|
Mtoto wa miaka 15, amzalisha mama kwa njia ya upasuaji.

4th July 2007, 08:55 AM
Mwandishi Wetu
HabariLeo; Wednesday,July 04, 2007 @00:01
Si jambo la kawaida kusikia mtoto mwenye umri wa miaka 15 duniani kufanya jambo kubwa linalowashangaza watu wengi kwa kuwa umri kama huo kwa watoto wa Afrika hususani Tanzania huwa kidato cha kwanza na wengine huwa bado kumaliza hata shule ya msingi.
Lakini hivi karibuni kwenye mji wa Manaparai ulioko Kusini mwa Jimbo la Tamil Nadu, nchini India;mvulana Dhileepan Raj(15), mtoto wa madaktari wawili amefanikiwa kumzalisha mama mmoja mwenye umri wa miaka 20, kwa njia ya upasuaji katika hospitali inayomilikiwa na wazazi wake ya Mathi Surgical and Maternity Hospital kwenye Jimbo hilo.
Tukio hilo lilifanyika chini ya uangalizi wa wazazi wake ambao walikuwa wakirekodi tukio zima kwa njia ya video na kuwa kitendo hicho ni cha kustaajabisha na cha kwanza kutokea duniani kufanywa na mtoto mwenye umri kama huo.
Kutokea kwa tukio hilo nchini humo kumekuja baada ya baba wa mtoto huyo Dk. K. Murugesan kutaka siku moja mwanae aweke rekodi ya tukio la kitabibu ili jina lake liingizwe kwenye kitabu cha rekodi duniani kiitwacho Guinness Book of Records, tukio ambalo amelitimiza kwa kuweka rekodi ya jina lake kwenye kitabu hicho.
Rekodi kama hiyo ya upasuaji haijawahi kuwekwa wala kutokea duniani kwa mtu mwenye umri kama huo na kuwa bado tukio hilo linawashangaza wengi ambao wanajiuliza Dhileepan alipata ujuzi huo wapi na chuo gani kwa kuwa mtoto kama yeye kwa kawaida huwa hajamaliza masomo ya sekondari na kuhitimu chuo,ili aweze kupata uzoefu wa kufanya upasuaji kama huo.
“Dk.Murugesan mwezi uliopita alionyesha mkanda aliourekodi wakati mtoto wake akifanya upasuaji huo kwenye hospitali yao huko Munaparai nchini India,” anasema Dk. Venkatesh Prasad Katibu wa Chama cha Madaktari nchini India (IMA), na kuongeza kuwa kwenye mkanda huo , Dk. Murugesan anaonekana akimchoma ganzi mgonjwa huyo kabla ya mwanae kuanza kazi ya upasuaji.
“Tulipata mshtuko tulipoona tukio hilo lililokuwa likirekodiwa kwenye mkanda, anasema Dk. Prasad wakati akizungumza na vyombo vya habari, na kusema kuwa IMA wamemuambia Dk. Murugesan kuwa kitendo hicho ni kinyume na maadili na pia ni kitendo cha ukiukwaji wa sheria”.
Hata hivyo kuna madai kuwa Polisi nchini humo wamewakamata wazazi wa mtoto huyo ambaye anadaiwa kufanya upasuaji huo, kwa lengo la kutaka jina lake liingie kwenye kitabu cha rekodi cha dunia.
Habari kutoka vyanzo mbalimbali zinasema kukamatwa kwa Dk. Murugesan na mkewe kumekuja baada ya Chama cha Madaktari nchini humo kuonyesha mkanda wa video unaoonyesha Dhileepan Raj akifanya upasuaji huo , na kusema Afisa mmoja wa wilaya ya Tiruchirappalli kwenye mji wa Tamil Nadu, Ashish Vachani alitoa taarifa hizo za kukamatwa kwa shirika la habari la Associated Press (AP).
Hata hivyo Msemaji wa kitabu hicho cha rekodi za Dunia, Amarilis Espinoza, aliliambia Shirika hilo la habari kwa njia ya barua pepe kuwa kitabu hicho hakiwezi kuidhinisha na kuweka kwenye rekodi jina la mtoto huyo, kwa kuwa kufanya hivyo kutachochea ukiukwaji wa maadili na kuzorotesha huduma za kitabibu kwa kufanya vitendo vya mzaa kwa maisha ya watu.
Hata hivyo wachunguzi wa mambo wanasema kuwa Dk.Murugesan, anaweza kuwekewa pingamizi la kutotoa huduma hiyo na pia kufunguliwa mashitaka kwa kuruhusu mwanae kufanya upasuaji ambao kwa kitabibu hakuwa amepitia chuo cha udaktari , bali kwa mujibu wa baba yake alikuwa amemfundisha mwanae huyu kufanya kazi hiyo kwa muda wa miaka mitatu!.
Dk. Prasad anasema kitendo hicho kilichofanywa na Dk. Murugesan kwa kumruhusu mwanae kufanya jambo kama hilo sio kizuri kwa kuwa ni kinyume kabisa na maadili ya kitabibu, jambo ambalo baba wa Dhileepan anasema sio mara ya kwanza kwa mwanae huyo kufanya upasuaji na kuwa amekuwa akimfundisha mwanae huyo kwa muda wa miaka mitatu iliyopita.
Hata hivyo Dk. Murugesan alikiambia chama hicho kuwa nia yake ilikuwa ni kuona siku moja jina la mwanae (Dhileepan) liko kwenye kitabu cha rekodi duniani.
Habari za mtoto huyo kufanya upasuaji huo ambao ulifanyika mapema mwezi Mei mwaka huu, zilisambaa ambapo Katibu wa Afya wa Serikali, V.K Subbaraj alisema uchunguzi wa jambo hilo unafanywa ili kubaini tukio hilo na Dk. Murugesan kuchukuliwa hatua za kisheria ikiwa kitendo kilichofanywa ni cha ukiukwaji wa sheria.
Vyanzo mbalimbali vya habari vinasema kuwa lengo la familia hiyo ilikuwa ni kuona tu jina la mtoto wao linawekwa kwenye rekodi ya kitabu cha dunia, na kuwa baadhi ya madaktari wa serikali walio kwenye chama hicho cha IMA, ambao waliona mkanda huo wa video ukirekodi tukio hilo wamesema kitendo hicho ni kinyume na maadili ya taaluma yao.
Habari zaidi kuhusu kukamatwa kwa wazazi hao wa Dheileepan hazijapatikana, ili kujua nini kitatokea kwa madaktari hao, licha ya kuwa baadhi ya madaktari nchini humo wanasema huenda Dk.Murugesan akanyang’anywa leseni ya kufanyia kazi kwa kitendo chake cha kumruhusu mwanae asiye na leseni wala mafunzo yanayotambulika kutoka chuo cha utabibu kufanya upasuaji huo.
Makala hii imetayarishwa na Mwandishi Wetu kwa msaada wa intaneti.
|
Kuntakinte
JF Senior Expert Member
Join Date: Sat May 2007
Location: Matombo, Morogoro
Posts: 790
Thanks: 6
Thanked 3 Times in 2 Posts
|
|