............
Tangu mchakato huu wa kulipatia Taifa Katiba mpya uanze suala la Muungano limekuwa ndilo suala kuu linalotawala usanifu wa kisiasa wa Visiwani. Kweli tangu Muungano uasisiwe Aprili mwaka 1964 umekuwa ukizungumzwa na kujadiliwa sana na Wazanzibari pengine kushinda suala lolote jingine la kisiasa lakini safari hii hili ndilo suala kuu linalowashughulisha Wazanzibari.
Inavyoonyesha ni kwamba suala hili haliwashughulishi hivyo wenzetu wa Bara. Si kwamba hawalitii maanani lakini hawalipi kipaumbele kama ndugu zao(1) wa Visiwani.
Inayumkinika kwamba hili zoezi la kukusanya na kuyaratibu maoni ya wananchi litahitimishwa katika muda wa miezi sita ijayo. Litapomalizika sitostaajabu nikiwaona baadhi ya watu wakitahayari na kujaribu kuziziba nyuso zao. Hawa ni wale wasioamini kwamba Tume itayawakilisha vilivyo maoni inayoyakusanya Zanzibar(2).
Wana msimamo huo kwa sababu hadi sasa maoni hayo yamekuwa ni ya kutoa mapendekezo yenye kutaka pawepo mageuzi ya kimsingi hasa kuhusu muundo wa Muungano(3) na wana wasiwasi kwamba Tume ya Katiba haitokuwa na ujasiri wa kuyawakilisha kidhati maoni hayo.
Kwa hakika kwa hali ya mambo inavyoendelea nina hakika kwamba idadi kubwa zaidi ya wananchi wa Zanzibar wataendelea kuiambia Tume itapoanza tena shughuli zake Zanzibar kwamba wanataka pawepo na Muungano wa(4) nchi mbili lakini uwe Muungano wa Mkataba na si wa Katiba(5).
Haiwezi kuwa vingine kwani pendekezo hilo linazidi kuungwa mkono Visiwani ingawa wapo wenye kulipinga na wenye kushikilia kwamba muundo wa sasa wa Muungano usalie ulivyo. Huu wa sasa pia ni Muungano wa nchi mbili lakini ni wa Katiba.
Hivi karibuni wasomaji kadhaa wa Raia Mwema, wote wakisema wametoka Bara, wameniandikia wakinitaka nielezee zaidi juu ya Muungano wa Mkataba.
Mmoja ameandika kwamba wananchi wengi hasa Watanganyika hawaelewi nini maana ya Muungano wa Mkataba na kwamba huu ni wakati muafaka kama watapata fursa ya kuuelewa huu Muungano wa Mkataba kwa sababu wakiuelewa nao pia wataupendekeza(6) wakati wa kutoa maoni na hivyo kuongeza uzito badala ya kuwaachia Wazanzibari peke yao.
Msomaji huyo ameendelea kuandika kwamba kwa hali ilivyo sasa hatima ya Muungano, uwepo au usiwepo, na aina gani ya Muungano kama utakuwepo, itaamuliwa na Wazanzibari “kwa sababu Watanganyika wengi wanaona vyote sawa isipokuwa viongozi…”
Kwa hakika si jambo la kushangaza kuona kwamba hisia kuhusu Muungano ni kali mno Visiwani kushinda Bara kwa sababu Wazanzibari ndio wenye kudai kwamba muundo uliopo sasa wa mahusiano kati ya Tanganyika na Zanzibar hauna manufaa kwao.(7)
Hivyo wanahisi kwamba ni chaguo lililo wazi kwao iwapo wanataka kuendelea na umbile la sasa la Muungo lenye muundo wa Kikatiba au pawepo na umbile mbadala la Muungano utaojengeka juu ya misingi ya Mkataba(8).
Nini tofauti ya aina hizo mbili za Muungano? Lile umbile la Muungano wa Katiba linakuwa na dola moja yenye kuhodhi mamlaka yote ya ndani na ya nje ya nchi na linaiwezesha Tanganyika kuyasimamia kwa ukamilifu yale yanayoitwa ‘Mambo ya Muungano.’
Wakati huohuo, Zanzibar inapoteza mamlaka yake kamili na uhuru wake wa kujiamulia itakavyo mambo yake ya ndani na ya nje na inakuwa na jukumu tegemezi ndani ya Muungano wake na Tanganyika.
Lile umbile la pili, la mbadala, ni la Muungano wa nchi zilizo huru na kila moja ikiwa na mamlaka kamili na uhuru wa kujiamulia mambo yake ya ndani na ya nje. Nchi hizo zitaunganishwa kwa Mkataba(9).
Muungano utaojengwa kwa Mkataba utairejeshea Tanganyika na pia Zanzibar mamlaka yao kamili ya kidola na utawezesha kuwapo utaratibu wa ushirikiano kati ya nchi mbili zilizo sawa(10) na zilizo huru na zenye mamlaka kamili ya kidola.
Mkataba, utaokuwa msingi wa Muungano huo, utaeleza wazi nchi hizo zitashirikiana juu ya mambo gani na namna ushirikiano huo utavyokuwa(11).
Jambo jingine la kuvutia katika Muungano wa Mkataba ni kwamba kila nchi itayotia saini mkataba wa muungano huo itakuwa na nguvu ya kutumia kura ya ‘turufu’ (veto). Hivyo hata katika jambo lililokwishakubaliwa kuwa la Muungano nchi fulani inaweza kuitumia nguvu yake ya turufu na kupinga pale itapohisi kwamba utekelezaji wa sera kuhusu jambo hilo unaihatarisha hiyo nchi au unakwenda kinyume cha maslahi yake.
Uzuri mwingine wa umbile hilo ni kwamba utaweza pia kuzivutia nchi nyingine zijiunge na Muungano huo kwa vile hakuna nchi itayohisi kwamba itaweza kumezwa na nyingine. Umbile hili la Muungano haliipi nchi yoyote nafasi ya kujitwika dhima ya ‘ukaka’ na kujifanya kuwa ni adhimu kwa sababu ya ukubwa wake uwe wa eneo au mwingineo.
Nchi zote zilizo ndani ya Muungano aina hiyo wa Mkataba zinakuwa na usawa bila ya kujali ukubwa wao au kima chao cha maendeleo. Sheria ya kimataifa na jumuiya ya kimataifa huziangalia nchi zote hizo kwa jicho moja na huziona kuwa ni sawa mbele ya sheria ilimradi kila moja ya nchi hizo iwe huru na iwe na mamlaka yake kamili ya kidola na ya utawala.
Mazingira ya kilimwengu katika milenia tuliyo nayo hayashajiishi wala kutia moyo kuwako kwa mahusiano kati ya nchi huru kama yalivyo sasa baina ya Tanganyika na Zanzibar ambamo nchi moja inaonekana ni ‘mshiriki mkuu’ na nyingine ‘mshiriki mdogo’(12)
Hapo ndipo panapozuka ile dhana ya kwamba mshiriki mdogo ameyahaulisha mamlaka yake ya utawala kwa mshiriki mkuu.
Mfano mzuri wa Muungano wa Mkataba ni ule Muungano wa Ulaya(13).
Kutoa mfano wa Muungano huo si kukiri kwamba huo ndio aina ya Muungano uliokamilika. La. Tusemacho ni kwamba ni mfano mzuri wa aina ya Muungano ulio bora kushinda huu tulio nao. Najua kwamba suala la ‘ukaka’ kuna wataoruka na kusema mbona Ujerumani na Ufaransa zinajifanya makaka katika Muungano wa Ulaya? Ni kweli kwamba nchi hizo mbili hujaribu kujitutumua katika masuala ya kiuchumi hasa yale yanayohusika na sarafu ya euro lakini haziwezi kushurutisha lolote kisiasa kwani lazima zifuate mkataba uliopo.
Mfano mwingine wa Muungano ulio bora kuliko huu tulionao ni ule Muungano wa Senegambia(14)
ulioziunganisha nchi mbili wanachama wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU) yaani Senegal na Gambia toka mwaka 1982 hadi 1989.
Muungano wao ulikuwa aina ya Muungano wa Mkataba na uliunganisha majeshi ya nchi hizo, pia uliunganisha mambo yao ya uchumi na fedha, uliratibu sera zao za mambo ya nje na mawasiliano na ulianzisha taasisi za Muungano. Urais wa Muungano huo ulikuwa ushikwe na Senegal ambayo pia ilikuwa iwe na thuluthi mbili ya viti vya Bunge la Muungano. Hata hivyo, juu ya kuwapo kwa Muungano huo kila nchi iliendelea kuwa na uhuru wake.
Mkataba huo wa Muungano ulianza kutekelezwa mwezi Julai mwaka 1982 lakini kwa bahati mbaya Muungano huo ukavunjwa mwaka 1989 kwa sababu Gambia ikilalamika kwamba ikiingiliwa na Senegal katika uhuru wake na mamlaka yake.(15)
Kama pana nia ya kuwa na Muungano wa dhati utaopelekea kuungana kwa Bara la Afrika basi suluhisho la matatizo yanayoyakabili mahusiano kati ya Tanganyika na Zanzibar lipo katika kuundwa kwa Muungano wa Mkataba. Hiyo si ndoto.
Jambo linalowahamasisha Wazanzibari watake Muungano wa Mkataba na Tanganyika ni hamu yao ya kutaka kuiendeleza nchi yao kwani wanatambua kwamba Serikali yao ya Umoja wa Kitaifa lazima iweze kutawala na kuendesha shughuli za nchi bila ya kungojea ridhaa kutoka Tanzania Bara hasa ikiwa Zanzibar itakuwa na sarafu yake yenyewe, mfumo wake wa kuendesha biashara pamoja na mfumo wake wa kodi na ushuru na uhuru wa wa kuwa mahusiano na mataifa ya nje.Pia iwe na uwezo wa kutumia mali zake asili bila ya kuwa na ubia na taifa lolote la kigeni.(16)
Mbali na kuwa suluhisho mujarab kwa matatizo yanayoukumba Muungano wa Tanzania, umbo hilo jipya la Muungano wa Mkataba litahakikisha kuwako kwa Muungano endelevu utaokuwa na uwazi na utaotoa haki sawa kwa nchi zote zitazojiunga nao na utazipa nchi za Tanganyika na Zanzibar mamlaka kamili ya kila nchi kujiamulia mustakbali wake bila ya kuomba ridhaa ya nchi mwenzake(17)
Tuombe tu kwamba Tume ya Mabadiliko ya Katiba baada ya kuyakusanya na kuyaratibu maoni ya wananchi itakuwa na hadhari itapotoa mapendekezo yake kwenye ripoti yake ya mwisho kwani suala hili ni nyeti.
Uchambuzi wangu: Chanzo cha taarifa hii ni makala katika gazeti la Raia mwema wiki hii.
Ili wasomaji waweze kuelewa hoja zangu vema nimeziwekea namba kwa minajili ya kuzjibu bila kupoteza maana. Ahmed Rajab amenishangaza na jinsi anavyobadili misimamo kila uchao 'change his position' kuhusu suala hili.
Ukisoma namba (1) anasema Tanganyika ni ndugu halafu anawaita nchi ya kigeni (16). Namba (2) anasema tume itakusanya maoni ya wznz kikamilifu hata kama tume hiyo inakusanya pia kutoka Tanganyika. Hapa anaonyesha kuwa wanaolilia hatima ya muungano ni ZNZ na siyo Tanganyika. Kwa mantiki hiyo wangeweza kufanya kura ya maoni wao kuamua hatima yao bila kusubiri tume.
Namba(3)na (8) anasema maamuzi kuhusu muundo wa muungano. Hapa anaikana hoja yake ya siku nyingi ya kutaka ZNZ ijitenge ili iwe kama Malyasia au Mauritius kama alivyowahi kuandika. Sasa anakiri kuwa WZN wanahitaji muungano. Wale wanaomfuata wamebaki njia panda kama alivyowaacha katika suala la serikali 3.
Namba (4) anashadidia hoja kuwa WZNZ wanataka muungano. Anamkana hata Maalim anayetaka ZNZ ijitenge. Tena anarudia hoja ya mkataba
Namba(6) anawatukana Watanganyika kuwa hawaelewi maana ya mkataba. Kwamba Watanganyika ni sawa na WZN wanaomwitikia hata pale anapoandika upuuzi. Kama anadhani hatuelewi mktaba angalia hoja zake zote ametaja mkataba bila kutuambia ni wa kitu gani(11). Huyu msomi wa ZNZ anataka tukubaliane na mawazo yake hata kama yana mapungufu, hayafai au ni ya elimu ya chini sana.
Namba (7)anasema muungano hauna manufaa ZNZ wakati huo huo anataka muungano (3)(4)(8)
Namba (9) anasema nchi zitaunganishwa kwa mkataba. Hajasema wa mambo gani. Namba (10)Anasema utaratibu wa ushirikiano wa nchi mbili zilzio sawa. Kwasahivi hakuna usawa kwasababu nchi moja inajiona mshiriki mkuu(12) Hasemi kuwa ushiriki mkuu unatokana na ukweli kuwa Tanganyika inatoa 100% na ZNZ 0%. wakati huo huo anataka kuwe na usawa(12) kwamba mmoja atoe sana na mwingine apokee huo ndio usawa anaouongelea.
Namba (11) anataja mkataba na ushiriki wa mambo, asichojaribu kukiandika ni kuwa mkataba wa ushiriki wa mambo gani. Hilo hajaweza kulisema wakati huo huo anatukana Watanganyika kuwa hawajui mkataba maana yake nini. Laiti angelijua maana ya mkataba asingekuwa anahangaika kila siku kuandika kitu asichokijua
Namba(13)anatolea mfano mzuri wa EU. Huyu mwandishi ni waajabu sana, alianza na kuvunja muungano ZNZ iwe kama Malaysia, akabadili kuwa na serikali 3, akaja mkataba sasa anatupeleka EU. Maana ya kuwa na EU ni ili WZN wafaidike na rasilimali za Tanganyika bila Watanganyika kufaidi rasilimali zao kama alivyoonyesha namba(16)(17)
Namba (14)Anashauri tuwe na muungano kama wa Senegambia wakati huo huo anasema ule ulishindwa (15). Ahmed anataka tuige uchafu ili mradi tu tuwe na mkataba anaotaka yeye. Anaandika jambo na kulikanausha hapo hapo, ushahidi wa kiwango dhaifu sana cha uandishi.
Namba(16)kama hataki ZNZ iingiliwe katika mambo yake basi ashauri muungano uvunjwe. Kwanini anatapa tapa na serikali 3, mkataba au mfumo wa EU. Kitendo cha kuwa na mkataba tayari ZNZ inapoteza uhuru sasa sijui anataka mamlaka kamili yapi. Mwandishi Ahmed anajichanganya na sina uhakika anajua anaandika nini.
Namba(17)Huko nyuma amesema mkataba utakuwa na kura ya turufu, hapa anasema kila nchi itakuwa na uhuru bila kuomba ridhaa ya nchi nyingine. Too low Ahmed
Watanganyika, hapa tulipo hatuna sababu ya kuwa na ushirikiano na ZNZ kwasababu ZNZ haina kitu cha maana cha kutoa. Wao wanataka kuwe na ushirikiano kama wa EU ili waendelee kuinyonya Tanganyika.
Ukweli ni kuwa yale madai kuwa Tanganyika inaizuia ZNZ sasa ni wazi ni uongo uliotukuka. Zanzibar haina ujanja inataka muungano kwa hiari au kwa lazima. Hizi habari za serikali 3, mkataba wa EU, wa Uswiss ni kutapa tapa kwa kutambua kuwa nje ya muungano atakayepigika na kuumia ni ZNZ.
Ahmed Rajab aache kututukana kuwa hatujui mkataba, yeye ndiye hajui kwasababu hajataja jambo hata moja. Ukweli ni kuwa anataka ushirikiano ili Tanganyika itoe rasilimali zake kama alivyosema katika ulinzi na usalama ambapo ZNZ haina bajeti, elimu ya juu ZNZ haina bajeti, soko la ajira ambalo ZNZ haina, soko la Biashara ambalo ZNZ haina, Ardhi ambayo ZNZ haina n.k. Hicho ndicho anataka katika hoja ya mkataba.
Tayari tuna EAC, SADC na UA, tukutane huko kama nchi huru. Upuuzi wa kusema eti tutawavutia wengine ni umahaluni wa hali ya juu. Tuwavutie kwanini wakati tayari tuna ushirikiano. Hatunatutakachopata kwa ushirikiano wowote ule, sisi tutakuwa losers na hapa ni wakati tuwaambie kuwa Wanatuhitaji na wafunge midomo, kinyume chake LET ZNZ GO!

Reply With Quote

Follow Us Here