Ansbert Ngurumo: Wither JK's CCM Chairmanship?

M-mbabe

JF-Expert Member
Oct 29, 2009
13,203
23,020
Ansbert Ngurumo ameandika kwenye column yake ya 'maswali magumu" gazeti la tz daima.......READ ON

================================================================================

SIKUSHTUSHWA na kauli ya ukali ya Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, kwamba kuna watu ndani ya chama chao wanataka kumwondoa mwenyekiti wao, Rais Jakaya Kikwete, na kuweka mwenyekiti mwingine kabla ya 2015.

Katika kujibu mapigo ya vijana wenzake waliomkosoa yeye na wenzake wanaodai kwamba nchi hii ni ya CCM; na katika kuwatunishia misuli vijana hao na wote anaodai wako nyuma yao, Nape alisema wote wanaofikiria kumwondoa Rais Kikwete kwenye uenyekiti ni wasaliti na wahaini.

Kauli ya Nape inazusha maswali mengi. Kwanza, wapo wanaojiuliza kama alichosema ni chake au alitumwa na Rais Kikwete. Wanaojua hali ya mambo ndani ya CCM, wanajua fika kuwa alichokisema Nape si kipya ndani ya CCM.

Kumekuwa na fukuto ndani ya CCM, linalotokana na hisia kwamba chama kimedorora, kimekuwa legelege. Matokeo yake na serikali imekuwa legelege. Maana yake ni kwamba iwapo wataendelea na uongozi wa aina hii hadi 2015, ni vigumu CCM kushinda uchaguzi.

Kwa hiyo, makundi kadhaa ya wanaokitakia mema chama chao wanadhani wakati wa kufanya mageuzi ndani ya CCM ni sasa. Na wanataka kuanza na uongozi wa juu, ili kukisuka vema chama na kukipa mwelekeo.

Wanakiri kwamba uongozi wa sasa umepwaya. Ambacho hawajakubaliana ni nani azibe nafasi ya Rais Kikwete. Baadhi ya mapendekezo yanayotolewa yanawalenga wastahafu kadhaa wanaosikilizwa, ambao huko nyuma wameonyesha uwezo wa kuongoza.

Hata hivyo, kundi hili linakosa jambo moja – ujasiri wa kusema hayo kwenye vikao rasmi vya chama. Wanaogopa kusema kwa sababu wanajua mwenyekiti wao haoni kile wanachoona wao.

Hajakubali kwamba ameshindwa kuongoza chama. Hakubaliani nao kwamba CCM imekuwa legelege mikononi mwake. Hivyo, hayupo tayari kumpisha yeyote achukue nafasi yake kabla ya muda aliofikiria yeye kung’atuka.

Na kwa kuwa mwenyekiti wao ni rais, wanaogopa pia nguvu ya dola ambayo anaweza kuitumia kuwashughulikia wale wanaotamani aachie uenyekiti kabla ya 2015.

Nadhani mamlaka haya ya dola aliyonayo Rais Kikwete ndiyo yanampatia Nape jeuri ya kuwasema wanaotaka mabadiliko hayo, kwani anajua analindwa na yule anayemtetea. Na kwa hakika, wengi wanasema kwamba Nape ametumwa kuwatisha wanaotamani mageuzi hayo. Kauli ya Nape si yake hasa, ni ya Rais Kikwete.

Pili, wote wenye akili timamu hawakubaliani na Nape kwamba kutamani kubadilisha uongozi unaoonekana dhahiri kwamba umeshindwa ni uhaini. Si mapinduzi ya serikali; bali ni mwamko wa kutaka kufanya mabadiliko ya uongozi wa chama ili kukiimarisha kwa ajili ya ushindani makini siku za usoni.

Hawa wanatambua kwamba jamii pana ya Watanzania sasa inaliona hilo, na ndiyo maana, miongoni mwa sababu nyingi zilizopo, wananchi wanakiunga mkono Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Wanajua kuwa CCM hii ya Rais Kikwete, kama itaendelea kufa kila siku namna hii, haitaweza kufua dafu mbele ya nguvu ya umma. Kwa maneno mengine, wanataka kumsaidia Rais Kikwete kukivusha chama katika uchaguzi ujao.

Wengine wanadiriki kusema kwamba kukijenga upya chama hicho ndiyo maana halisi ya dhana ya kujivua gamba. Na ndiyo jinsi ya kukiondolea ombwe la uongozi linalokikabili. Maana niliwahi kuandika kwamba dhana ya kuvuana magamba ilichochewa na harakati za baadhi ya wanachama kupendekeza kwamba Rais Kikwete na Yusuph Makamba wapumzishwe majukumu ya uongozi waliyonayo.

Mwenyekiti akajiwahi, akayateka mapinduzi kwa kumpumzisha katibu mkuu ili kupoza hasira; na akaanzisha vuguvugu la kujivua gamba kwa kuwanyoshea vidole wengine.

Tatu, Nape amefanya lile alilopaswa kuzuia. Amewasaidia Watanzania wote kutambua kwamba ndani ya CCM mambo yameharibika kiasi hicho, kwamba hata wanawaza kumwondoa mwenyekiti wao.

Ingawa hali hii ilijulikana kwa baadhi yao ndani ya chama, kauli ya Nape imetangazia taifa zima kile ambacho yeye alitaka kiwe siri, na kiwe mwiko. Kwa maana nyingine, amewahamasisha hata wana CCM wengine kuanza kutafakari mustakabali wa chama chao.

Amewasaidia kuanza kufikiria udhaifu wa mwenyekiti wao, na kuwaza nani anaweza kuziba nafasi hiyo.

Ingawa si lazima mabadiliko hayo yatokee sasa, kwa sababu Rais Kikwete naye anajaribu kwa nguvu zake zote kuyazuia, kauli ya Nape imeacha kovu. Hata kama kidonda kitapona, alama inabaki; kovu linaonekana.

Nape angeweza kumfichia Rais Kikwete udhaifu wake huu kwa njia mbili – ama kwa kutolizungumza kabisa hadharani, au kwa kuwasaidia wanaotaka kumwondoa mwenyekiti wafanye hivyo kistaarabu ili kuhakikisha chama hakimeguki, na anayeondoka hajihisi kudhalilika.

Nne, kauli ya Nape imezusha swali la msingi. Kumetokea kitu gani ndani ya CCM hadi baadhi ya wanachama na viongozi wawaze kumwondoa Rais Kikwete kwenye uenyekiti wake?

Katika mazingira yasiyo na dosari kubwa, kwa chama kinachoongozwa na mwenyekiti ambaye pia ni rais wa nchi, si rahisi kwa viongozi kuanzisha mchakato wa kumwondoa kiongozi mkuu katika nafasi yake.

Swali hili, pamoja na kwamba linawagusa wana CCM na wananchi wengine wanaofuatilia siasa za CCM, linamgusa mwenyekiti mwenyewe.

Angepaswa kujiuliza kwa nini kwa mara ya kwanza katika histosia ya CCM viongozi na wanachama wao wanaona mwenyekiti amevaa viatu vinavyompwaya!

Kuwapuuza na kuwatisha wanaowaza hivyo hakusaidii kukijenga chama chao. Wanaweza kunyamaza kwa vitisho hivyo, lakini hakuna atakayeweza kuzuia kile wanachokipanga kimya kimya.

Na hata kama watasitisha mpango wa kumwondoa mwenyekiti sasa, atabaki kuwa mwenyekiti asiye na nguvu, asiye na mvuto na asiye na kauli.

Atakuwa ni mwenyekiti aliyetikisika, ambaye anadhani njia pekee ya kujiimarisha kwenye kiti ni kuwatikisha wanaomtikisa, au kuwasaliti wale anaodhani ndio wanamsaliti.

Na mwenyekiti akishatikisika, chama chake kitakuwa legelege tu. Na kwa kuwa ndicho kilicho madarakani, itatoka wapi serikali imara?

Kwa hiyo, ingawa kwa macho ya kipropaganda wanaweza kuonekana wasaliti na wahaini kwa kufikiria kubadilisha uongozi wa chama chao, yawezekana wanafanya uhaini wa kukijenga na kukiimarisha ili kukipa mustakabali chama chao.

Wakati mwingine nadhani wasaliti na wahaini hawa wa CCM ni watu muhimu sana. Hebu kwanza tuwasikilize!
 
Haya yanayotokea sasa hivi ndani ya CCM ni njia ya mteremko kuelekea kwenye anguko kuu, CCM haitainuka tena milele. CCM itapoteza dola 2015 au hata kabla ya mwaka huo, na hapo amini msiamini uvundo uliojificha ndani ya viongozi waliopo na waliopita wa CCM ndo utakapotanda angani na kuchafua kabisa hali ya hewa ya Tanzania. Hili halina ubishi, kwa sasa hivi viongozi wa CCM ni wachafu wasio na mfano. Na uchafu wao huo ndo unaowafanya watumie nguvu iliyopitiliza kugombania madaraka na mfano ni chaguzi ndogo za Busanda na Igunga.

Dalili ninayoiona huko mbele ni UMWAGAJI MKUBWA WA DAMU ambao utasababishwa kwa 100% na CCM kung'ang'ania madaraka pindi wananchi watakaposema basi. Na dalili zenyewe zinaonekana wazi kabisa kwa wao kushindwa kusimamia madai ya msingi ya mabadiliko ya katiba. Bado wanataka kutupeleka kwenye uchaguzi wa 2015 tukiwa na Tume ya Uchaguzi ya CCM, yaani kama mechi ya mpira basi refarii ni wenyewe, washika vibendela wenyewe, kamisaa wenyewe, wachezaji wenyewe na walinzi wa usalama uwanjani ni wenyewe harafu wanaita timu ya upinzani ije kucheza nao. Safari sidhani kama mashabiki watawakubalia, na hapo ndipo watakapolazimisha ushindi na kusababisha UMWAGAJI MKUBWA WA DAMU. Mungu ibariki Tanganyika.
 
Back
Top Bottom