KakaJambazi
JF-Expert Member
- Jun 5, 2009
- 18,711
- 12,067
Dawa ya vidonda vya tumbo utata
DAWA ya Fiterawa inayodaiwa kutibu vidonda vya tumbo, ubora wake umezua utata baada ya Taasisi ya Utafiti wa Dawa za Asili ya Chuo Kikuu cha Muhimbili na Mkemia Mkuu, kukana kuthibitisha matibabu yake.
Uchunguzi uliofanywa na HabariLeo Jumapili baada ya kupokea malalamiko ya baadhi ya watu kutosaidiwa na dawa hiyo na kuwa haijathibitishwa, umebaini kuwapo mawasiliano kati ya Muhimbili na mmiliki wa dawa hiyo, Rahabu Rubago, yakimtaka kuifanyia utafiti zaidi kwa sampuli zinazohusisha watu wengi zaidi.
Barua ya Muhimbili yenye kumbukumbu namba ITM/CB/III/12 ya Novemba 3, 2008 iliyosainiwa na mtaalamu wa tiba ambaye ni mtafiti Dk. C.S. Khadudu inataka ufanyike utafiti zaidi kwa tiba ya dawa hiyo.
Utafiti huu umezingatia utambuzi wa kemikali inayoingizwa katika utumbo kabla na baada ya matibabu. Pamoja na wagonjwa 10 kupona, imethibitisha umuhimu wa dawa hii.
Hata hivyo, kama inavyoonekana sampuli ni ndogo, hakuna takwimu zinazoonesha uthamani wake, hivyo kuna haja ya kufanyika utafiti wa mti unaotumika kwa kutumia sampuli kubwa zaidi, inasema sehemu ya barua hiyo. Barua hiyo iliyokuwa inajibu maombi ya Rubago ambaye anaitumia kama kielelezo cha uthibitisho wa tiba ya dawa hiyo, inaonesha kuwa utafiti wa Fiterawa umefanywa kwa watu 18, na watu 10 wamepona, watatu wakiendelea na matibabu na watano wakiachana na tiba hiyo.
Alipoulizwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Dawa za Asili, Dk Zakaria Mbwambo, alishangazwa na hatua ya Rubago kutumia jina la Muhimbili kutangaza tiba yake na kuwa suala hilo watalipeleka kwenye vyombo vya sheria. Kwa muda mrefu amekuwa akitangaza dawa yake kuthibitishwa na Muhimbili, lakini si kweli.
Inasikitisha, kwani anachotumia kujitangazia ni barua za mawasiliano baina yetu na yeye, kitendo anachokifanya ni kosa. Alileta hiyo dawa yake, tukiwa bado tunaendelea na uchunguzi, mwenzetu akaanza kujitangaza.
Ilikuwa ni lazima tujue ni kwa nini watu watano waliacha matibabu, kuna mambo mengi ya kupitia kabla ya kuthibitisha tiba ya dawa. Dawa hii ililenga kwenye dalili kama vile panadol na ndio mara nyingi zinatangazwa. Dk. Mbwambo alisema kwa muda mrefu sasa, wamekuwa wakitaka kukutana na Rubago, lakini wameshindwa kutokana na visingizio vingi.
Tumejaribu kumwita ili tuzungumze naye kwa muda mrefu kwa kupitia Chama cha Waganga wa Jadi, lakini imekuwa ngumu, mara anasema yuko Musoma, siku nyingine yuko Uingereza. Tumeamua kulipeleka suala hilo kwa Mwanasheria wa Chuo (Muhimbili) ili alichukulie hatua za kisheria. Rubago alipoulizwa kuhusu hali hiyo, alisema dawa yake imethibitishwa na Muhimbili, Mkemia Mkuu, Wizara ya Afya na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA).
Hao wanaosema kuwa dawa yangu haijathibitishwa ni maadui zangu, kama unataka uthibitisho nenda Muhimbili, Mkemia Mkuu, TFDA na hata wabunge wanaothibitisha kutibiwa na dawa yangu. Nina ruhusa za mpaka Waziri wa Afya kuanzia ujumbe na hata barua, alisisitiza.
Mwandishi wa habari hizi alikwenda katika ofisi za Buguruni kujua ukweli wa suala hili, hata hivyo Rubago alitoa maelekezo kwa msaidizi wake ili aoneshe nyaraka za uthibitisho wa Muhimbili, Mkemia Mkuu na kibali cha biashara kutoka kwa Mganga Mkuu wa Wilaya.
Alipoulizwa kwa njia ya simu ni kwa nini anatumia jina la Muhimbili kuthibitisha dawa yake na kutoitika mwito wa taasisi hiyo, alisema:
Sikuwahi kupokea barua ya Muhimbili zaidi ya kupigiwa simu, siwezi kuitwa kwa simu na kuamini, maana kuna wakati niliwahi kutekwa.
Muhimbili hawawezi kunizuia kutoa tiba, wao wanatakiwa kuithibitisha tu. Mbona metakelfin inaweza kumponesha mmoja na mwingine ikambabua? Unajua maadui zangu wako Muhimbili, na kama wanataka kunichukulia hatua za kisheria niko tayari kukabiliana na hilo, alisema.
HabariLeo Jumapili ilipozungumza na Kaimu Mkemia Mkuu wa Serikali, Daniel Matata, alisema ofisi yake haijathibitisha ubora na uwezo wa dawa hiyo kutibu vidonda vya tumbo bali wanachoangalia ni usalama wa matumizi yake kwa mwanadamu.
Mtu akileta sampuli yake hapa, tunaangalia kama ni salama kwa matumizi na hapo tunaangalia kama haina madhara kwa mtumiaji, tunaangalia kusiwe na madini tembo, sumu za asili kwenye mmea, sumu za asili za mazingira na kemikali zingine.
Imekuwapo tabia ya wanaotoa tiba mbadala, kudai kuwa dawa zimethibitishwa na Mkemia Mkuu, kwa kufanya hivyo ni kosa. Hii ni ofisi kubwa na kutumia jina letu inajenga imani kwa wananchi. Wanachotakiwa kutangaza ni uthibitisho kuwa iko salama. Tunavyochunguza sampuli za dawa ni kama tunavyofanya kwenye maji au juisi, alisema.
Barua ya Mkemia Mkuu yenye namba 341/VOL/XII ya Novemba 13, 2008 iliyosainiwa na Fundi Msanifu Mkuu Daraja la I, J. Ngahyoma na kuthibitishwa na Mkemia Mkuu wa Serikali (wakati huo), Ernest Mashimba, ilibainisha kuwa dawa hiyo ina Alkaloids isiyotambulikana, inayotumika kutibu magonjwa mbalimbali ya binadamu kutegemeana na ushauri wa mtoaji.
Hata hivyo, barua hiyo ilimtaka Rubago kuwasiliana na kitengo cha dawa za asili cha Chuo Kikuu cha Muhimbili kwa ushauri zaidi. Kwa upande wa TFDA, bado haijaanza kusajili dawa za tiba asili na kuwa kazi hiyo itafanyika Desemba.
Hawezi kuitaja TFDA, kwa sababu ndio kwanza tumeanza utaratibu wa kusajili dawa za asili mwaka huu na kwa wakati huu tunapokea maombi na Desemba ndipo tutakapoanza kuzipitisha zinazofaa. Baada ya hapo dawa ambazo hazitasajiliwa hazitauzwa, alisema Kaimu Mkurugenzi wa TFDA, Mitangu Fimbo, ambaye alisema ni watu tisa tu waliopeleka maombi.
HabariLeo ilikutana na mgonjwa wa vidonda vya tumbo ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini na kudai kutibiwa na Rubago mwaka 2009, lakini mpaka sasa hajapona.
Mwaka 2009 ndipo nilipojua dawa ya Fiterawa, baada ya kwenda kwenye maonesho ya Sabasaba, nilipewa dozi ya kwanza ambayo ilikuwa ni madumu sita kila moja likiwa na lita tano iliyonigharimu Sh 450,000, pamoja na kufuata masharti yote hali ilizidi kuwa mbaya.
Nilikwenda tena nikapewa dozi ya pili ambayo niliimaliza Septemba mwaka huo huo na hakukuwa na mabadiliko, ingawa kwa kiasi ilipunguza gesi. Nilivyoona sijapona nilikwenda kuzungumza naye (Rubago) na alinishauri nikapime virusi vya Ukimwi akidai kuwa hiyo inachangia vidonda kutopona.
Nilipima na kukuta sina na hapo akanieleza kuwa huenda vidonda vyangu ni sugu au nimekosea masharti, baada ya kuona hivyo, niliamua kuachana naye, alisema.
Sosi: Habarileo.
DAWA ya Fiterawa inayodaiwa kutibu vidonda vya tumbo, ubora wake umezua utata baada ya Taasisi ya Utafiti wa Dawa za Asili ya Chuo Kikuu cha Muhimbili na Mkemia Mkuu, kukana kuthibitisha matibabu yake.
Uchunguzi uliofanywa na HabariLeo Jumapili baada ya kupokea malalamiko ya baadhi ya watu kutosaidiwa na dawa hiyo na kuwa haijathibitishwa, umebaini kuwapo mawasiliano kati ya Muhimbili na mmiliki wa dawa hiyo, Rahabu Rubago, yakimtaka kuifanyia utafiti zaidi kwa sampuli zinazohusisha watu wengi zaidi.
Barua ya Muhimbili yenye kumbukumbu namba ITM/CB/III/12 ya Novemba 3, 2008 iliyosainiwa na mtaalamu wa tiba ambaye ni mtafiti Dk. C.S. Khadudu inataka ufanyike utafiti zaidi kwa tiba ya dawa hiyo.
Utafiti huu umezingatia utambuzi wa kemikali inayoingizwa katika utumbo kabla na baada ya matibabu. Pamoja na wagonjwa 10 kupona, imethibitisha umuhimu wa dawa hii.
Hata hivyo, kama inavyoonekana sampuli ni ndogo, hakuna takwimu zinazoonesha uthamani wake, hivyo kuna haja ya kufanyika utafiti wa mti unaotumika kwa kutumia sampuli kubwa zaidi, inasema sehemu ya barua hiyo. Barua hiyo iliyokuwa inajibu maombi ya Rubago ambaye anaitumia kama kielelezo cha uthibitisho wa tiba ya dawa hiyo, inaonesha kuwa utafiti wa Fiterawa umefanywa kwa watu 18, na watu 10 wamepona, watatu wakiendelea na matibabu na watano wakiachana na tiba hiyo.
Alipoulizwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti wa Dawa za Asili, Dk Zakaria Mbwambo, alishangazwa na hatua ya Rubago kutumia jina la Muhimbili kutangaza tiba yake na kuwa suala hilo watalipeleka kwenye vyombo vya sheria. Kwa muda mrefu amekuwa akitangaza dawa yake kuthibitishwa na Muhimbili, lakini si kweli.
Inasikitisha, kwani anachotumia kujitangazia ni barua za mawasiliano baina yetu na yeye, kitendo anachokifanya ni kosa. Alileta hiyo dawa yake, tukiwa bado tunaendelea na uchunguzi, mwenzetu akaanza kujitangaza.
Ilikuwa ni lazima tujue ni kwa nini watu watano waliacha matibabu, kuna mambo mengi ya kupitia kabla ya kuthibitisha tiba ya dawa. Dawa hii ililenga kwenye dalili kama vile panadol na ndio mara nyingi zinatangazwa. Dk. Mbwambo alisema kwa muda mrefu sasa, wamekuwa wakitaka kukutana na Rubago, lakini wameshindwa kutokana na visingizio vingi.
Tumejaribu kumwita ili tuzungumze naye kwa muda mrefu kwa kupitia Chama cha Waganga wa Jadi, lakini imekuwa ngumu, mara anasema yuko Musoma, siku nyingine yuko Uingereza. Tumeamua kulipeleka suala hilo kwa Mwanasheria wa Chuo (Muhimbili) ili alichukulie hatua za kisheria. Rubago alipoulizwa kuhusu hali hiyo, alisema dawa yake imethibitishwa na Muhimbili, Mkemia Mkuu, Wizara ya Afya na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA).
Hao wanaosema kuwa dawa yangu haijathibitishwa ni maadui zangu, kama unataka uthibitisho nenda Muhimbili, Mkemia Mkuu, TFDA na hata wabunge wanaothibitisha kutibiwa na dawa yangu. Nina ruhusa za mpaka Waziri wa Afya kuanzia ujumbe na hata barua, alisisitiza.
Mwandishi wa habari hizi alikwenda katika ofisi za Buguruni kujua ukweli wa suala hili, hata hivyo Rubago alitoa maelekezo kwa msaidizi wake ili aoneshe nyaraka za uthibitisho wa Muhimbili, Mkemia Mkuu na kibali cha biashara kutoka kwa Mganga Mkuu wa Wilaya.
Alipoulizwa kwa njia ya simu ni kwa nini anatumia jina la Muhimbili kuthibitisha dawa yake na kutoitika mwito wa taasisi hiyo, alisema:
Sikuwahi kupokea barua ya Muhimbili zaidi ya kupigiwa simu, siwezi kuitwa kwa simu na kuamini, maana kuna wakati niliwahi kutekwa.
Muhimbili hawawezi kunizuia kutoa tiba, wao wanatakiwa kuithibitisha tu. Mbona metakelfin inaweza kumponesha mmoja na mwingine ikambabua? Unajua maadui zangu wako Muhimbili, na kama wanataka kunichukulia hatua za kisheria niko tayari kukabiliana na hilo, alisema.
HabariLeo Jumapili ilipozungumza na Kaimu Mkemia Mkuu wa Serikali, Daniel Matata, alisema ofisi yake haijathibitisha ubora na uwezo wa dawa hiyo kutibu vidonda vya tumbo bali wanachoangalia ni usalama wa matumizi yake kwa mwanadamu.
Mtu akileta sampuli yake hapa, tunaangalia kama ni salama kwa matumizi na hapo tunaangalia kama haina madhara kwa mtumiaji, tunaangalia kusiwe na madini tembo, sumu za asili kwenye mmea, sumu za asili za mazingira na kemikali zingine.
Imekuwapo tabia ya wanaotoa tiba mbadala, kudai kuwa dawa zimethibitishwa na Mkemia Mkuu, kwa kufanya hivyo ni kosa. Hii ni ofisi kubwa na kutumia jina letu inajenga imani kwa wananchi. Wanachotakiwa kutangaza ni uthibitisho kuwa iko salama. Tunavyochunguza sampuli za dawa ni kama tunavyofanya kwenye maji au juisi, alisema.
Barua ya Mkemia Mkuu yenye namba 341/VOL/XII ya Novemba 13, 2008 iliyosainiwa na Fundi Msanifu Mkuu Daraja la I, J. Ngahyoma na kuthibitishwa na Mkemia Mkuu wa Serikali (wakati huo), Ernest Mashimba, ilibainisha kuwa dawa hiyo ina Alkaloids isiyotambulikana, inayotumika kutibu magonjwa mbalimbali ya binadamu kutegemeana na ushauri wa mtoaji.
Hata hivyo, barua hiyo ilimtaka Rubago kuwasiliana na kitengo cha dawa za asili cha Chuo Kikuu cha Muhimbili kwa ushauri zaidi. Kwa upande wa TFDA, bado haijaanza kusajili dawa za tiba asili na kuwa kazi hiyo itafanyika Desemba.
Hawezi kuitaja TFDA, kwa sababu ndio kwanza tumeanza utaratibu wa kusajili dawa za asili mwaka huu na kwa wakati huu tunapokea maombi na Desemba ndipo tutakapoanza kuzipitisha zinazofaa. Baada ya hapo dawa ambazo hazitasajiliwa hazitauzwa, alisema Kaimu Mkurugenzi wa TFDA, Mitangu Fimbo, ambaye alisema ni watu tisa tu waliopeleka maombi.
HabariLeo ilikutana na mgonjwa wa vidonda vya tumbo ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini na kudai kutibiwa na Rubago mwaka 2009, lakini mpaka sasa hajapona.
Mwaka 2009 ndipo nilipojua dawa ya Fiterawa, baada ya kwenda kwenye maonesho ya Sabasaba, nilipewa dozi ya kwanza ambayo ilikuwa ni madumu sita kila moja likiwa na lita tano iliyonigharimu Sh 450,000, pamoja na kufuata masharti yote hali ilizidi kuwa mbaya.
Nilikwenda tena nikapewa dozi ya pili ambayo niliimaliza Septemba mwaka huo huo na hakukuwa na mabadiliko, ingawa kwa kiasi ilipunguza gesi. Nilivyoona sijapona nilikwenda kuzungumza naye (Rubago) na alinishauri nikapime virusi vya Ukimwi akidai kuwa hiyo inachangia vidonda kutopona.
Nilipima na kukuta sina na hapo akanieleza kuwa huenda vidonda vyangu ni sugu au nimekosea masharti, baada ya kuona hivyo, niliamua kuachana naye, alisema.
Sosi: Habarileo.