
By
ndamo emmanuel
Ilikuwa Jumapili ya tarehe 9 Dec 2011 saa kumi na mbili asubuhi, nilikuwa nikitembelea bustani iliyoko nyuma ya Nyumba yangu. Miguu yangu ilipata mshituko wa ghafula niliposhuhudia jambo hili lililonikosesha amani, hadi nikaamua kuomba maoni kwa wasomaji wenzangu ili kupata nini hasa maana ya nilichokiona. Nilisikia mshindo mkubwa uliotokana na mwanguko wa kitu fulani kutoka katika mti mkubwa wa Mzambazau uliokuwa karibu yangu! Nilipotazama mbele yangu, nilimwona kinyonga aliyepasuka tumbo huku mayai yakitapakaa mahali pale, na alikuwa katika hatua za mwisho wa uhai wake. Mengi ya mayai hayo, yalikuwa yamepasuka yakiwa na mchanganyiko wa chembe za damu na ute mweupe kama wa yai la kuku lililoanza kutunga kifaranga! Wazo liliniijia kichwani niangalie kwa umakini zaidi,kwa maana niliwahi kusimuliwa na babu yangu kuwa kinyonga jike akipata mimba na mimba ile ikikua na kufikia muda wa kuzaa, kinyonga huyo hupanda mtini, juu kabisa ya matawi akaangalia chini na kulenga palipo na jiwe kubwa, au sehemu iliyo ngumu na akajiachia kutoka kwenye matawi ya mti huo. ili aangukiapo mwamba huo, tumbo lipasuke ili mayai yaliyokomaa tumboni mwake yapasuke vilevile ili watoke watoto walio hai baada ya yeye kufa, maana tumbo lipasukapo na uhai wake hufikia mwisho! Baada ya uchunguzi uliodumu kwa zaidi ya nusu hivi, ndipo nilipogundua yafuatayo: 1.Mzoga wa Kinyonga yule ulikuwa na mchanganyiko wa rangi ya KIJANI na MANJANO! 2. Kinyonga Yule mayai yake yalikuwa hayana dalili yoyote ya kukomaa, hivyo kupoteza matumaini na bahati nadra ya kushuhudia tukio la mwanzo wa maisha ya Vinyonga wengi watoto, walio matokeo ya mwisho wa maisha ya kinyonga jike mama yao! 3.Kifo cha kinyonga yule kilitokana na ajali baada ya kukatika tawi la mti lililoonekana pembeni kidogo ya mzoga ule! Nilikumbuka siku ya mdahalo ulioandaliwa na kituo cha katiba UDSM, mwezi mmoja kabla ya Rais kuridhia uandikwaji wa Katiba Mpya, Mchangiaji wa mwisho kabisa katika mdahalo huo Uliorushwa na kituo cha I.T.V, alikuwa mzee niliyemkadiria umri wa miaka 80 hivi, Na alisema yafuatayo………''Ili kinyoga aweze kuzaa na kuendeleza kizazi, lazima afe kabla ya watoto wake kuanza maisha.'' Akamaliza kwa kusema ‘’SITAKUFA HADI NITAKAPOSHUHUDIA KIFO CHA C.C.M’’ Niliondoka kwa huzuni bustanini, huku nikibaki na maswali mengi kadhaa yasiyo na majibu! Baadhi ya maswali yaliyokuwa yakipita kichwani mwangu ni kama yafuatayo! Nilijiuliza kuwa, Ikiwa kupasuka kwa tumbo la kinyonga yule yalikuwa ni maono juu ya kufa kwa C.C.M, Je mbona nisione mayai yakitoa watoto wa kinyonga kama ilivyo ada? Nini kitatokea ikiwa C.C.M itakufa na Isipate mrithi wa kuendeleza kizazi? Na ikiwa Mama atakufa na watoto tumboni, Nini Itakuwa Mustakabali wa kizazi kijacho kama sio GIZA? IKIWA MSOMAJI MWENZANGU UTAFIKIRIA MAONO JUU YA MAANA HALISI YA KIFO NA MATOKEO YA KINYONGA HUYU ‘’WA KIJANI NA MANJANO’’ KWA MUKTADHA WA KISIASA NCHINI TANZANIA, NISAIDIE KUBORESHA TAFSIRI YA MAONO HAYA. NOTE: NO PART OF THIS ARTICLE SHOULD BE REPRINTED NOR REPRODUCED FOR BUSINESS USES OTHER THAN IN JAMII FORUM WITHOUT PRIOR CONSENT OF THE AUTHOR. THANK U 0759-069406
Follow Us Here