha siasa za chuki na ukabila.

Naye Rais wa Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania, Thadeus Ruhaichi, ameitaka serikali kuendesha taifa kwa misingi ya umoja , amani, utulivu na mshikamano badala ya kuligawa taifa katika misingi ya udini na ukabila.

Nacho Chama cha Wananchi (CUF) jana kimeanza mikutano ya hadhara katika mikoa ya Tanga, Lindi, Mtwara, Pwani, Dar es Salaam na Unguja, kwa lengo la kuishitaki serikali ya CCM kwa wananchi.

CUF inaishitaki serikali ya CCM, kwa kushindwa kuboresha maisha ya wananchi wake na kusababisha mgawo wa umeme, kupanda kwa gharama za maisha, matatizo ya sekta ya afya, miundombinu mibovu na matatizo ya elimu.

Mikutano hiyo ya CUF na mambo wanayoishitaki serikali kwa wananchi yanafanana kwa kiasi kikubwa kama kile kilichokuwa kikifanywa na Chama cha Demokarasia na Maendeleo (CHADEMA) ambacho kilionekana kinafanya uchochezi.

CUF haifanyi maandamano kama ilivyokuwa kwa CHADEMA, ambayo ilijiwa juu na viongozi wa vyama vya siasa na watendaji wa serikali kuwa inafanya uchochezi kwa kuwashawishi wananchi waichukie serikali iliyopo madarakani kinyume cha Katiba na sheria. Mikutano hiyo ya CUF itakuwa ikiongozwa na Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba, wabunge na viongozi wa chama hicho.
 
Cuf wakifanya mikutano wao hawaleti uvunjufu wa amani lkn cdm wakianza tu wao wanaleta uvunjifu wa amani, ama kweli cuf=ccmB
 
UVCCM msifanye na msijejaribu kufanya mnachotaka kukifanya. hakuna zaid ya Riz1 tena ikibidi tumpe uenyekiti ili na yeye atuongoze kama baba yake. Mbona sioni shida yake? Mkome msifanye ujinga mnaotaka kuufanya.
 

Similar Discussions

0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom