Bujibuji Simba Nyamaume
JF-Expert Member
- Feb 4, 2009
- 74,834
- 155,782
YADHIHIRIKA MURO ANATEMBEA NA KIFO MKONONI, ALAZIMIKA KUISHI MAFICHONI
Yule Daktari aliyepigwa risasi iliyomkosa mtangazaji wa habari za uchunguzi wa Shirika la Utangazaji la Tanzania (TBC1) Jerry Muro, Dk. Paul Andrew ametoboa siri kwa kusema kuwa kitendo chake cha kujeruhiwa mguuni kwa risasi ni njama za wazi zilizofanywa na wabaya wao.
Akizungumza na gazeti hili mwishoni mwa wiki iliyopita, Dk. Andrew alitoboa siri kuwa ana undugu na Jerry, na kuongeza kwamba amekuwa akijijengea maadui na wafanyakazi wa taasisi moja (jina tunalihifadhi) ambao wamekuwa wakikiuka maadili ya kazi ya udaktari na kila anapowaonya, anageuka kuwa adui kwao.
Naweza kusema wazi kwamba wafanyakazi hao ambao wana kawaida ya kufanya kazi kinyume cha maadili, huniona adui yao kila ninapokwenda kuwaonya, naweza kusema wanahusika na njama za kutaka kuniua na kunizushia mambo ya hatari katika jamii, japokuwa pia inawezekana nia ya wadunguaji ilikuwa kumpata Jerry, alisema Dk. Andrew.
Akifafanua zaidi Daktari huyo ambaye ni mtaalamu wa magonjwa ya binadamu alisema siku ya tukio Machi 12, mwaka huu akiwa na Jerry, alishangazwa kuona gari moja dogo lenye rangi ya fedha (Silver) likiwapita kwa kasi wakiwa nje ya Mahakama ya Hakimu Mkazi, Kisutu alikokwenda kwenye kesi ya ndugu yake huyo (Jerry Muro).
Alisema walikuwa nje ya mahakama na wakati huo walikuwa wakipanga kwenda kumuona mwanasheria, lakini ghafla gari lilipita na tukio hilo likatokea.
Lile gari tuliligutukia baada ya mimi kupigwa risasi mguuni na kuanguka, tukaliona linakwenda kwa kasi huku nikiachwa nikivuja damu nyingi sana na wakati huo huo risasi ikiwa imetoboa kiatu na kuingia mwilini mwangu, mguu wa kushoto, alisema Dk. Andrew.
Alisema mara baada ya kitendo kile na kujikuta akiwa chini, watu walikusanyika lakini ndugu zake wakamkimbiza Hospitali ya Marie Stopes anakofanyia kazi kwa gari alilokuwa akiendesha Jerry na baada ya kufika na kufanyiwa uchunguzi, madaktari walisema mshipa wa damu ulikatika ndiyo maana alikuwa akivuja damu nyingi.
Alifafanua kwamba madaktari hao walimshona jeraha na akalazwa hapo, hivyo huwa analitafakari tukio hilo ambalo hadi sasa linamtia hofu na woga mkubwa.
Hata hivyo, baadhi ya ndugu wa Andrew na Jerry Muro waliozungumza na gazeti hili kwa masharti ya kuhifadhi majina yao walisema kuna kila dalili kwamba aliyekuwa akiwindwa siku hiyo kumalizwa ni Jerry na sasa anatembea na kifo mkononi.
Tuna wasi wasi mkubwa na ndugu yetu kwa sababu waandishi wengi duniani wanaofanya kazi za uchunguzi huishia pabaya, hapa nchini tulikuwa na Bw. Stan Katabalo ambaye alifichua kashfa ya Loliondo, kifo chake kilikuwa ni cha kutatanisha, tuna mashaka Jerry wanaweza kumfanya hivyo hivyo, alisema mmoja wa ndugu hao.
Aidha, ndugu huyo alionesha wasiwasi wake kwa jeshi la polisi kuwa hata kesi ambazo Jerry aliwahi kuziripoti polisi kwa kufungua majalada, hakuna kilichofanyika hadi sasa, hali wanayoitafsiri kuwa wanasusa masuala ya ndugu yao kwa kuwa tu alianika uozo wa polisi wa usalama barabarani.
Jerry aliwahi kufungua kesi tatu tofauti katika Kituo cha Oysterbay na Kituo Kikuu cha Polisi kutokana na kushambuliwa na kuibiwa laptop iliyokuwa na kumbukumbu muhimu lakini kesi zote zimeganda katika vituo hivyo vya usalama wa raia.
Gazeti hili liliwahi kuzungumza na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ilala, Faustine Shilogile kuhusiana na kesi hizo lakini akasema RB namba OB/RB/1855/2009 (Wizi wa Laptop) ipo Kituo cha Oysterbay hivyo hawezi kujua kinachoendelea huko wakati shauri namba CD/ IR/148171 (shambulio) na CD /RB/ 15133/2009 zipo Kituo Kikuu cha Polisi, akaahidi kufuatilia.
SOURCE:- SHIGONGO'S WEBSITE