Benki ya Dunia wataka posho ipunguzwe

Luteni

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
2,274
301
(Kutoka Gazeti la Habari Leo 20/01/2010)
BENKI ya Dunia imeishauri Serikali ya Tanzania kupunguza matumizi ya ulipaji wa posho kwa maofisa wake kwani inatumia mabilioni ya fedha kulipana posho hali inayochangia baadhi ya miradi ya maendeleo utekelezaji wake kukwama.

Katika mada yake aliyoitoa kwenye kikao cha mapitio ya matumizi ya bajeti ya serikali kilichoitishwa jana na Benki ya Dunia, Mchumi wa benki hiyo Emmanuel Mungunasi alisema katika bajeti ya mwaka huu wa fedha Sh bilioni 325.9 zimetengwa kwa ajili ya maafisa kulipana posho katika wizara na idara za serikali na Sh bilioni 6.4 zimetengwa kama posho katika ngazi ya halmashauri za wilaya.

“Hizi ni fedha nyingi katika nchi maskini kama Tanzania, wasiwasi wangu ni kwamba kama hatutakuwa na utamaduni wa kupunguza posho hizi, fedha nyingi zitaenda mikononi mwa watu binafsi badala ya kwenda kwenye maendeleo,” alisema kwenye mkutano huo uliohudhuriwa na wawakilishi wa nchi wahisani.

Mchumi huyo alisema kinachoshangaza zaidi fedha hizo huwa zinanufaisha watu wachache tu katika wizara na idara za serikali, hivyo hata kama zitapunguzwa hakutakuwa na athari zozote kwa watumishi na kwa serikali yenyewe.

Alisema posho hizo sio zile ambazo ziko kwenye mikataba ya ajira ya watumishi ambayo kisheria inatambulika, bali hizi zinazopingwa na benki hiyo ni zile wanazolipwa kupitia vikao, kazi maalumu za miradi na posho nyinginezo ambazo alidai zinagharimu fedha nyingi kuliko uwezo wa nchi.

Alihoji kuwa kama utekelezaji wa miradi mingi ya serikali inatekelezwa katika ngazi ya halmashauri ya wilaya na manispaa iweje posho hizo nyingi zitumike katika mawizara na idara za Serikali Kuu ambazo ziko Dar es Salaam.

“Hapa ndipo kwenye tatizo, posho nyingi ziko Serikali Kuu wakati miradi iko wilayani, mbona hatuoni bajeti kubwa huko wilayani ya Kigoma au Moshi kwenye miradi husika? Alihoji Mungunasi.

Mchumi huyo pia alisema kuna haja ya Tanzania kuongeza kasi ya ujenzi wa miundombinu kama barabara na miundombinu ya maji ambayo alisema ni sekta mbili ambazo zinafanya vizuri.

Lakini pia alisema licha ya sekta ya elimu na afya na kilimo kutengewa fedha nyingi, lakini ujenzi wa miundombinu kwenye sekta hizo bado mdogo na akashauri kwamba kuna haja ya serikali kuwekeza zaidi katika ujenzi wa miundombuni ya sekta hizo tatu.

Eneo lingine alilozungumzia mchumi huyo ni utoaji wa fedha kwenye Bajeti ya Serikali na kusema kuwa kuna tatizo kwa baadhi ya wahisani kutotoa fedha hizo kwa wakati hivyo kukwamisha miradi ya maendeleo iliyokusudiwa.

Alitoa takwimu za utoaji wa fedha hizo na kuonyesha kuwa fedha za ndani zinatolewa kwa wakati mara nyingi kuliko fedha zinazotolewa na wahisani hasa kwenye sekta za kilimo, elimu, afya, nishati, barabara na maji.

Katika mada yake pia mchumi huyo alizungumzia ugawaji wa raslimali katika elimu ambako unaonesha kuwa baadhi ya maeneo yanapata fedha nyingi na akaeleza kuwa hiyo inatokana na tofauti za walimu walioko kwenye eneo hilo. Alitaja wilaya za Tabora, Mpanda, Urambo, Kibondo, Ngara kuwa zina walimu wachache na hivyo zimekuwa zinapokea kiasi kidogo cha fedha ukilinganisha na wilaya za Lindi, Kibaha na Iringa.

“Hapa kuna haja ya serikali kuweka vivutio katika maeneo ambayo yana watumishi wachache wa elimu na afya ili watumishi waweze kwenda maeneo hayo wanayokimbia,” alisema.

Naye Musa Bilfeya kutoka PINGO alihoji fedha ambazo hazitumiki kwenye miradi mbalimbali huko wilayani kama zinawekwa wazi. Alisema kiasi ch fedha zinazotolewa na serikali ni nyingi na zinazotumika huko wilayani kwenye miradi ni kidogo na haifanani na thamani ya fedha.

Naye Mchumi wa Benki ya Dunia tawi la Tanzania Paolo Zacchia alisema Tanzania itaendelea kupokea misaada mingi ndani ya miaka 15 hadi 20 ijayo hadi hapo itakapoweza kusimama imara kiuchumi.

Alisema nchi kama China ambayo imepiga hatua kubwa kimaendeleo hadi leo hii inaendelea kupokea mikopo na misaada kutoka nchi wahisani kama benki ya dunia. Alisema Tunisia taifa ambalo liko juu katika pato lake halisi la ndani nayo inaendelea kupata misaada.

“Hivyo Tanzania itaendelea kukopa na kupata misaada iimarishe sekta za elimu, afya na miundombinu. Bila hivyo haiwezi kupiga hatua,” alisema Zacchia.
 
Back
Top Bottom