JUMAPILI, SEPTEMBA 23, 2012 10:38 NA MWANDISHI WETU, KAHAMA
*Kauli zake zadaiwa kuichimbia ‘kaburi’ CCM
*Mgeja adai amekuwa kama mbogo aliyejeruhiwa
*Nalaila Kiula aibuka, aonya kugawana vyeo
*Asema kama si mtoto wa kigogo huchaguliwi
MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja amesema kitendo cha Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta kwenda mbele ya wanafunzi wa darasa la saba kuishushia tuhuma nzito CCM, ni sawa na kukichimbia kaburi chama hicho.
“Sita anazidi kuichimbia kaburi CCM, amekuwa na kauli ambazo hazifai kutolewa mbele jamii…iweje aendee kumwaga ***** mbele ya wajukuu zake,”alihoji Mgeja.
Akizungumza na MTANZANIA Jumapili jana, Mgeja alisema Sitta ameshindwa kuonyesha ukomavu wa siasa akiwa kiongozi wa Serikali kwa sababu hakupaswa kuropoka maneno mazito mbele ya wanafunzi wa shule ya msingi.
Juzi, Sitta ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mahafali ya 11 ya shule ya Msingi Kwema wilayani Kahama, alisema ndani ya CCM kuna viongozi mafisadi wanaopaswa kuondolewa mara moja.
“Nimesikitishwa mno na kauli ya Sitta kwa sababu yeye ni kiongozi wa Serikali, hakutakiwa kuzungumza maneno ya aina hii mbele ya wanafunzi wa shule za msingi … tena kibaya zaidi amekikashifu chama chetu vibaya,”alisema Mgeja.
Alisema Waziri Sitta, sasa anafananishwa kama mbogo aliyejeruhiwa ndani ya CCM na kumuomba Rais Jakaya Kikwete kuwa makini na kauli za mawaziri wake kwa sababu zinasababisha wananchi waendelea kuichukia CCM.
Alisema Sitta, alipaswa kutumia vikao husika ndani ya chama ambavyo vinaweza kushughulikia matatizo yaliyopo ndani ya CCM.
“Kitendo cha kuwahutubia wanafunzi wa darasa la saba kuhusu mambo ya ufisadi ni jambo la hatari sana. Sitta alipaswa kuwaeleza juu mifumo ya mitihani yao ambayo imekuwa ikibadilika mara kwa mara au Watanzania wamejipangaje kukabiliana na changamoto za Soko la Pamoja la Afrika Mashariki, hapa tungesema wazi amewasaidia watoto wetu.
“Wale wanafunzi walipaswa kuelezwa vizuri athari za kubadilika kwa mitaala ambayo huwaathiri masomo.
“…kuwashushia tuhuma za ufisadi ni aibu. Watanzania wa leo wamechoshwa na maneno ya mafisadi ndani ya Serikali, wanataka vitendo,” alisema.
Alisema mambo anayofanya Waziri Sitta ni kampeni chafu ambazo zinalenga kuwachafua na kuwabeba wagombea wengine katika uchaguzi mkuu ujao ndani ya CCM.
Alisema katika ziara yake mkoani Kagera, Waziri huyo alisema maisha bora kwa kila Mtanzania ni kama ndoto, hali ambayo inaonyesha wazi anapingana na kauli ya Mwenyekiti wa CCM,Rais Jakaya Kikwete.
“Waziri amekosa maneno ya kuwapa matumaini Watanzania na kusababisha kuzungumza maneno kama hayo ambayo yanasababisha kukichimbia kaburi Chama cha Mapinduzi katika uchaguzi Mkuu ujao 2015,” alisema Mgeja.
Mmoja wa wananchi ambaye alizungumza na MTANZANIA Jumapili,Sued Mussa alisema: “Kitendo cha Waziri Sitta kuendelea kulalamika mara kwa mara tena kwa wanafunzi ambao ni wajukuu zake, ni kukimwagia CCM sumu baridi ambayo ni hatari kuliko sumu ya kawaida.”
Alisema Sitta kuzungumzia watu wana vitambi, ni hoja mufilisi kutokana na ukweli kuwa wakati huu wananchi wanataka kutatuliwa kero za maisha zinazowakabili.
“Namshangaa mno kwa sababu alipokuwa Spika wa Bunge sikuwahi kumsikia akitetea maslahi ya wakulima au wafanyakazi, zaidi ya kusikia akitaka mafisadi waondeke ndani ya chama tena kibaya zaidi bila kuwataja majina,”alisema.
Alisema alipaswa kuzumgumzia mambo ya msingi na changamaoto zilizopo katika Wilaya ya Kahama, kama vile kuwapo migodi mikubwa ya dhahabu na kilimo cha mpunga ambao wananchi wa wilaya wamekuwa wakihangaika nacho miaka nenda rudi.
Juzi akiwa wilayani Kahama ambako alialikwa kuwa mgeni rasmi katika mahafali ya 11 ya Shule ya Msingi Kwema, Sitta alisema uchaguzi unaoendelea ndani ya CCM umevurugika kutokana na kuingiliwa na mafisadi kupata viongozi ambao watalinda maslahi yao.
NALAILA KIULA
Naye aliyewahi kuwa Waziri wa Ujenzi katika Serikali ya awamu ya tatu, Nalaila Kiula ameibuka na kudai Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinaelekea kuwa chama cha familia kutokana na kundi la wototo wa vigogo kuwania nafasi za uongozi.
Akizungumza na MTANZANIA Jumapili mjini Dar es Salaam juzi, Kiula alisema hali ndani ya CCM inaendelea kuwa mbaya kutokana na viongozi walio madarakani kuandaa familia zao na kuzipatia nafasi ndani ya chama.
Alisema ameshangazwa na kitendo cha mke wa kiongozi wa juu kuwania ujumbe wa Halmashauri Kuu (NEC), jambo ambalo halitoi picha nzuri kwa jamii.
“Hakuna busara inayotumika ndani ya CCM na viongozi waliopo madarakani yaani hata Rais Kikwete ameshindwa kushauriana na mke wake juu ya kugombea nafasi ya ujumbe wa NEC… haiwezekani nyumba moja itoe vichwa vitatu.
“Nimesikia mtoto wa kiongozi wetu wa chama amepita bila kupingwa, hii ni picha mbaya ndani ya jamii…lakini pia mke wa mheshimiwa naye kapita bila kupingwa, enzi za Mwalimu Nyerere jambo kama hilo halikuwapo ndani ya CCM.
“Natoa mawazo au ushauri huu kwa sababu nakipenda chama changu na siyo chuki. CCM imekuwa sultani na hali hii ya familia au ukoo mmoja kupewa nafasi kupata uongozi ndani ya chama itakipeleka pabaya kama ngome hii haitavunjwa mapema.
“Kwanza naiomba Kamati Kuu ya CCM imshauri mke wa mheshimiwa aondoe jina…namuomba Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama ajipange kukisafisha hususan wakati huu wa kutafuta viongozi, vinginevyo hali hii ikiendelea itakiharibu chama,” alisema.
Alisema kama CCM haitazingatia sifa katika kuwapata viongozi wazuri itaendelea kuwa katika migogoro na kugawanyika katika makundi mawili yanayokinzana mtazamo na maslahi ya taifa.
Alisema umefika wakati CCM kutenga muda wa kusikiliza hotuba zilizokuwa zikitolewa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere wakati wa uhai wake juu ya kupata viongozi waadilifu na wanaojali maslahi ya nchi na wananchi kwa ujumla.
Kama CCM itaendelea kupuuza ushauri unaotolewa na viongozi au wadau itazidi kufifia na kupoteza dira na kuvifanya vyama vya upinzani kutumia mwanya huo kuwarubuni wananchi, alisema.
Alisema katika hali ya kawaida asilimia kubwa ya viongozi wanaopata nafasi ndani ya CCM ni wale ambao baba zao au ndugu waliwahi kufanya ndani ya chama na wengine hupata kwa kutumia nguvu ya fedha.
Akizungumza harakati zilizoanza na baadhi ya viongozi kuonnyesha nia ya kugombea nafasi ya urais mwaka 2015, alisema wengi hao si waadilifu na wanagombea kuficha maovu yao.
Kitendo cha baadhi ya viongozi kuonyesha nia ya kugombea nafasi hiyo mapema inatokana na uchu wa madaraka, alisema.
“Wanaotaka kugombea urais mwaka 2015 ni viongozi sasa, hii ni tamaa ya madaraka na nimekuwa nikifanya tathmini yangu binafsi nimegundua wanataka kuficha maovu yao.
“Unajua siku hizi huwezi kumdanganya Mtanzania wa leo, tunafamu kinachotafutwa kupitia nafasi hiyo, watu wanafanya mambo yasiyotakiwa, sasa wanajua wakipata urais hawataguswa,” alisema.


Reply With Quote

Follow Us Here