Aga Khan kuwapima saratani ya matiti wanaume

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,316
33,125
HOSPITALI ya Aga Khan imeandaa kliniki maalumu kwa ajili ya kuwapima wanawake na wanaume kuona kama wanakabiliwa na saratani ya matiti.Meneja Masoko wa hospitali hiyo, Eva Kairuki alisema jana kuwa kliniki hiyo itafanyika kwenye hospitali hiyo jijini Dar es Salaam kuanzia Oktoba 2 hadi 16 mwaka huu.

Alisema kliniki hiyo pia itafanyika mjini Zanzibar Oktoba 9 katika Hospitali ya Mnazi Mmoja na kwamba katika kliniki zote madaktari na wauguzi bingwa wa hospitali hiyo na madaktari wengine watakaojitolea watawapima watu watakaojitokeza na kuwapatia matibabu bure.

“Hospitali yetu inaendesha mpango huu ikiwa na lengo la kuwahamasisha wanawake na wanaume kujenga mazoea ya kupima saratani ya matiti mara kwa mara ili waweze kutibiwa mapema ugonjwa ukiwa katika hatua za awali,”alisema Kairuki.

Alisema mwanamke mmoja kati ya wanawake tisa wanapatwa na ugonjwa huo barani Afrika na kwamba wanaume pia wanapatwa na ugonjwa huo ingawa ni kwa kiwango kidogo cha asilimia tano kati ya wagonjwa wote. Alisema kazi kama hiyo ilifanyika mwaka jana ambapo wanawake 700 walijitokeza na wale waliokutwa na saratani walitibiwa bure.

Alisema mwaka huu wanatarajia kuwa zaidi ya wanawake 2000 watajitokeza. Meneja Masoko huyo alisema matibabu ya ugonjwa huo ni wastani wa kati ya Sh 500,000 na Sh 3 milioni saratani ya matiti ikiwa katika awamu changa na inapokomaa gharama hizo huongezeka zaidi hivyo huwawia vigumu wanawake wengi kuweza kupata matibabu ipasavyo.

Alisema mgonjwa anapotambuliwa akiwa katika ngazi ya kwanza au ya pili uwezekano wa kupona na kutibiwa ni mkubwa tofauti na saratani hiyo inapokuwa katika ngazi ya tatu na nne kwani mgonjwa huwa ameathirika sana na matibau yake huwa magumu.

Alisema utafiti unaonyesha kuwa katika mataifa yaliyoendelea wanawake wanaokumbwa na ugonjwa huo wapo katika umri wa wastani wa miaka 35-36 wakati katika bara la Afrika wanaokumbwa na balaa hilo ni wenye umri mdogo wa wastani wa miaka 19 na 24 Tanzania ikiwa mojawapo

Chanzo: Aga Khan kuwapima saratani ya matiti wanaume
 
Back
Top Bottom