Ilikuwa ni huko Tarime. Wananchi wakawa wamejiandaa kumpokea Waziri Mkuu "kwa mabango" ya kuhoji mambo mbalimbali. Polisi wakaona kwa sababu zao kuwa hilo halipaswi kutokea, wakawatia mbaroni raia wale. Mbunge wao akalalamika mbele ya Waziri Mkuu. Waziri Mkuu "akawakumbusha" Polisi kuwa kila mtu ana haki ya maoni n.k "akawaamuru" waachilie raia wale. Polisi wakatii. Watu wakashangilia na kuona Waziri Mkuu ni mtetezi wa Katiba na haki za raia. Wakamshukuru. Kati hayo yote, hakuna aliyemuuliza Waziri Mkuu*, ametoa wapi mamlaka hayo ya kuamuru polisi kumwachilia mtuhumiwa au mshtakiwa? Tukiamini kuwa Waziri Mkuu ana uwezo huo je itakuwa kosa kuamuru pia kuwa Waziri Mkuu ana uwezo wa kuamuru mtu ashikiliwe na Polisi au chombo kingine cha usalama (kama TAKUKURU?)
Utawala wa kiimla, huanza pale ambapo kiongozi anafikiri ana uwezo wa kuamuru jambo likafanyika hata kama hana uwezo huo kisheria. Binafsi, sipendi, tena sitaki, na ninakataa kabisa Waziri Mkuu kujivika madaraka asiyo nayo. Je, siku nyingine akimuamuru Polisi amtwange mtu risasi, polisi atatakiwa kutii amri hiyo? Je, akiamua kuamuru "mbaya wake" atiwe mbaroni kwa kisingizio chochote kwa tu yeye ni Waziri Mkuu, mtu huyo atiwe mbaroni.
Mhe. Waziri Mkuu, hauna mamlaka hayo, hauna uwezo huo kisheria. Niko tayari kusahihishwa kama Waziri Mkuu anayo mamlaka hayo!! Vinginevyo, akome kuamuru mambo yasiyo ndani ya uwezo wake. Katiba yetu inasema hivi kuhusu madaraka ya Waziri Mkuu:
52.-(1) Waziri Mkuu atakuwa na madaraka juu ya udhibiti,
usimamiaji, utekelezaji wa siku hata siku wa kazi na shughuli za
Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2) Waziri Mkuu atakuwa Kiongozi wa Shughuli za Serikali
Bungeni.
(3) Katika utekelezaji wa madaraka yake, Waziri Mkuu
atatekeleza au kusababisha utekelezaji wa jambo lolote au
mambo yoyote ambayo Rais ataagiza kwamba yatekelezwe.
53.-(1) Bila ya kuathiri masharti ya Katiba hii, Waziri Mkuu
atawajibika kwa Rais kuhusu utekelezaji wa madaraka yake.
(2) Serikali ya Jamhuri ya Muungano, chini ya mamlaka ya
Rais, ndiyo itakuwa na uwezo wa kufanya maamuzi juu ya sera ya
Serikali kwa jumla, na Mawaziri, chini ya uongozi wa Waziri Mkuu,
watawajibika kwa pamoja Bungeni kuhusu utekelezaji wa shughuli
za Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
NB* - Angalia sijatumia jina la Waziri Mkuu aliye madarakani. Nazungumzia mtu yeyote mwenye kushikilia nafasi hiyo. Katika hoja hii hata hivyo ninamzungumzia Mhe. Edward Lowassa (CCM - Monduli)

Reply With Quote

Follow Us Here