Barrick yapewa maeneo 92 kufanya utafiti

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,011
Date::11/1/2008
Barrick yapewa maeneo 92 kufanya utafiti
Frederick Katulanda, Mwanza
Mwananchi

WAKATI sekta ya madini ikizidi kupigiwa kelele kwa kushindwa kunufaisha nchi hii, imebainika kuwa Kampuni ya Barrick ndiyo inayoongoza kwa kupewa maeneo mengi ya kuchimba na kufanya utafiti wa madini nchini.

Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi Jumapili umeonyesha kuwa orodha ya makampuni yaliyo na leseni za utafiti na uchimbaji kati ya leseni 535, zilizotolewa tangu mwaka 2000 hadi hivi karibuni, Kampuni ya Barrick ndiyo inayoongoza kwa kuwa na leseni za utafiti 92 kati ya hizo 40 zinamilikiwa na Kampuni ya Barrick Exploration na 52 zinamilikiwa na makampuni tanzu ya Kampuni Barrick Tanzania, kutafiti katika maeneo mbalimbali nchini.

Taarifa ya utafiti nchini iliyopatikana Wizara ya Nishati na Madini, inaonyesha kuwa leseni hizo za utafiti zilizotolewa kwa makampuni yake na idadi katika mabano ni Kampuni ya Afrika Mashariki Gold Mine (12), Kampuni ya Pangea Minerals Ltd (24),na Kampuni ya East Africa Mine Ltd (16).

Barrick ni moja kati ya makampuni makubwa ya kigeni katika sekta ya madini hapa nchini ambayo imekuwa ikimiliki migodi kadhaa mikubwa ya madini.

Kwa sasa kampuni hiyo inaendesha migodi mitatu mikubwa ya madini ambayo ni Bulyanhulu ulioko Kakola wilayani Kahama, Mgodi wa North Mara yenye leseni mbili za SML 18/96 kwa eneo la Nyabirama na SML 17/96 kwa eneo la Nyabigena wilayani Tarime mkoani Mara na ule wa Tulawaka SML 157/03 ulioko wilayani Bihalamuro mkoani Kagera.

Kampuni hiyo ya Barrick pia kwa sasa iko katika hatua za mwisho kuanza uchimbaji wa madini ya dhahabu katika migodi ya Buzwagi wilayani Kahama ule wa madini aina ya Nikeli Kabanga mkoani Kagera, hivyo kuifanya kuwa migodi mikubwa mitano nchini.

Baadhi ya maeneo ambayo kampuni hiyo infanya utafiti wa madini hivi sasa kupitia Kampuni ya Barrick Exploration Africa Ltd ni maeneo ya vijiji vya Buhungukira, Mhunze wilayani Kwimba, Imweru, Busolwa, Lunguya, Siga Hill, Kasubuya, Bupamwa na Mwamboku wilayani Geita, Kabale wilayani Sengerema, Munangu wilayani Magu yote yakiwa mkoani Mwanza.

Mengine ni Kakindu, Ushirombo wilayani Bukombe mkoani Shinyanga, Fort Ikoma wilayani Serengeti, Nyasirori Musoma vijijini, Kubaisa wilayani Tarime mkoani Mara. Leseni hizi zilitolewa kati ya kipindi cha mwaka 2000 na 2005 zikiruhusu utafiti wa madini ya dhahabu kwa kampuni hiyo na kutaja kiasi cha kilomita za mraba kwa kila eneo.

Pia kampuni hii ina leseni sita za utafiti wa madini aina ya Nikel kupitia kampuni ya Kabanga Nikel Co. Ltd.

Barrick ni kampuni mama ya Kampuni ya Pangea Minerals inayomiliki mgondiwa Tulawaka, mwaka 2001 ilianza uchimbaji wa madini katika mgodi wa Bulyanhulu Kahama , wakati mwaka 2006 ilichukua mgodi wa North Mara ulikuwa chini ya Kampuni ya Placer Dome Inc.

Kampuni ya Geita Gold Mining inayomiliki mgodi wa madini ya dhahabu Geita mkoni Mwanza nayo ni moja ya kampuni kubwa za kigeni inayomiliki mgodi wa madini ya dhahabu.

Afisa Uhusiano wa Kampuni ya Barrick, Teweli Teweli alipoulizwa kuhusiana na kampuni yake kumiliki keseni nyingi za uchimbaji na utafiti alisema hali hiyo haitokani na upendeleo bali uwezo wao.

Alisema Barrick ni kampuni inayoheshimika kwa uchimbaji wa dhahabu kutokana na kumiliki migodi 27 duniani.

"Hili sio suala la upendeleo ni suala la kibiashara, Barrick imeomba kwa serikali na kupatiwa. Yapo makampuni mengine, lakini Barrick ndiyo imeonyesha kuwa na uwezo mkubwa wa kuendesha migodikutokana na kuwa na migodi 27, hivyo jambo hilo haliwezi kuitwa upendeleo," alisema Tweli.

Tangu mwaka 1998 sheria ya madini ilipopitishwa, Tanzania imekuwa mzalishaji mkubwa katika soko la dunia la dhahabu, pia mzalishaji wa dhahabu wa tatu Afrika baada ya Afrika Kusini na Ghana lakini sekta hiyo imekuwa ikichangia asilimia 3.2 tu ya pato la taifa na asilimia 3.6 ya kodi zote za serikali.

Hivi karibuni Barrick Gold Tanzania ilisema kwamba inatarajia kuanza kupata faida katika mgodi wake wa Bulyanhulu mwaka 2014.

Meneja mkuu wa mgodi huo, Greg Walker, alikaririwa akisema kwamba hivi sasa bado hawajaanza kupata faida kutokana na kuendelea kurudisha gharama ya mtaji walizowekeza katika mgodi huo walipoanza mwaka 2001 ambazo ni Dola za Marekani 750 milioni.

Alisema hivi sasa wanalipa kodi isipokuwa kodi inayotokana na faida na kwamba mgodi huo unatumia fedha nyingi katika kufadhili wananchi wanaoishikatika sekta ya aelimu , maji na afya.

Hata hivyo, Peter Edson anaripoti kuwa Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja amesema uvumi uliopo kwamba Kampuni ya Barrick Internation ndiyo inayoongoza kuhodhi maeneo ya machimbo ya madini na ya utafiti, ni fikra hasi na kwamba Watanzania wanatakiwa kuziacha.

Waziri Ngeleja aliyasema hayo mwanzoni mwa wiki hii, alipokuwa akiongea na mwananchi jumapili wakati alipokuwa akikabidhi miradi ya Umeme, Maji, Barabara, na Simu katika eneo la Salasala jijini Da r es Salaam kwa taasisi husika.

“Siyo kweli kwamba Barrick ndiyo wanamiliki migodi mingi na kwamba wamepewa maeneo mengi ya kufanya utafiti wa madini, huu ni uvumi tu ambao unatakiwa kuachwa” alisema Ngeleja.

Alisema Leseni nyingi za uchunguzi wa madini zimetolewa kwa wawekezaji wa ndani ambao ni sekta binafsi kwa minajili ya kikundi, kamapuni ama tasisis yeyote iliyomo ndani ya nchi na ina nia ya kufanya tafiti za madini.

Alisema zaidi ya asilimia 80 za leseni zilizokwisha kutolewa zinamilikiwa na watanzania wenyewe, na kuongeza kuwa kila baada ya miezi mitatu wawekezaji wanaofanya tafiti wanalazimika kufikisha taarifa za maendeleo ya tafiti zao wizarani.

“Nia ya Serikali ni kutaka kuifanya sekta hii ya madini, iweze kuendeshwa na watanzania wenye, ili rasilimali hiyo iboreshe maisha yao na kukuza uchumi wa ndani katika Taifa hili,alisema waziri Ngeleja.

Hata hivyo, alitoa wito kwa wawekezaji wa ndani kuendelea kujitokeza kwa wingi ili waweze kupewa maeneo ya utafiti watakayoyaendeleza kwa manufaa ya nchi yao, watanzania na wao binafsi.

Alisema pamoja na matatizo mbalimbali yanayoikabili sekata hiyo, serikali inafanya juhudi katika kurekabisha sheria mbalimbali ili ziweze kuleta unafuu kwa wawekezaji wa ndani ikiwa ni pamoja na shughuli ya utafiti iweze kufanayika katika kipindi cha miaka saba.
 
God I wish we didn't have these minerals beneath our ground. Or is that I wish we didn't have incompetence at the high echelons of society and power?
 
Back
Top Bottom