Akaunti ya kigogo TANESCO yazuiwa;Yakutwa na zaidi ya Sh. bilioni moja, uchunguzi waendelea

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797

Waandishi Wetu

Toleo la 250
18 Jul 2012



  • Yakutwa na zaidi ya Sh. bilioni moja, uchunguzi waendelea
  • Mpango wa kupandikiza mgawo ‘feki' wa umeme wafichuliwa

SIKU chache baada ya kusimamishwa kazi kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme (TANESCO), William Mhando na wenzake: Robert Shemhilu, Lusekelo Kassanga na Haruna Mattambo, akaunti ya mmoja wa vigogo wa shirika hilo ngazi ya menejimenti iliyoko katika moja ya benki nchini imezuiwa na vyombo vya dola nchini, Raia Mwema, limeelezwa.

Akaunti ya kigogo huyo (jina la benki na la mwenye akaunti yanahifadhiwa ili kutoharibu uchunguzi unaoendelea) imekutwa na fedha zaidi ya shilingi bilioni moja na sasa inadaiwa kuzuiwa kwa baraka za mamlaka za juu.

Vyanzo kadhaa vya habari vimeeleza ya kuwa kigogo huyo amekutwa na mabilioni hayo ya fedha huku chanzo cha mapato hayo yasiyolingana na kipato chake kama mtumishi wa umma kikiwa ni utata.

Hata hivyo, wakati uchunguzi huo wa awali unaofanywa na vyombo vya dola nchini ukiwa unaendelea, kwa upande mwingine kumebainika kuwapo na kampeni kali za kuuokoa uongozi wa TANESCO unaochunguzwa kwa sasa, juhudi ambazo zimekuwa zikihusisha hata Kamati za Bunge.

Kamati za Bunge ambazo baadhi ya wajumbe wake wanahusishwa katika ‘kuokoa' jahazi la uongozi wa TANESCO uliosimamishwa ni pamoja na Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma.

Baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo sasa wanatajwa kuanza kumwandama Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi pamoja na Waziri Profesa Sospeter Muhongo na Naibu wake, George Simbachawene, wanaotajwa kuwa na msimamo mkali dhidi ya kile kinachodaiwa kuwa ni uzembe na ubadhirifu ndani ya TANESCO.

Mgawo feki wa umeme

Kwa mujibu wa taarifa zilizopo, kwa muda mrefu sasa kumekuwa na njama za kuandaa na kufanikisha mgawo ‘feki' wa umeme nchini kwa njia mbalimbali. Lengo la mgawo huo ni kuwanufaisha baadhi ya vigogo TANESCO kwa njia ya ununuzi wa mafuta ya kuendeshea mitambo.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili na kuthibitishwa na vyanzo mbalimbali vya habari ndani ya Wizara ya Nishati na Madini pamoja na TANESCO, umebaini kuwa baadhi ya mitambo ya kuzalisha umeme jijini Dar es Salaam, na hasa baadhi ya mitambo iliyopo eneo la Ubungo na Tegeta imekuwa ikizimwa ili kuhalalisha migao na mpango wa ununuzi mafuta unaowaingizia fedha vigogo. Orodha ya mitambo inayozalisha umeme kwa mafuta jijini Dar es Salaam ni pamoja na IPTL, Symbion na Aggreko.

Taarifa zilizopo zinazidi kubainisha kuwa, baada ya kuzima mitambo hiyo na kusababisha mgawo wa umeme (usio wa lazima-feki), wito wa kuzalisha umeme wa mafuta hujitokeza.

Ni katika wito huo ambao msingi wake ni kupandikiza mgawo feki wa umeme, wakati mwingine Serikali hutoa fedha za ununuzi wa mafuta lakini wakati mwingine fedha hizo huchotwa kutoka TANESCO, shirika ambalo kila mwezi hukusanya shilingi karibu ya bilioni 100 kutoka kwa wateja wake.

Katika ununuzi huo wa mafuta kwa ajili ya kuendesha mitambo ili kuongeza uzalishaji wa umeme, mambo kadhaa huzingatiwa ili kunufaisha wahusika.

Jambo la kwanza ni kupatikana kwa kile kinachoitwa "ten percent" kinachogawanywa kwa waliofanikisha mpango huo. Pili, ni kuendelea kufanya wizi katika kiwango cha mafuta kilichokwishakununuliwa kwa ajili ya kuwasha mitambo husika.

Mchezo huo mchafu unadaiwa kuripotiwa kwa baadhi ya viongozi wa TANESCO lakini hapakuwa na hatua zilizopata kuchukuliwa hadi pale suala hilo lilipofika katika uongozi wa Wizara ya Nishati na Madini.

"Suala hili limekuwa likifanyika kwa muda mrefu sasa, umeme unakatwa na kuzalishwa kwa kiwango cha chini ili kuibua mahitaji ya kuzalisha umeme kwa njia ya mafuta ili TANESCO wanunue. Katika ununuzi huo kuna suala la 10% na wizi wa hayo hayo mafuta yanayonunuliwa lakini pia ni manufaa kwa kampuni za uzalishaji umeme huo kwa kuwa zinakuwa zikifanya biashara kwa kuuza umeme huo TANESCO.

"Ni suala lililowahi kuripotiwa lakini likapuuzwa na menejimenti, ila miezi takriban mitatu kupita baada ya kuripotiwa kuliwahi kufanyika kikao cha wafanyakazi wote kupitia TUICO, baada ya wafanyakazi kutia shinikizo kuhusu hujuma hizi Mkurugenzi wa TANESCO, Mhando naye ndipo akadai kupata taarifa hizo hapo kwa mara ya kwanza na aliahidi kuchukua hatua," kilieleza chanzo kimoja cha habari.

Hujuma kwa mtambo wa Kinyerezi

Hujuma nyingine inayotajwa kufanyika ndani ya TANESCO ni kuahirishwa mara kwa mara kwa mchakato wa kuanzisha mtambo wa kuzalisha umeme eneo la Kinyerezi, jijini Dar es Salaam.

Mtambo huo ambao utazalisha umeme kwa kutumia gesi, unatajwa kuwa tishio dhidi ya mtandao wa wauzaji mafuta kwa TANESCO kwa ajili ya uzalishaji umeme kwa kutumia mafuta.

"Kutokana na tishio la mradi huu utakapokamilika kuwanyima ulaji, walikuwa wakiukwamisha. Ni mradi wa megawati 240. Huu (mradi wa Kinyerezi) utaua kabisa mpango wao wa ulaji kwa kuandaa mgawo feki na kuzalisha umeme kwa mafuta. Waziri Muhongo alipoingia alihakikisha mradi unasainiwa ili kuanza....lazima wampige vita na aliwaeleza katika moja ya vikao (waziri) kuchukizwa na tabia hiyo,"

Wabunge nao watajwa

Mbunge mmoja wa Viti Maalumu kutoka mikoani (kwa sasa hatutamtaja kwa kuwa hatukufanikiwa kumpata) anadaiwa kunufaika na uongozi wa TANESCO uliosimamishwa.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotufikia,mbunge huyo anadaiwa kupewa zabuni ya kusambaza matairi kwa ajili ya magari ya TANESCO kupitia kampuni yake. Madai yanayoelekezwa kwa mbunge huyo ni kwamba, kampuni yake ilipewa zabuni baada ya zabuni hiyo ‘kuporwa' kutoka kwa kampuni nyingine.

Lakini wakati mbunge huyo wa Viti Maalumu akihusishwa na madai hayo, mbunge mwingine na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, Freeman Mbowe, naye anadaiwa kuwa na maslahi na uongozi uliosimamishwa wa TANESCO.

Kwa mujibu wa vyanzo kadhaa vya habari, Mbowe, ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) amekuwa katika mazungumzo yanayotajwa kwenda vizuri ili auziwe mtambo wa kufua umeme unaoitwa Kikuletwa, ulioko katika Jimbo la Hai, ili baada ya kununua aweze tena baadaye kuiuzia umeme TANESCO kama inavyofanyika kwa kampuni nyingine za uwekezaji nchini ambazo kwa muda sasa zimekuwa zikitajwa kuuza umeme kwa bei kubwa.

Raia Mwema
halikufanikiwa kumpata Mbowe kusikia maelezo yake, lakini mmoja wa viongozi wa kurugezi za chama hicho, John Mrema, amemweleza mwandishi wetu kuwa anayetaka kununua mtambo huo si Mbowe binafsi bali ni Halmashauri ya Wilaya ya Hai.

"Mbowe kama mbunge alikuwa akisaidia kufanikisha hilo. Mpango uliopo ni kununua mtambo huo wa siku nyingi ambao hautumiki ni kuukarabati na kisha kuanza kuzalisha umeme ambao sehemu itatumiwa na wananchi wa Hai na kiasi kingine cha umeme kitauzwa TANESCO," alisema Mrema.

Suala la kusimamishwa kwa uongozi huo wa juu wa TANESCO limevuta hisia nyingi huku makundi ya watu wakipita huku na kule kujaribu kubatilisha uamuzi huo, mengine yakidai kwamba taratibu za kuusimamisha zimekiukwa, mengine yakivurumisha tuhuma nzito dhidi ya uongozi wa wizara na mengine yakitaka Bodi nzima ya TANESCO iondolewe kwa vile baadhi ya wajumbe wa Bodi hiyo wamekuwa wakifanya biashara ya mafuta na shirika hilo.

Raia Mwema
limefahamishwa kwamba timu ya uongozi wa wizara jana ilikuwa Dodoma ambako iliitwa kwenda kujieleza mbele ya Kamati za Bunge zinazohusiana na TANESCO.

Tarifa zaidi zilizopatikana tukienda mitamboni zilieleza kwamba pamoja na kukutana na kamati hizo, timu hiyo ya wizara imeomba kukutana kwanza na kamati ya CCM ambako mtoa habari wetu ametufahamisha kwamba patamwagwa kila kitu hadharani kuhusiana na nani wanahujumu TANESCO, nani wanaofadika nayo na kwa njia zipi.

Kusimamishwa kwa Injinia Mhando na wenzake kulikuja kiasi cha siku tatu tu baada yaRaia Mwema kuripoti taarifa za kuwako makundi ya wafanyakazi wa Wizara ya Nishati na Madini na wenzao ndani ya mashirika na taasisi tanzu za wizara hiyo, wanaohujumu jitihada za sasa za kuisuka upya wizara na taasisi na mashirika yake.

Jitihada hizo, kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya habari serikalini, zimekuwa pia zikiwahusisha kwa karibu baadhi ya wenyeviti wa bodi za mashirika na taasisi hizo na watendaji wakuu wake ambao wanahisi ya kuwa, kwa mazingira mapya wizarani, ajira zao zinakaribia ukingoni kutokana na ama utendaji binafsi usiokidhi au kwa kushindwa kudhibiti uozo katika taasisi na mashirika yao.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, mtandao wa makundi hayo ulioungana ulikuwa ukiendesha kampeni ya kuukataa uongozi wa wizara kwa madai kwamba umekuwa ukiendesha mambo kibabe.

Raia Mwema
limedokezwa pia kwamba nje ya wizara, taasisi na mashirika yake, mtandao huo unaungwa mkono na baadhi ya wabunge, wengine wakiwa katika kamati zinazohusiana na wizara hiyo, na kwamba mipango iliyokuwa inasukwa ili kupeleka ujumbe kwa mamlaka husika kuwa uongozi wa wizara haufai, uondolewe, ni pamoja na kukwamisha bajeti ya wizara itakayowasilishwa bungeni wiki ijayo.

Hoja nyingine zanazodaiwa kushadidiwa na mtandao huo kama sababu za ziada kutaka mabadiliko ya uongozi wizarani ni kuwa Waziri mpya, Profesa Sospeter Muhongo, si mwanasiasa, ubunge wake uliompa uwaziri umetokana na yeye kuteuliwa na hilo linawakera baadhi ya wabunge wa majimbo ambao wanaona si vyema wao kuachwa, mtu wa "kuja" akapewa nafasi hiyo kubwa tena katika wizara inayotajwa kuwa tajiri na yenye ulaji kama ya Nishati na Madini.

Ukiacha hilo, Raia Mwema limeambiwa pia ya kuwa madai mengine ni suala ambalo chimbuko lake ni ukabila. Waziri Profesa Muhongo anatoka Mkoa wa Mara ambako ndiko anakotoka pia Katibu Mkuu, Eliachim Maswi, ingawa inafahamika kwamba wanatoka katika maeneo mawili tofauti ya mkoa huo. Kwa mujibu wa madai ya wana mtandao huo, Profesa Muhongo na Maswi kwa kutoka katika Mkoa mmoja na sasa wanafanya kazi ofisi moja ni tatizo.

Alipoulizwa na Raia Mwema juu ya madai hayo, mwanzoni mwa wiki iliyopita, Maswi alisema hakuwa na namna ya kuzuia watu wasizungumze wanayoyataka. Alisema yawepo au yasiwepo, yeye na timu wanayoijenga wizarani wameamua kufanya kazi ili kuleta tija katika maeneo waliyokabidhiwa kuyasimamia.

"Rais Jakaya Kikwete aliyetuteua hakufanya hivyo ili tuje hapa tuchezecheze. Tumepewa majukumu ya kutekeleza. Hebu niambie, nyumbani kwako siku hizi umeme unakatika mara ngapi?

"Ukiona kuna mawazo kama hayo, ujue tunafanya kazi. Sisi hatutajali yanayosemwa, kipimo chetu ni kama umma unaridhika. Kama unaona baadhi ya kero zilizokuwapo, zilizokuwa ndani ya uwezo wetu, sasa zimepungua kwenye vitu kama umeme, na kama tumeanza kupata stahili yetu kwenye maeneo kama ya migodi ujue wizarani sasa kuna wachapakazi," alisema Maswi.

Katibu Mkuu Maswi aliteuliwa na Rais Kikwete kuwa Kaimu Katibu Mkuu katikati ya Julai mwaka jana, kiasi cha mwaka mmoja uliopita, akichukua nafasi iliyokuwa imeachwa na David Jairo aliyekuwa ametuhumiwa na Bunge, pamoja na mambo mengine, kwa ubadhirifu.

Aidha, Profesa Muhongo, mmoja wa Watanzania wachache wataalamu wa jiolojia, amejiunga serikalini mwanzoni mwa Mei, mwaka huu, baada ya kuteuliwa na Rais Kikwete kwanza kama mbunge kupitia nafasi 10 za Rais kuteua wabunge kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mashirika yaliyo chini ya Wizara ya Nishati na Madini ni Shirika la Umeme (TANESCO) ambalo Mwenyekiti wake wa Bodi ni Jenerali mstaafu na mkuu wa zamani wa Majeshi, Robert Mboma, Mtendaji wake Mkuu ni Mhandisi Godfrey Mhando.

Mengine ni EWURA ambalo Mwenyekiti wake wa Bodi ni Simon Sayore; huku Mtendaji Mkuu akiwa Haruna Masebu; Wakala wa Umeme Vijijini (REA) ambalo Mwenyekiti wake wa Bodi ni Balozi Ami Mpungwe na Mtendaji Mkuu ni Dk. Dk Lutengano Mwakahesya; Wakala wa Madini (TMAA) ambalo Mwenyekiti wake wa Bodi ni Dk. Yamungu Kayandabila, Mtendaji Mkuu akiwa Mhandisi Paul Masanja.

Mengine ni STAMICO ambalo Mwenyekiti wa Bodi ni Ramadhani Omari Hatibu, Mtendaji Mkuu akiwa Grey Mwakalukwa; GST lililo chini ya Uenyekiti wa Bodi wa Profesa Idrissa Kikula na Mendaji Mkuu akiwa Profesa Abdul Mruma na TPDC ambalo Mwenyekiti wake ni Michael Mwanda na Mtendaji Mkuu ni Yona Kilagane.











 
shirika linazalisha zaidi ya bilioni 100 kwa mwezi, halafu linasua sua kussuply umeme?
bei ya nguzo ni kubwa kupita kiasi......


anyway...
pole zake huyo "kigogo" aliwazunguka wenzie nini?
 
This must be a plotted conspiracy. Kama serkali imeposti hizo hela kwenye akaunti je? Hapa lazima kufuatilia ziliingizwa lini ni na nani usije kuta wale waliokuwazuiliwa wasifanye mabo yao wameamua kuwafanyizi nchi hii si ya kwao . Madai hayo hayawezi kuaminiwa na yeyote zaidi ya mashabiki wake. Viserkali corrupt haviwezi kuaminiwa na wananchi. Na lazima viongozi wake hupigwa kwa mawe na wananchi wenye hasira.
 
Mambo mengi yanayofanana na haya yamekuwa yakiripotiwa lakini hakuna kinachofanyika. Hii inatuumiza sana sisi wananchi. Tutaponea wapi? Mzigo wote wa umeme tunaubeba sisi wanyonge kwa manufaa ya wachache! aaaaagh! hiviii ..........aaagh ngoja niwahi kutandika kitanda changu nijilalie mapemaaaa mie maana LUKU NAYO IMEISHA. LOL maisha gani haya???? ....
 
Hapo watauwana. Kuna mihela mingi humo ya ujanja ujanja. Unafikiri H. Clinton alikuja burebure? It is a life time investment. si tutakacho ni umeme tu ili tuweze kuwasha video na kucheza mziki kupunguza stress. Kupikia hatuwezi tunasubiri mikaa ya mkorosho at the end climate change itufagie wote.
 
kwani akaunti ya ridhiwani kikwete ina shilingi ngapi? mbona haizuiwi?
 
Mwandishi wa habari hizi ni wa gazeti la raia mwema, ambalo nalo limegeuka tena kuwa rai. Ukweli kuhusu tanesco ni jambo kubwa kama bahari ya hindi, hatujui sasa mkweli ni nani
 
Wizi unaofanywa na baadhi ya viongozi ndani ya Serikali ya Jk ni jambo la kawaida sana mnashangaa nini!!!?,au nyie ni wageni Tanzania.
 
hili gazeti nimeacha kulinnua baada ya kushindwa kusoma maandishi yake kila nikinnua
 
kama hizo habari ni kweli kuna haja ya kufanya complete overhaul ya TANESCO. tupate undani zaidi Tanesco wenyewe mpo tupeni undani zaidi, nchi hii inakwenda wapi ufisadi kila kona!!!
 
I see! kwa hiyo matatizo na shida tunazopata ni kwa ajili ya kufanikisha program za wateule wachache? Bilioni siku hizi imekuwa kitu cha kawaida ndani ya masikio yetu,mpaka tunaona kuwa ni hela ya kawaida tu(vijisenti).
lakini ninasikitika zaidi kuona kwamba, matatizo kama haya yanatokea na kuanikwa katika taasisi nyingi tu lakini hatuoni anayefikishwa mbele ya vyombo vya sheria! Jamani nafikiri watanzania tujifunze kusema ''sasa basi''.
 
Mimi kipande hiki ndicho cha mgao feki nisichokielewa..
Kwa mujibu wa taarifa zilizopo, kwa muda mrefu sasa kumekuwa na njama za kuandaa na kufanikisha mgawo ‘feki' wa umeme nchini kwa njia mbalimbali. Lengo la mgawo huo ni kuwanufaisha baadhi ya vigogo TANESCO kwa njia ya ununuzi wa mafuta ya kuendeshea mitambo.
Sasa kama utakata umeme hayo mafuta sii hayahitajiki? ukiwasha mitambo yote ndipo mafuta zaidi yanapohitajika hivyo supply lazima iwepo kumudu demand. Unapoondoa Demand inakuwaje wanafaidika na supply? kama wanazima makusudi wakati mafuta yapo imechunguzwa na kubainika stock iliyopo?
 
Hapo watauwana. Kuna mihela mingi humo ya ujanja ujanja. Unafikiri H. Clinton alikuja burebure? It is a life time investment. si tutakacho ni umeme tu ili tuweze kuwasha video na kucheza mziki kupunguza stress. Kupikia hatuwezi tunasubiri mikaa ya mkorosho at the end climate change itufagie wote.
Hahahahha umenifurahisha lakini point tupu!!
 
huo ni uonevu na kutoana kafara...kuanzia Rais baraza la mawaziri wakurugenzi wa mashirika ya umma na mabenki wote watuonyeshe akaunti zao i can guarantee you hakuna hata mmoja akaunti yake ina chini ya shs billion 1....waache ku deal na small fish...tunawataka wale mapapa
 
kama hizo habari ni kweli kuna haja ya kufanya complete overhaul ya TANESCO. tupate undani zaidi Tanesco wenyewe mpo tupeni undani zaidi, nchi hii inakwenda wapi ufisadi kila kona!!!

Tuanze na meneja mahusiano Badra Masoud kama bado yupo Tanesco maana yeye alikuwa nambari moja kuhonga editors ili habari mbaya za TANESCO zisiandikwe kama wafanyavyo viwanda vya bia hasa Serengeti breweries na suala la pollution kwa wakazi, PPF kwa ubadhirifu. Sasa kama TANESCO imeanza basi nendeni na sehemu nyingine ambako kuna uozo.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom