Bill
JF-Expert Member
- Oct 5, 2007
- 8,277
- 8,492
Mwenyekiti wa Taifa wa Chama Cha Jamii (CCJ), Richard Kiyabo (kulia), akiangua kilio baada ya yeye na Katibu Mkuu wake, Renatus Muabhi, kuweka mashada ya maua kwenye kaburi la hayati Baba wa Taifa, Mwalimu JK. Nyerere, Butiama mkoani Mara jana.
*Wabubujikwa machozi kaburini kwake
*Wahutubia hadhara, kadi kama njugu
Viongozi hao walikutana na mkuu wa familia hiyo, Chifu wa Wazanaki, Japhet Wanzagi na mmoja wa watoto wa Mwalimu, Madaraka Nyerere.
Viongozi wa CCJ waliotembelea familia hiyo ni Mwenyekiti, Richard Kyabo na Katibu Mkuu, Renatus Muabhi.
Mbali na Chifu Wanzagi na Madaraka, mazungumzo hayo pia yaliwahusisha wazee mashuhuri wa kijiji cha Butiama.
Katika mazungumzo hayo, Chifu Wanzagi alionekana kutoridishwa na jinsi sera ya ubinafsishaji ilivyoshindwa kuwaondoa Watanzania katika dimbwi kubwa la umaskini.
Alisema kuwa ubinafsishaji huo ungefanyika wakati wa Mwalimu Nyerere, asingevumilia hali hiyo.
Chifu Wanzagi alisema ingawa yeye ni mwana-CCM damu ambaye hawezi kukihama chama hicho kikongwe, lakini sera ya ubinafsishaji imeshindwa kabisa kuwasadia Watanzania kuondoka katika umaskini.
"Mimi ni mwa-CCM, lakini kwa kweli sijui leo Mwalimu (Baba wa Taifa) angekuwepo angesema nini. Haiwezekani nchi ikatoa madini kwa watu wa nje, tena kwa bei poa huku wananchi wanaozunguka migodi hiyo wakikabiliwa na umaskini mkubwa, jambo hili linatusikitisha sana," alisema Wanzagi, ambaye pia ni msemaji wa familia hiyo.
Alipongeza uanzishwaji wa chama hicho kwa kutambua kuwa kila Mtanzania ana haki ya kuchagua kujiunga na chama chochote cha siasa chenye lengo la kuleta mabadiliko katika nchi bila kuathiri umoja wa kitaifa.
Naye Madaraka alisema Butiama ni eneo la kila Mtanzania kwa kuwa ndipo alipozikwa Baba wa Taifa, hivyo kila mtu au chama cha siasa kina haki ya kufika na kutoa heshima katika kaburi la kiongozi huyo.
"Butiama ni ya Watanzania wote, hivyo kila chama au mtu ana haki ya kufika kwa lengo la kuona kazi mbalimbali zilizofanywa na Baba wa Taifa wakati wa uhai wake, ambazo zimehifadhiwa katika makumbusho yake na kuona sehemu alipozikwa," alisema na kuongeza:
"Tena bila ya ubaguzi wowote, kama mwenyewe alivyokuwa akituasa Watanzania leo na kesho kuwa wamoja na kabila lao ni Tanzania."
Kyabo alisisitiza kuwa lengo kuu la kuanzishwa kwa chama hicho ni kuhakikisha kinaenzi mema yote yalipiganiwa na Baba wa Taifa kwa maslahi ya Watanzania wote ingawa sasa yameonekana kusaulika.
Alisema ndani ya CCJ, rushwa na ufisadi ni ajenda ya kwanza ambayo itasimamiwa kikamilifu.
Alisema vitendo hivyo vilionekana wazi kumkera Baba wa Taifa kutokana na kusababisha kuwepo kwa baadhi ya watu wachache wanaonufaika na rasilimali za nchi huku idadi kubwa ya Watanzania ikiwa katika lindi kubwa la umasikini.
"Leo tumekuja kuona mahali alipompumzishwa mwasisi wa Taifa la Tanzania ikiwa ni uzinduzi wa safari yetu ya nchi nzima kuelezea misingi yote iliyowekwa na Baba wa Taifa kwa nchi hii kwani CCJ inathamini kwa dhati michango hiyo, hiyo ndio sababu tumekuja kuwaeleza kuwa Mwalimu tutamtumia kila kona ya nchi yetu," alisema mwenyekiti Kyabo.
Naye Muabhi alisema kushamiri kwa vitendo vya rushwa na ufisadi kunatokana na maamuzi ya viongozi wa CCM kukiuka misingi mizuri iliyoasisiwa na Baba wa Taifa kwa kuanzisha Azimio la Arusha ambalo walidiriki kuliua ili kupata mwanya wa kujineemesha.
"Narudia kuwajulisha kuwa CCJ tunathamini sana misingi iliyowekwa na Baba wa Taifa katika uongozi wa nchi hii, ndio maana tutatumia nguvu zetu zote kuirejesha kupitia CCJ baada ya wao kuua Azimia la Arusha, baada ya kubaini linawaumbua," alisema.
Hata hivyo, viongozi hao walionekana kububujikwa machozi wakati wakiweka mashada ya maua katika kaburi la Hayati Mwalimu Nyerere, hali ambayo iliamsha simanzi kubwa kwa baadhi ya wananchi na wazee wa kijiji cha Butiama waliofika kuonana na viongozi hao.
Baadaye viongozi hao walifanya mkutano wa faragha ndani ya nyumba ya Baba wa Taifa kati yao na Madaraka na Chifu Wanzagi. Hata hivyo, baada ya kukutana, wote walikataa kueleza kilichozungumzwa kwa zaidi ya nusu saa.Baada ya kutoa kijijini Butiama, viongozi hao wa CCJ walikwenda katika mtaa wa Bugharanjabho, Kata ya Buhare katika Manispaa ya Musoma na kutoa pole kwa familia tatu zilizokumbwa na mauji ya ndugu zao 17 waliouawa kikatili kwa kukatwa mapanga usiku wa Februari 16, mwaka huu.
Na katika hatua nyingine, umati wa wakazi wa mjini hapa na vitongoji vyake, jana walijitokeza kununua kadi za CCJ wakati wa mkutano wa uzinduzi wa chama hicho uliofanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi Mkendo.
Mkutano huo uliohutubiwa na viongozi wa kitaifa wa chama hicho na kuhudhuriwa na idadi kubwa ya vijana, wafanyabishara na baadhi ya wananchi wa kawaida.
Wananchi walikuwa wakiimba kuwa sasa ni wakati wa ukombozi kutokana na kujinasua kutoka katika makucha ya wakoloni.
Aidha, katika mkutano huo, wananchi hao walimchagua Mwenyekiti wa muda wa CCJ mkoani Mara, Sospiter Manumbu, ambaye atasimamia shughuli zote za chama hicho ikiwemo kutafuta ofisi rasmi ya mkoa na kufungua ofisi za wilaya mkoani Mara.
Licha ya mkutano huo kumalizika saa 12:00 jioni, bado kulikuwa na mamia ya wananchi waliokuwa wamefoleni katika viwanja vya Shule ya Msingi Mkendo wakisubiri kununua kadi za chama hicho kipya.
CHANZO: NIPASHE