|
Ansbert Ngurumo
WABUNGE wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) someni alama za nyakati. Sikilizeni sauti za wananchi. Fanyeni kazi mlizotumwa. Acheni usaliti wa dhamira nzuri ya Watanzania waliowachagua.
Huo ndio ujumbe wangu wa leo kwa wabunge. Kila Mtanzania anajua ‘kosa’ walilotenda Jumanne wiki hii. Tumeona matokeo ya vikao vyao wanapojifanya kamati ya CCM kuhujumu hoja za msingi zinazoletwa na wapinzani wao.
Jambo moja ni dhahiri. Sauti ya wabunge si sauti ya wananchi. Wabunge wa CCM wanajitetea, hawatetei wananchi. Wabunge wetu wamejitenga na umma. Wameambatana na watawala.
Wabunge hawa wamewakana wananchi. Hawataki tena kuwa wawakilishi wao. Wanawakilisha nafsi zao na za viongozi wao. Wabunge wetu wametukana. Wameishiwa maswali na hoja. Sasa wananchi wanajisemea. Wanauliza. Wanahoji.
Sikiliza swali kuu wanalojiuliza wananchi: “Bunge ni mali ya nani?”
Kwa bahati mbaya, wabunge wetu wanadhani ni lao! Wananchi wamekerwa na ubabe na maigizo kwa heshima ya CCM. Sikiliza sasa kauli ya wananchi:
“Wabunge wasiwe mawaziri. Michezo ya kuigiza Bungeni mwiko. Spika acha ubabe. Samwel Sitta ajiuzulu hajatenda haki. Ahadi ya rais ya madini iko wapi? Mfumo wa uchumi umefanya wananchi mataahira na iwe isiwe, ukweli utakuwa kweli daima.”
Kama Rais Jakaya Kikwete, waziri Mkuu Edward Lowassa na Spika Samuel Sitta wanataka kujua wananchi wanawaza nini, wasome maneno hayo kwa umakini mkubwa. Wayatafakari kwa kina. Hiyo ndiyo kauli ya wananchi. Wamedhihirisha hivyo wiki hii katika maandamano na matamko kadhaa.
Vitisho dhidi yao havisaidii. Sheria, madaraka na haki ya Bunge ya mwaka 1988 haina nguvu kuliko kauli ya wananchi. Bunge linataka kulazimisha heshima kutoka kwa wananchi wanaoanza kulidharau na hata kutaka livunjwe. Je litaweza?
Katibu wa Bunge, Damian Foka, anadiriki kuwakejeli wananchi wanaoandamana kupinga hatua ya Bunge dhidi ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini ambaye wabunge wa CCM walimlia njama na kumsimamisha kazi.
Foka anawaita eti “wanaojiita wanaharakati.” Kwani ni akina nani? Hizo wanazofanya si harakati? Lakini wanaharakati wenyewe wamekuwa waungwana, hawajawasema wabunge kwamba “wanajiita wabunge.”
Ajabu! Viwango na kasi vya Spika, Samuel Sitta, vimemezwa na mbwembwe za CCM. Sitta kwisha!
Na kitakachomponza Sitta ni udhaifu wake mwenyewe kwa kujipendekeza kwa serikali na kuendekeza urafiki. Woga wake kwa waziri mkuu na rais ndiyo unamfikisha hapa. Laiti asingewaogopa wanamtandao wenzake, sasa hivi Bunge lingekuwa na kanuni mpya ambazo zingeepusha aibu hii.
Matukio haya ya kauli na maandamano ya wananchi ni mwanzo mpya wa harakati mpya za kisiasa nchini Tanzania. Ni ishara kwamba wananchi wamechoka na wameamua kuanza kuchukua hatua.
Ukimya wao ulitumiwa vibaya. Sasa wameamka. Wamegundua kwamba waliokabidhiwa dhamana ya kuongoza nchi wanaipeleka watakavyo kwa sababu wana wabunge wengi. Waliopewa dhamana ya kuwasahihisha, kuwasimamia na kuwakosoa watawala, wanawasifu na kuwaangukia!
Nchi inageuzwa jalala la wageni. Wananchi wanaambulia ajira za kuitwa vibarua. Wanaendelea kuwa maskini na kuendeleza wanaosaini mikataba inayofichwa na walio madarakani.
Somo la historia walilosoma huko nyuma juu ya wakoloni walivyoingia na kusaini mikataba na machifu wetu waliopewa shanga na bunduki wakawauza watu wao; sasa limeanza kuzama na kufanya kazi ndani ya vichwa vya Watanzania.
Wamegundua kwamba wasipoamka sasa nchi hii itarudi katika ukoloni mwingine mbaya zaidi unaoongozwa na dhana ya utandawazi. Watawala wetu wa sasa, kama walivyokuwa machifu wetu, wamekuwa maswahiba na “watumishi” wa wakoloni wapya wanaotusainisha mikataba na kuchimba utajiri wetu, kasha wakaturushia makombo, wabunge wakashangilia.
Wananchi wamegundua kwamba watawala wetu wamepofuka kiasi cha kuyaona makombo hayo kuwa ni faida kwa taifa; faida inayowalamizimisha kuwapigia magoti wanyonyaji na kuwakemea wenye mali wanapohoji mazingira na umuhimu wa mikataba hiyo.
Tusipojihadhari, Tanzania sasa inanyemelewa na ombwe la uongozi. Wenye akili wanajua kwamba wananchi wakishamalizana na wabunge wataelekea wapi. Hawako tayari kuacha nchi iwe “tena” na ombwe la uongozi!
Wanasema: “Hapana. Hatuwezi kukubali ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya viturudishe kwenye utumwa mpya. Kama mmeshindwa kutuongoza, tutajiongoza. Kama mnashindwa kututetea, tutajitetea. Kama mmeshindwa kubadili kanuni dhalimu tutazivunja, maana yake hizi ndizo mnazotumia kuhalalisha ubabe na vitisho!”
Haya ndiyo ndiyo maswali muhimu ya leo kutoka kwa wananchi kwenda kwa Bunge, akiwamo rais. Ni maandamano na kauli nzito ni itangazo rasmi kwamba wawakilishi wa wananchi wameshindwa kazi, na wanakula msharara wa bure.
Kumbuka kwamba wiki iliyopita yalifanyika maandamano mengine ya wafanyakazi kulaani maisha duni yanayosababishwa na serikali inayoishi peponi.
Wananchi hawa si wajinga. Wanajua kuwa Tanzania ni nchi yenye madini mengi tu. Lakini wanajua kuwa madini hayo yanajenga miji na majiji makubwa ya Ulaya, Canada na Marekani, huku Kahama, Mererani, Geita, Tarime na kwingineko kukibaki mashimo, vumbi, magonjwa na vifo vitokanavyo na utajiri wa madini tulipewa na Mungu, na viongozi wetu wakaugawana na wageni.
Kinachowashtua wananchi ni kwamba tumefikia mahali pa kuyafuata makombo hayo hata nje ya nchi. Yaani mawaziri wameanza kutembea na mihuri mfukoni hata wakiwa safari za nje, kubembeleza na na kujikomba kwa wawekezaji!
Wananchi wanasema hapana, wabunge wanatoa vitisho? Wanamtetea nani? Nchi ni ya wawekezaji au wananchi?
Tumewahi kuhojiana sana huko nyuma. Hivi kama Mwalimu Julius Nyerere na wenzake wangeamua kukomba madini haya, kizazi hiki cha akina Jakaya Kikwete, Edward Lowassa, Rostam Azizi, Samule Sitta, Nazir Karamagi kingeyakuta? Hizo safari za kwenda kusaini mikataba London zingekuwepo leo?
Naomba niwakumbushe watawala wetu kwamba wananchi wanajua kuwa sasa hivi nchi yetu, Bara na Visiwani inaongozwa kirafiki. Lakini urafiki si hoja kama wahusika wangetimiza wajibu wao na kuleta mabadiliko waliyotuahidi.
Tazama timu hii. Amani Karume, Jakaya Kikwete, Edward Lowassa, Samuel Sitta, Nazir Karamagi, Rostam Azizi… Orodha ni ndefu, ila hawa ndio wanaozungumzwa inapoibuka hoja ya urafiki. Ni marafiki wa kweli kweli, na wa muda mrefu. Unapozungumza mtandao, hawa ndio vinara; wanaobaki ni wafuasi.
Unapomgusa mmoja unawagusa wote hao. Ndiyo maana ilikuwa rahisi kuzima ‘kasi’ ya Sitta alipodiriki kuleta kanuni mpya za Bunge haraka haraka. Kwamba bado ziko mafichoni leo, hata baada ya kamati ya Bunge kumaliza kazi yake muda mrefu, ni kwamba zilikuwa zinapitiwa, kuchunguzwa na kuhaririwa.
Zitto Kabwe alipomgusa Karamagi, alikuwa anapambana na kundi zito. Nadhani anajua kwamba Karamagi aliposaini mkataba huo jijini London alikuwa ameambatana na Rais Kikwete katika ziara ya kikazi. Hivyo, huwezi kumshitaki Karamagi kwa Kikwete, kwa kuwa wote wanajua jinsi mkataba ulivyosainiwa.
Hii ndiyo inawapa jeuri wabunge kama Ruth Msafiri (Muleba Kusini - CCM) kuhoji: “itakuwaje Zitto amlalamikie Karamagi wakati mamlaka iliyomteua (rais) haijamlalamikia?” Kama Kikwete angekuwa na uwezo wa kulalamika, angelalamikia huko huko London kabla Karamagi hajatia saini mkataba.
Hivyo, Zitto pia hakujua kwamba anapambana na mamlaka kubwa. Kama alijua, basi hilo ndilo linamfanya shujaa leo.
Hasira za wananchi ni kwamba Bunge haliongozwitena na Spika, bali viongozi wa serikali. Wanahesabu idadi ya vikao vya wabunge wa CCM kama kamati ya CCM kila wanapokumbana na hoja nzito inayotetea maslahi ya wananchi. Wanamlaumu Sitta kwa kuwa mnyonge hivi, na mtiifu kwa kanuni alizokwishasema kwamba hazifai. Yanasemwa kiasi kwamba hata sisi tulio mbali tunayasikia. Wao hawayasikii? Au ndiyo jeuri hiyo?
Watu wanajua kuwa Karamagi ni mfanyabiashara mkubwa, na ana ushirika na baadhi ya hao niliowataja juu, na wanajua Baraka hizi zinatoka wapi na kwa nini? Wananchi wanajua mengi, ila wamekuwa kimya kwa muda mrefu, wakabaki kuyasambaza haya mitaani na mitandaoni. Wanaogopa kusema ili ‘lisitoke kwao.’
Lakini usiri uliotawala katika sokomoko la mkataba wa Buzwagi ndio uliowaamsha. Zaidi ya hayo, vitisho ambavyo serikali inajaribu kutumia sasa kuzima sauti zao na harakati zao.
Wanashangaa kwamba wabunge wao, waliokuwa wanadai serikali iape mikataba kwa sababu ina utata, sasa wamepata fursa ya kuibana serikali walau iwaonyeshe mkataba huu; wanaishia kusema “maelezo ya waziri yanajitosheleza.”
Ama ni uwezo mdogo wa kuchambua majibu ya waziri au ni uoza tu wa dhamiri kwa ajili ya kulindana. Nimefuatilia neno kwa neno mjadala wa Bunge tangu Zitto Kabwe alipotoa hoja yake hadi John Malecela alipohitimisha hukumu ya wabunge! Sikuona mbunge hata mmoja wa CCM aliyetumia akili ya ziada kuona kwamba majibu ya waziri yalihitaji uchambuzi wa kina na maswali ya ziada.
Wananchi wamegundua kwamba wabunge wa CCM walishangilia mbwembwe za Karamagi ‘kumzodoa’ Zitto lakini si kiini cha hoja.
Bunge linaposema Zitto Kabwe amesema uwongo, wanannchi wanahoji. Uwongo gani?
Zitto Kabwe alisema mkataba haukusainiwa Tanzania. Ni kweli. Alisema mkataba ulisainiwa na waziri. Ni kweli. Alisema waziri amesaini mkataba nje ya nchi, London. Ni kweli. Alisema aliusaini mwezi wa pili. Ni kweli. Kabwe alisema waziri alilificha Bunge taarifa hizo. Ni kweli.
Alihoji ‘haraka ya nini?’ Waziri akajibu ‘ili tuspipoteze fursa iliyojitokeza.’ Zitto Kabwe akauliza ‘unadhani dhahabu ingeoza kama ndizi?’ Wananchi wanajua kuwa haiozi. Akasema mkataba ule ni mbaya, ulete tuuone. Waziri hataki! Ajabu! Hata wabunge wanaomshangilia waziri hawajauona mkataba.
Kama Spika na wabunge wanabaki wamekumbatia kanuni mbaya, hawaoni hisia na maswali ya wananchi, basi kazi imewashinda. Wananchi sasa wanaona kwamba Bunge linageuzwa ukumbi wa sinema.
Wanasikitikia hoja za kujidhalilisha zinazotolewa na wabunge wao, hasa wa CCM. Wakato Msafiri anadai kwamba serikali yetu inatenda kazi kwa uaminifu mkubwa, wananchi wanaitilia shaka, kwani kama ingekuwa na uaminifu huo, hata Rais Kikwete asingesema tupitie mikataba ya madini.
Na kama serikali ingekuwa inatenda kazi kwa uaminifu kisi hicho, hizi kashfa tunazosikia zisingekuwapo, wala isingefanya njama kuzima harakati za kuunda kamati ya Bunge kuchunguza.
Nilitarajia wabunge washangae na wahoji usiri wa Karamagi hadi suala hili lilipoibuliwa na Zitto Kabwe.
Kama hawawezi kutilia shaka mwenendo huu, wanafanya nini Bungeni? Kutii kanuni?
Baadhi wanasema majibu ya Karamagi yameleta utata wa ziada, kwani wakati anasema kupitia upya mikataba kumemalizika Novemba mwaka jana; Rais Kikwete katika mahojiano na Redio Sauti ya Amerika (VOA) mapema mwezi huu alidokeza kwamba upitiaji mikataba haujaisha.
Wabunge walishindwa kuhoji sababu ya mgongano huo. Na kama shughuli hiyo ilishakamilika, mbona Karamagi hakueleza hadi lilipoibuliwa na Zitto Kabwe?
Wakati akina Suleiman Kumchaya wanamnukuu Mwalimu Julius Nyrere kwamba haraka ya waziri kusaini mkataba inaenda sambamba na kauli ya Mwalimu Nyerere kwamba “wakati wenzetu wanatembea sisi tukimbie;” wananchi wanamhoji Kumchaya kuhusu mbio hizi.
Mwalimu Nyerere alisema tukimbie kuelekea wapi? Tuwaachie wageni madini? Si ni huyu huyu aliyesema hayaozi?
Mwalimu angefurahi kama tungekimbilia kuwekeza katika elimu, teknolojia na mtaji ili tuweze kumiliki raslimali zetu kwa faida yetu. Lakini tukimbilie London “kuuza” mali za Watanzania kbla hawajazinduka?
Bado wananchi wanajiuliza kwa nini Mudhihir Mudhihir, Hafidh Ali na John Samuel Malecela waliacha mianya yote hii wakakimbilia kumshindilia mbunge mwenzao aadhibiwe, huku Malecela akionya kwamba watakaofanya kama Zitto watashughulikiwa hivyo hivyo?
Hapo ndipo swali la wananchi “Bunge ni mali ya nani?” linapopata uzito. Huu ndiyo uzoefu tunaoambiwa?
Kweli, wananchi wana hasira. Na sasa wameanza kuona hasara ya kujaza wabunge wengi wa CCM Bungeni. Wanatamani wangekuwa na kina Zitto Kabwe walau 50 tu. Wanakerwa na bunge kuwa kamati ya CCM. Wanakerwa na wabunge kulinda urafiki wao na wakubwa badala ya kutetea wananchi wao.
Mwananchi mmoja alinitumia ujumbe huu Jumatano asubuhi:
“Nina hasira nyingi juu ya mambo yaliyotokea bungeni jana. Kwa kweli siamini kuwa nchi hii imechagua wabunge wapuuzi kwa kiasi hicho. Kwa hakika, hata kujikomba huku kunakoonyeshwa na baadhi ya wabunge wa chama tawala kumevuka mipaka ya uvumilivu; yaani wamegeuza jumba letu kama kijiwe cha kuvunia maslahi?”
Wabunge wetu ndivyo mnavyoonekana. Wakati tukitafakri sakata hili, tukumbuke kauli za Rais Kikwete na Sitta siku lilipozinduliwa jengo jipya la Bunge, Dodoma, Juni mwaka jana.
Rais Kikwete alisema: “Jengo hili, si tu kwamba linapendezesha sura ya mji wa Dodoma, bali pia linaipa haiba mpya demokrasia yetu. Hiki ni kiota cha mijadala muhimu ya kitaifa, mijadala itakayoamua mwelekeo wa demokrasia yetu, hatima ya maendeleo yetu na mustakabali wa taifa letu.
“Kwa ninavyoelewa mimi, jukumu la msingi la mbunge ni kuyapa sauti matumaini, matarajio na matakwa ya watu wetu. Wabunge ni vipaza sauti vya Watanzania waliowachagua. Bila shaka kwa kuutumia kwa ukamilifu ukumbi huu wa Bunge ulio mzuri na wenye vifaa vya kisasa, sauti za Watanzania zitasikika bila mikwaruzo. Aidha, matarajio yao yatawasilishwa, kujadiliwa, kufanyiwa kazi na kupatiwa majibu kwa ufanisi zaidi sasa.”
Sitta alisema: ““Mazingira mapya ya jengo hili lenye huduma bora zaidi za kibunge hayatakuwa na maana ikiwa sisi wabunge wa Bunge hili hatutakidhi matarajio ya nchi kuhusu utendaji bora zaidi na wa makini zaidi katika kupambana na maovu ya rushwa, uzembe, huduma zenye usumbufu kwa wananchi na ulegevu wa kila aina unaowazuia Watanzania kuyafikia maisha bora kwa kasi inayojenga matumaini.
“Tunaposherehekea kuanza kutumika kwa ukumbi mpya wa Bunge, sisi wabunge tunao wajibu wa kuweka dhamira ya dhati na kujipanga upya ili tutimize majukumu yetu ya kikatiba kwa namna ambayo itaongeza tija na kuimarisha imani ya wananchi kuhusu Bunge lao.”
Wananchi wamegundua kumbe zilikuwa kauli tupu! Wananchi wanazikumbuka, wabunge wameshazisahau! |
|