| Saturday, 25 February 2012 18:05 |
Na. L. W. Nzela
KWA mara nyingine raia wasio na silaha wameuawa mikononi mwa Polisi na kwa mara nyingine ni wao wanalaumiwa kwa vifo vyao.
Kwa mara nyingine jeshi hili chini ya Said Mwema, limeendelea kuona uhai wa Watanzania kuwa ni kitu cha kuzima kama utani bila ya kuwajibishwa yeyote.
Kwa mara nyingine makala hii itaonekana ni ya kupandikiza chuki kwa sababu inanyoshea kidole moja kwa moja Jeshi la Polisi kuwa kwa ujumla wake limepoteza weledi wake, halijali haki za raia wala haki za binadamu. Lina maofisa ambao vidole vyao vinawashwa kuua!
Yaliyotokea Songea siku ya Jumatano hayawezi kutetewa kwa namna yoyote ile. Kwamba, wananchi wanaoandamana kupinga mauaji ya wananchi katika mazingira ya kishirikina wao wenyewe wanauawa ni kashfa ndani ya kashfa.
Naweza kusema pasi ya shaka kuwa watu wengi wanaouawa kwa kutumia silaha za moto (bunduki) nchini, wanakufa kwenye mikono ya polisi au vyombo vya usalama.
Ni mara chache sana kuwaona raia wanauana kwa kutumia bunduki. Hii ni kinyume na nchi kama Afrika ya Kusini, Honduras, Jamaica au hata Marekani ambapo mauaji ya silaha za moto, hutokea mikononi mwa raia wenyewe.
Tatizo ni fikra za kikoloni
Napendekeza kwamba, mojawapo ya makosa makubwa ya nchi yetu ni kupokea Jeshi la Polisi lililoundwa kulinda utawala wa kikoloni na kulifanya kuwa jeshi la polisi la kuwalinda wananchi.
Jeshi la Polisi la mkoloni lilikuwa na jukumu la kuhakikisha wakoloni wanaishi katika hali ya utulivu na amani na raia wao nchini hawabughudhiwi na wenyeji. Wananchi wetu walikuwa wakiliogopa jeshi hilo kwani halikuwa la kwao na halikuwa rafiki kwao.
Profesa Issa Shivji akiandika katika kazi yake mojawapo ya A Study of Police Powers and Political Expression (REDETt, 2001) anasema kwa Kiingereza kuwa, “The police force in Tanzania is the creation of the colonial period, particularly of the British”. Yaani “Jeshi la Polisi la Tanzania limetoana na enzi za wakoloni, hususan Waingereza”.
Akielezea sifa za jeshi la mkoloni Shivji anasema kuwa lilikuwa na sifa zifuatazo
• Linawajibika kwa mtawala;
• Limepangwa kwa vyeo;
• Lenye silaha na la kiuanamgambo;
• Likiwa limejitenga na jumuiya likiwa na lengo la uwatia hofu wananchi wahofie wenye mamlaka.
Akielezea historia fupi ya jeshi letu hili kutoka katika fikra za wakoloni Shivji anatudokeza kuwa ni mwaka 1950 kikosi cha polisi cha magari kiliundwa ambacho ndio mwanzo wa ‘Field Force Unit’ (FFU). Anasema (kumbuka ni miaka kumi iliyopita akiandika haya); “Hadi leo hii FFU inaendelea kuweka hofu ndani ya wananchi na inajulikana kwa ukatili wake kama ambavyo tumeshuhudia mara kwa mara kwenye TV”.
Ni kikosi hiki ndicho kilichoenda kuzima mgomo wa makuli mwaka 1950 ambapo watu wawili waliuawa, tuhuma zikiwa ni zile zile ambazo tumezisikia Songea – kukusanyika pasipo kibali.
Ni kikosi hiki hiki kilichotumika kuzima mgomo wa kiwanda cha Kilombero mwaka 1986 ambapo raia 4 waliuawa. Kwa ufupi tulichonacho leo hii ni mazao ya ukoloni na hatujaweza kubadilisha.
Ni jeshi la polisi la kisiasa
Sijapata muda wa kusoma matokeo ya utafiti wake wote (Shivji) kuhusu hali ya jeshi letu la Polisi kwa msingi wa kazi yake hiyo hapo juu. Lakini matukio mbalimbali ambayo yametokea kuanzia 1995 hadi sasa yamenifanya niamini kuwa jeshi letu halijawa chini ya raia kama inavyopaswa na limekuwa ni jeshi la kisiasa. Lina malengo ya kulinda na kuwanufaisha wanasiasa walioko madarakani na linadharau ya moja kwa moja dhidi ya wananchi. Bado linajiona ni jeshi la watawala na siyo wananchi.
Hii ni hatari katika mazingira ya demokrasia. Wananchi wanapojitokea – kwa haki waliyonayo kama chanzo cha utawala – na kusema tunaandamana kupinga au kuunga mkono jambo fulani mwitikio wa kwanza wa polisi haupaswi kuwa - wataifanya CCM ionekane vibaya!
Mwitikio wao ulipaswa kuwa hivi; “Tufanye nini ili wananchi waweze kuelezea hisia zao za kisiasa katika mazingira ya amani na utulivu – hata kama yatakuwa na maneno makali ya kisiasa?” Bahati mbaya jeshi hili chini ya IGP Mwema limepoteza uwezo huo.
Kuliunda upya
Binafsi ninaamini hakuna namna ya kulibadilisha jeshi letu isipokuwa kwa kuliunda upya ikiwa ni pamoja na maafisa wote kupewa mafunzo ya kuelewa haki za raia na haki za binadamu. Haitoshi kutoa mafunzo ya juu juu tu kuna tatizo la msingi katika jeshi hili na ipo haja ya baadhi ya maafisa kuondolewa warudi uraiani.
Tatizo hili la msingi litaendelea kutusumbua kwa muda mrefu. Watanzania waliochoshwa na vitendo vya ukatili na ukiukaji mkubwa wa haki za raia na za binadamu unaofanywa na baadhi ya polisi, wanalo jukumu la kutafuta chama kingine ambacho kitaweka wazi lengo na sera ya kulivunja jeshi hili.
Tusipofanya hivyo, tutaendelea kufa mikononi mwa polisi kama mbu anavyokufa mikononi mwa mtu. Jeshi hili hili ambalo linalindwa na kutetewa na wanasiasa hawa hawa litaendelea kupiga risasi watu mgongoni huku viongozi wake wakitumia mistari ile ile tuliyoisikia miaka hamsini iliyopita! Na kama hatutaonesha hasira ya kutosha na kutaka kina Mwema wawajibike tutaendelea kukodolea televisheni zetu kila baada ya miezi michache tukishuhudia watu wakipopolewa kwa risasi kama swala msituni.
Ndugu zangu, Jeshi la Polisi linatakiwa kuwa ni mlinzi wa wananchi na rafiki wa jumuiya. Lakini historia inavyojirudia mara kwa mara inatuonesha kuwa ni jeshi lenyewe ndilo limetengeneza uadui wa kudumu na wananchi wake.
Kuanzia Mererani, Nyamongo, Mwembe Chai, Pemba, Tanga, Mwanza, Mbeya n.k, jeshi hili limekuwa likiwashambulia wananchi bila kukemewa.
Si Rais wala Waziri Mkuu ambaye amewahi kuonesha kuguswa na hili; si Spika wa Bunge wala wabunge wa CCM wamewahi kuzungumzia hili. Lakini tunashuhudia hoja za ajabu ajabu zinaletwa bungeni kwa mbwembwe, isipokuwa hoja ya kukemea ukatili wa Polisi!
Mpaka auawe nani ndio tutakasirika?
Niandikie: [email protected]
|
Follow Us Here