BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,007
Spika azima hoja binafsi
na Charles Mullinda, Dodoma
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
na Charles Mullinda, Dodoma
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
SPIKA wa Bunge, Samuel Sitta, jana alizuia kuwasilishwa bungeni kwa hoja binafsi tatu zilizokuwa zimewasilishwa kwake na wabunge.
Spika Sitta alitangaza uamuzi wake wa kuzuia kuwasilishwa kwa hoja hizo wakati akitoa matangazo bungeni baada ya kumalizika kwa kipindi cha maswali na majibu.
Aidha, Spika Sitta pia alizuia kusomwa kwa taarifa ya serikali kuhusu mgodi wa Kiwira kwa kile alichoeleza kuwa yapo masuala yaliyowasilishwa na Kamati ya Nishati na Madini ambayo serikali inahitaji muda wa kuyajibu kabla ya kuileta hoja hiyo bungeni kujadiliwa.
Hoja binafsi zilizozuiliwa ni pamoja na iliyowasilishwa na Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed (CUF) akitaka kuwepo kwa mabadiliko ya vifungu katika katiba, vitakavyoweka ukomo wa ukubwa wa serikali.
Akitoa sababu za kuizuia hoja hiyo, Sitta alisema haiwezi kujadiliwa kwa vile inaingiliana na marekebisho ya Katiba.
Alisema Ibara 98 ya Katiba inaeleza kuwa jambo kama hilo, linahitaji kushughulikiwa kwa kuwasilisha muswada bungeni na si kuwasilishwa na mbunge mmoja kama hoja binafsi.
Hoja nyingine ni ile iliyowasilishwa kwake na Mbunge wa Karatu, Dk. Wilbrod Slaa, iliyokuwa ikitaka maelezo ya serikali kuhusu madai ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Laurence Masha, kuingilia mchakato wa utengenezaji wa vitambulisho vya taifa kinyume cha Sheria ya Manunuzi ya Serikali.
Alisema baada ya kuipeleka hoja katika Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, ambako ilijadiliwa na yeye kupewa ushauri, amekubaliana na ushauri wa kamati hiyo kuwa litakuwa jambo la busara mchakato wa zabuni hiyo kuendelea, kwani umekwisha kuchelewa.
Alisema baada ya mchakato huo kukamilika na kama kutakuwa na malalamiko kuhusu zabuni hiyo ilivyoendeshwa, jambo hilo linaweza kurejeshwa bungeni na kujadiliwa ili kuona ni nani alikosea.
Hoja ya tatu iliyozuiliwa na Spika Sitta ni ile iliyowasilishwa na Mbunge wa Viti Maalumu, Halima Mdee (CHADEMA) iliyohusu mgogoro katika eneo la Chasimba, mkoani Dar es Salaam.
Spika Sita alieleza kuwa ameridhika kuwa shauri hilo liko mahakamani hivyo haliwezi kujadiliwa bungeni.
Kabla ya kutangaza kuzuiwa kwa hoja hizo, Spika alisema Mbunge wa Muleba Kusini, Wilson Masilingi (CCM), aliondoa mwenyewe hoja yake iliyohusu uwajibikaji wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa katika halmashauri, baada ya kushauriana na kukubalika kuwa huu si wakati muafaka wa kuiwasilisha.
Wakati huo huo, Spika Sitta alieleza kuwa kutojadiliwa kwa taarifa ya serikali kuhusu utekelezaji wa maazimio mbalimbali ya Bunge iliyowasilishwa jana, kumetokana na taarifa hizo kuendelea kufanyiwa kazi.
Taarifa hizo ni ya zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura ulioipa ushindi Kampuni ya Richmond Development ya Houston, Marekani, uendeshaji usioridhisha wa Shirika la Reli Tanzania (TRL) unaofanywa na Kampuni ya Rites ya India.
Nyingine ni kuhusu utendajii wa kazi usioridhisha wa Kampuni ya Tanzania International Container Terminal Services (TICTS) na taarifa kuhusu uendeshaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL).
Chini ya kanuni 37 kifungu cha 9 cha Bunge, Spika alisema aliziangalia taarifa hizo na kuona kuwa kuzijadili ni kupoteza muda na hivyo akaamua yachukuliwe maelezo ya kamati za Bunge, yawakilishe maoni yao.
Hata hivyo aliwaambia wabunge kuwa uamuzi huo hauzuii katika mkutano ujao, mbunge kuleta hoja ili ijadiliwe kwa kina.