TANZANIA sasa imekuwa nchi ya misiba na tunadiriki kusema kwamba mara nyingi misiba hiyo imekuwa ya kujitakia. Haipiti siku kabla vyombo vya habari havijatangaza habari za vifo vya mamia ya watu vinavyotokana na ajali barabarani katika kila kona ya nchi yetu. Ajali za vyombo vya majini, kama ilivyo kwa vyombo vya safari za anga na reli zimezidi kuongezeka na kujenga dhana miongoni mwa wananchi kuwa, siyo tu ajali zimekuwa sehemu ya utamaduni wetu, bali pia kwamba ajali hizo kamwe haziepukiki.
Tumeshindwa kupata muarobaini wa kupunguza, kama siyo kukomesha ajali hizo zinazopoteza maisha ya Watanzania. Badala ya kufanya uamuzi mgumu wa kuchukua hatua stahiki dhidi ya vyanzo vya ajali hizo na kusimamia sheria za usafirishaji kwa kuhakikisha sheria hizo zinauma kila upande pasipo woga wala upendeleo, viongozi wetu wamebaki kuwa vinara wa kutoa rambirambi kwa wafiwa. Tunathubutu kusema kwamba vifo vingi vinavyotokana na ajali hizo vimetokea kwa sababu Serikali imeshindwa kutimiza wajibu wake.
Juzi mchana utamaduni huo wa ajali ulijirudia baada ya miili ya abiria wapatao 50 kuopolewa wakiwa wamefariki dunia na wengine 137 kuokolewa wakiwa majeruhi baada ya meli ya Skagit iliyokuwa imebeba abiria kutoka Dar es Salaam kwenda Zanzibar kuzama karibu na Kisiwa cha Chumbe, kilomita 19 kutoka Bandari ya Malindi, mjini Zanzibar. Hata hivyo, kumekuwapo na mkanganyiko kuhusu idadi kamili ya watu waliokuwa katika meli hiyo, kwani jana mamlaka husika zilikuwa zikitoa kauli zilizokuwa zinatofautiana au zinakinzana.
Hii ni ajali ya pili mbaya kutokea visiwani humo katika kipindi cha miezi 10 tu tangu ilipotokea ajali nyingine ya MV Spice Islander Septemba 2011 ambapo watu wapatao 240 walikufa na wengine zaidi ya 1,500 hawajulikani walipo hadi leo baada ya meli hiyo kuzama ikiwa safarini kuelekea Pemba ikitokea Bandari ya Malindi, Unguja na tume iliyoundwa na Rais Mohamed Shein kuchunguza ajali hiyo ilitoa ripoti iliyosema kuwa, meli hiyo ilikuwa imebeba mizigo na abiria kuliko uwezo wake.
Hata hivyo, siyo mara ya kwanza kwa meli hiyo iliyozama juzi kukumbwa na misukosuko ikiwa imebeba abiria baharini. Mei mwaka huu, abiria wapatao 300 walinusurika kufa baada ya meli hiyo kushika moto katika eneo la Nungwi ulioanzia kwenye injini wakati ikielekea Unguja kutoka Pemba. Zipo taarifa kutoka shirika moja la kimataifa kuwa, meli hiyo ilinunuliwa mwaka 2011 kutoka Marekani, lakini wataalamu walionya mwaka 2006 kwamba meli hiyo ilikuwa haifai tena kubeba abiria.
Jambo moja linalojitokeza hapa ni kwamba meli zinazosafirisha abiria katika maziwa na bahari zetu siyo salama na hazifai tena kwa sababu zimechakaa, hivyo kustahili tu kuuzwa kama vyuma chakavu. Inashangaza kuona serikali zetu katika pande zote mbili za Muungano hazithamini maisha na ustawi wa watu wake na hazioni umuhimu wa kununua meli zilizo salama kwa ajili ya usafiri wa wananchi.
Hili linathibitishwa na ukweli kwamba MV Liemba iliyozama katika Ziwa Tanganyika miaka michache baada ya Uhuru halijapata meli nyingine hadi leo. Kama hiyo haitoshi, MV Bukoba iliyozama katika Ziwa Victoria mwaka 1996 na kuua watu 1,000 haijapata mbadala wake hadi leo, huku MV Victoria iliyoanza kutumika katika ziwa hilo tangu miaka ya 60 ikisubiriwa kuzama na kuua maelfu ya abiria wakati wowote kutokana na kuzeeka kupita kiasi. Ni jambo la ajabu kwamba Ziwa Nyasa limekosa meli kwa miongo mingi sasa na kuacha wananchi wakiweka maisha yao rehani kwa kutumia usafiri usio salama.
Tunazishauri serikali zote mbili zitambue kwamba majuto ni mjukuu, kwa maana ya kuhakikisha kwamba vyombo vya usafiri vinakuwa salama badala ya kusubiri kutokea kwa ajali na kuwa wepesi wa kutoa rambirambi na hata kuamuru bendera zote nchini zipeperushwe nusu mlingoti.


Reply With Quote

Follow Us Here