Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
Na. M. M. Mwanakijiji (Tanzania Daima)
MARA baada ya Rais Kikwete kumaliza kuhutubia hotuba yake iliyokuwa inangojewa kwa hamu na Watanzania, nilijikuta katika mawazo yangu yaliyopotoka nikimuona Rais Kikwete kama baba wa ule mchezo wa utotoni wa watoto wangu eh!
Niliweza kumuona upande mmoja Rais Kikwete akiwa amesimama na kuwaangalia Watanzania na huku akijibizana nao katika kuwatahadharisha kuhusu simba aitwaye fisadi. Ilikuwa hivi:
JK: Watanzania eh
WTZ: Eh
JK: Mimi Rais wenu!
WTZ: eh!
JK: Sina nguvu tena!
WTZ: Eh
JK: Ya kukamata mafisadi
WTZ: Eh
JK: Mafisadi ni wajanja
WTZ: Eh
JK: Wamekomba Benki Kuu Watoto wanaendelea kuitia Eh kwa shauku!
JK: Wamelangua na Rada
Wameiba Meremeta
Wamechota nayo EPA
Na makampuni mengine
Sasa kimbieni!
Watanzania kila mmoja anavyojua anaanza kutimkia kwake na kufanya mambo yake kuokoa maisha yake na ya familia yake. Kwa hakika hivyo ndivyo nilivyomuona Rais Kikwete.
Katika makala yangu ya wiki iliyopita yenye kichwa cha habari: Macho ya Taifa yanakutazama Kikwete, nilisema kuwa hotuba ya Rais Kikwete inaweza kuwa ni ya kuleta matumaini au ya kukata matumaini.
Na nilisema kati ya mambo mengi ambayo wananchi walikuwa wanasubiri kuyasikia ni suala la Zanzibar na maamuzi ya suala la EPA.
Kuhusu Zanzibar nilisema kuwa: La maana katika kujadili matatizo ya ndoa yetu ni kusema kuwa kwanza ndoa ipo na halali; kwamba Muungano upo na halali.
Na la pili ni kukubali on principle and in fact kuwa zile nchi mbili zilizoungana hazipo tena (siyo kuwa moja ipo nyingine haipo) na kilichopo ni nchi moja.
Ni kutoka hapo ndipo mjadala wa kero za Muungano unaweza kufanyika. Hili la kusema ati mmoja bado ni nchi na mwingine siyo nchi ni kuzugana. Je, Rais Kikwete alikisema hiki?
La hasha! Rais Kikwete alijaribu kwa kiasi kikubwa kujibu suala la Zanzibar ni nchi au si nchi lakini kwa kufanya hivyo akawa amejiingiza kwenye tatizo jingine. Kwa maoni ya Rais katika mambo yetu ya nje na mahusiano na mataifa mengine nchi ni Tanzania. Katika mambo yetu wenyewe nchi ni Zanzibar na nchi ni Tanganyika.
Kwa maneno mengine Rais wetu anaamini kuwa kuna nchi tatu! Kuna nchi moja ambayo ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ndani yake kuna nchi mbili, ambazo bado zipo nazo ni Zanzibar na Tanzania.
Hili linapinga kauli yake ya awali kwenye hotuba hiyo kuwa nchi hizo mbili zilisalimu mamlaka yake na kuunda nchi moja Aprili 26, 1994.
Kwamba nchi ya Zanzibar na nchi ya Tanganyika ziliamua kutoweka ili kujenga nchi moja yenye mamlaka yote ya nchi (sovereignty).
Rais Kikwete alishindwa kuitetea Katiba kwa kuweka wazi kuwa nchi hiyo moja (kwa mujibu wa Katiba Ibara 1- 4) inaongozwa na serikali mbili (si nchi mbili).
Katiba inaeleza wazi kuwa nchi hiyo moja iitwayo Tanzania, inaongozwa na Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, si Serikali ya nchi ya Tanganyika na Serikali ya nchi ya Zanzibar.
Sasa haya siyo maneno ya Mwanakijiji, bali ndivyo ilivyo katika mkataba wa Muungano ambapo inasemwa hivi: Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar zitaungana na kuwa Jamhuri moja ya hakimiya.
Na katika mkataba huo huo unaelezea kuwa Rais wa Zanzibar atakuwa ndiye msaidizi wa Rais wa Jamhuri katika kuendesha na kusimamia Serikali ya Zanzibar.
Hivyo mkataba wa Muungano wa awali ulimweka Makamu wa Rais wa Muungano (kati ya makamu wawili) kuwa ndiye atakuwa Rais wa Zanzibar.
Sitaingia kwa undani suala hilo, lakini ukweli ni kuwa walioboronga na kuharibu ni pale wakati wa kuandika Katiba ya Kudumu mwaka 1977 na mabadiliko yake ya 1984, ndipo walipovikoroga vipengele vya Muungano wetu.
Ni hapo ndipo tulipoanza kupotea kweli kweli na ndipo ambapo sisi wengine tuliamini kuwa Rais Kikwete angeweza kuonyesha njia ya kurudia.
Hakufanya hivyo na badala yake kudai kuwa nchi ya Tanganyika nayo ipo, kitu ambacho wote tunajua haipo (isipokuwa kwenye mawazo ya Mtikila na Watanganyika wengine).
Lakini Kikwete alisema kweli pale alipohamaki kuwa kama kuna jingine waliseme wale wanaoendeleza mjadala huu.
Kitu ambacho mimi niliandika wazi kwenye makala ile na kusema wanachogombea Zanzibar si nchi au ni nchi, kwa sababu Mkataba wa Muungano upo na unajulikana.
Wanachogombea nilisema ndugu zetu wa Zanzibar wanapigia kelele kuwa si nchi, wanachogombania kwa kweli ni kuwa nchi kamili, kisheria na kwa kila hali.
Na nikisema kama mtu haamini maneno yangu, Rais Kikwete asikike akitangaza kuwa Tanzania ni nchi moja na Zanzibar ni sehemu ya Muungano, si nchi.
Zanzibar hakutakalika, kwani CCM Zanzibar itameguka kutoka Bara, watashikamana na CUF na kwa pamoja watatangaza nchi huru.
Kikwete hakuwa na ujasiri wa kusema embe ni embe na chungwa ni chungwa, licha ya uwezo na mamlaka yote kuwa nayo. Akabakia kulia tu sina nguvu tena.
Kwenye suala la EPA niliandika hivi wiki iliyopita hata kama Rais Kikwete atatangaza hatua dhidi ya watu na makampuni yaliyochukuliwa hatua, kufilisiwa au kurudisha fedha, ukweli utabakia kuwa pongezi hizo atazipata Kikwete.
Nilisema hivyo kwa sababu kina Mwanyika walishindwa kufanya walichoagizwa na Rais kufanya.
Na leo tumesikia Rais Kikwete akitangaza kwa majigambo kuwa watuhimiwa hao wamenyanganywa pasi zao za kusafiria, magari na majumba na ati wana hali mbaya kweli.
Katika mawazo yetu ya kupenda kuzugwa tukashangilia na kupiga makofi. Hatukujiuliza hayo magari yaliyofilisiwa yameegeshwa wapi? Wapiga picha huru waonyeshwe magari hayo! Vinginevyo yamefilisiwa na kupigwa mnada na walionunua ni wakuu wengine wa serikali!
Yaani vyawezekana vimetoka kwa fisadi huyo kwenda kwa potential fisadi.
Hatukujiuliza hayo majumba yaliyokamatwa yako vitalu gani, maana hata kibanda cha nyasi nacho ni nyumba!
Leo hii makundi ya watu wamevaa njano na kijani wanaandamana kuunga mkono maneno. Wakati wengine tulifunga safari kutembea miguu kuunga mkono Azimio la Arusha lilioendana na vitendo thabiti leo hii kwa kupenda kuzugwa tumejikuta tunaandamana kushangilia maneno na si vitendo.
Tunakumbuka tulivyoimba wakati ule mabepari walia, mabepari walia, kukatiwa mirija, walipotangaziwa, walipotangaziwa Azimio la Arusha.
Hivi baada ya hotuba ya Kikwete mnafikiri kuna fisadi yeyote analia kwa sababu amekatiwa mirija ya ufisadi?
Rais amebakia kusema tu mimi rais wenu, sina nguvu tena.
Lakini cha kufurahisha zaidi ni pale alipodai kuwa ana nguvu za kumsweka mtu yeyote ndani na maswali baadaye.
Walio waoga wakaamini maneno hayo. Wapo walioamini kuwa Rais wa Tanzania ana nguvu ya kuamuru Mtanzania akamatwe pasipo sababu yoyote na nje ya sheria.
Yaani rais aote ndoto mwanakijiji anamboa halafu kesho yake asema mkamateni mwanakijiji!
Nguvu hizo hana, hajawahi kuwa nazo katika Tanzania huru, na kama kuna mtu amemdanganya kuwa anazo, huyo mtu atimuliwe kazi!
Rais wa Tanzania ana nguvu ambazo tumempatia kikatiba na kisheria.
Nje ya hapo hana nguvu zozote zile. Mahali pekee ambapo Rais wa Tanzania anaweza kujihisi dikteta ni pale atakapotumia sheria ya madaraka ya Rais wakati wa hatari (Emergency Powers Act) ya mwaka 1986.
Hata hivyo pamoja na sheria hiyo, nayo inaweka mipaka ingawa inampa rais uwezo mkubwa sana.
Hata hivyo nguvu hizo zinaingia tu pale ambapo rais ametangaza hali ya hatari, na kwa kadiri ninavyojua mimi Tanzania haijatangazwa hali ya hatari.
Sasa kama kina Mwanyika wamemzuga Rais kuwa ana nguvu za kufanya lolote kwa kutumia sheria hiyo pasipo kutangaza hali ya hatari na wao wakaenda kuwanyanganya watu mali zao na hati zao kwa sababu Rais kaagiza, naamini ni kinyume cha sheria na wale ndugu walionyanganywa mali zao wana haki ya kwenda mahakamani kudai warudishiwe.
Sasa ninaelewa kwa nini serikali haikutaka kwenda mahakamani.
Inaogopa kuumbuliwa. Mara nyingi serikali imekuwa ikidai kama una ushahdi wa ufisadi wa mtu nenda mahakamani. Leo hii wao wana ushahidi mkubwa wa wizi wa EPA na mambo mengine lakini wamekuwa wa kwanza kukwepa mahakama.
Wakati sisi vidagaa tunaambiwa tukiwa na ushahidi dhidi ya kiongozi yeyote basi twende mahakamani, wao ambao wana ushahidi wa wizi, kughushi, na matumizi mabaya ya madaraka wanakwepa mahakama hizo.
Sababu kubwa na ya kipuuzi ni kuwa ati wakienda mahakamani watuhumiwa wanaweza kushinda kesi na fedha zisirudishwe na wao wasikutwe na hatia.
Hii ni sababu ya kijinga kwa sababu mahakama ndio mahali ambapo ukiwa na mashtaka dhidi ya mtu, ukweli utachambuliwa ili kuona haki inapatikana.
Kama utashindwa kuthibitisha kuwa alifanya unachodai kufanya, basi ni kosa lako wewe mwenyewe na watu wakifunguliwa ndio utawala wa sheria.
Si wengi tunakumbuka kisa cha kada wa CCM kule Arusha aliyetuhumiwa kufanya ujambazi, mahakama ya chini ikamuona kuwa na hatia na baadaye mahakama ya juu ikaamua kumuachilia kutokana na ushahidi dhaifu.
Si tunakumbuka kesi ya Rage na jinsi alivyoanza kutumikia kifungo na baadaye kuachiliwa? Si tunakumbuka kesi ya Nalaila Kiula, ambaye naye baada ya kudaiwa kuwa ni fisadi, alijikuta akiachiliwa na mahakama?
Jamani, hivyo ndivyo mahakama zinatakiwa kufanya kazi.
Kwa serikali kutokwenda mahakamani imeonyesha kuwa inatafuta haki kwa upendeleo au uonevu.
Serikali ikienda mahakamani mashahidi wataitwa, ushahidi utawekwa hadharani, na watuhumiwa wataweza kujitetea na pia kuwahoji wanaowatuhumu, hiyo haki ya mtu kufikishwa mahakamani (Habeas Corpus) ni haki ya msingi.
Lakini serikali yetu inaonekana wameamua kwenda nje ya utawala wa sheria.
Naamini wale wanaotuhumiwa kuiba EPA wataaamua kufanya kile ambacho serikali haitaki kufanya, nacho ni kwenda mahakamani kupinga maamuzi hayo ya serikali.
Hatuwezi sisi kama taifa kukubali kuwa na mifumo sambamba ya sheria ambapo mwizi wa kuku anakamatwa na kufikishwa mahakamani na haambiwi aende kutafuta kuku mwingine arudishe bali anakutana na mkono mrefu wa sheria wakati walioiba mabilioni ya EPA wanapewa karibu miezi nane ya kutafuta fedha na kuzirudisha.
Lakini wakati huo huo Rais anasema ana mamlaka makubwa.
Yaani ana mamlaka makubwa ya kushindwa kuagiza sheria ifuatwe, yaani ana mamlaka makubwa ya kukubali kupokea ripoti ya kitu ambacho hakuagiza, yaani rais wetu ana mamlaka makubwa ya kutuzuga, tukazugika!
Kilichonishangaza mimi zaidi ni jinsi gani baadhi yetu wanapenda na wanafurahia mazingaombwe.
Niliandika siku chache kabla ya hotuba kule kwenye mtandao wa Jamiiforums.com kuwa mwishoni mwa wiki mtasikia watu wakiandamana kupongeza hotuba ya rais.
Niliyasema hayo kabla ya kusikia hotuba yenyewe! Sikuhitaji kuisikia na sikuhitaji kukisia mwitikio wa watu.
Ni jambo ambalo sasa hivi tunalielewa ni hulka ya Watanzania. Tumeacha kushangilia vitendo na sasa tumebakia kushangilia maneno.
Na wiki hii yote mtaendelea kusikia mikoa mbalimbali na jumuiya mbalimbali zikipongeza hotuba ya rais na sitashangaa mtaona kwenye magazeti wakianza kutuma salamu za pongezi kwa hotuba.
Watasimama watetezi wa maneno kuwa hotuba ilikuwa ni nzuri, imekuja wakati muafaka, na imeonyesha kuwa Kikwete yuko makini! Kumbe walichofanyiwa ni mchezo wa watoto wangu eh!
Yaani Watanzania tunaambiwa kuwa Tanzania sasa si kichwa cha mwendawazimu, bali ni kinyozi, tunaandamana kushangilia ingawa wenyewe tumeshuhudia kuwa tunashindwa hata kulinda goli letu moja hadi tunafungwa na golikipa! Wenyewe tunasema tumefanikiwa katika soka.
Binafsi ningeona Watanzania wameamka kama wangeunga mkono maneno machache aliyosema Spika Sitta ambayo ilikuwa ni kuwaambia wenye mamlaka ukweli (speaking truth to power).
Maneno ya Spika ya dakika saba ndiyo ambayo wengi wetu yalitupa faraja na matumaini kuliko maneno ya saa tatu na nusu ya rais.
Rais angeweza kusema alichosema ndani ya saa moja na mafanikio ya serikali yake angemuachia Waziri Mkuu atakapoahirisha Bunge baadaye siku chache zijazo.
Sasa namuonea huruma Pinda sijui na yeye ataimba sifa gani za Serikali ya Awamu ya Nne.
Nasema tukubali tu yaishe. Tukubali kuwa miaka miwili na nusu iliyopita tumeuziwa mbuzi kwenye gunia na tulichopata ndicho tunachostahili.
Tukubali ya kwamba miaka miwili ijayo haitakuwa tofauti na iliyopita, kwani kama wameshindwa kumkunja samaki angali bado mbichi wataweza akikauka?
Tukubali kuwa tulifanya makosa tulipomchagua Kikwete na sasa aidha tuangalie humo humo CCM au nje yake, mtu ambaye ataliongoza taifa letu kwenye neema ifikapo 2010.
Mwenzenu nimeshaamua kuwa mhula mmoja wa utawala wa Kikwete unatosha. Tumuombee uzima na afya, ili aendelee kuitawala nchi yetu kwa amani, umoja na mshikamano.
Tumuombee aendelee kuvuta muda hivyo hivyo na ufisadi ili hatimaye wananchi wauchoke kweli kweli.
Na tumuombee kuwa ifikapo 2010 atatambua kuwa hana sababu ya kugombea tena urais, na yeye mwenyewe kwa kutumia hekima na busara ataamua kumpisha mwana CCM mwingine au rais mwingine kutuongoza kwenye neema ya kweli.
Inawezekana ni kweli yeye ni chaguo la Mungu, saa na wakati huu ili kutuonyesha Watanzania kuwa kuanguka kwa CCM kumeanza. Yawezekana kama vile Farao alivyosimamishwa na moyo wake kufanywa mgumu ili wana Waisraeli waondoke Misri kwa mkono wa maajabu wa Mungu.
Yawezekana Kikwete naye amesimamishwa ili Watanzania hatimaye tuuone ukuu wa Mungu. Kwani na sisi tunastahili nchi ile ya ahadi, inayotiririka maziwa na asali, ambapo mafisadi hawawezi kukinga mikono tena kuchota.
Hata hivyo Kikwete bado anaweza kuokoa urais wake na kujipa nafasi nyingine. Nitakuambia wiki ijayo kwa vipi.
Watanzania eh!
NB: Asante Said Michael kwa kuchora katuni hii kwa muda mfupi. Ubarikiwe. Kazi zake nyingine zinaonekana kwenye kijarida na kwenye bulogu yake HAPA