Leo Mwigulu Mchemba ameomba mwongozo kuhusu ushahidi wa John Mnyika alioufikisha kwenye ofisi za Bunge.
Cha msingi hapa ni kwamba Job Ndugai ameeleza kuwa wabunge waache tabia ya uongo na kujiamini kwamba wana ushahidi. Ndugai ameeleza kwamba wote ambao waliwahi kufikisha ushahidi kwa Spika Hakuna hata mmoja aliyeleta ushahidi unaokidhi vigezo vya ushahidi.
Kuhusu ushahidi alioleta Mnyika, Ndugai kasema kwamba Mnyika ameleta maelezo ya utangulizi na wala si ushahidi halisi. Hivyo, kwa suala hili la Mnyika ameamua kulifikisha kwenye Kamati ya Maadili ya Bunge na huko Mnyika ataandikiwa barua kama hatua ya kwanza.
Binafsi hapa sina matatizo na uamuzi wa Job Ndugai, uamuzi wa kiti cha Spika. Sitetei uhalisi wa ushahidi aliowasilisha John Mnyika.
Hoja yangu ni jinsi Ofisi ya Spika inavyoshughulikia masuala haya.
Tangu Bunge hili la 10 limeanza chini ya Anne Makinda kama Spika, sikumbuki ni idadi gani ya wabunge hasa wa CHADEMA wameombwa kuleta ushahidi na wakaleta. Kwa kutaja ninaojua ni Godbless Lemma, Zitto Kabwe, Ezekah Wenje nk.
Lakini leo ni miezi 17 imepita tangu mtu wa kwanza kuambiwa alete ushahidi na haukushughulikiwa. Ushahidi huo ni ule wa Godbless Lemma ambaye sasa hauhitajiki kwa sababu mbunge hoja yake inakufa anapokoma kuwa mbunge na hivyo suala la Lemma limefungwa hivyo.
Lakini bado kuna ushahidi mwingi wa wengine una zaidi ya mwaka hatuoni kasi yoyote ya kushughulikia.
Sasa umekuja ushahidi wa John Mnyika. Haujamaliza hata siku mbili Kiti cha Spika kimetoa maamuzi kwamba upelekwe Kamati ya Maadili na haki ili Mnyika aanze kuwajibika kwa kuandikiwa barua. Narudia simetetei Mnyika na inawezekana kabisa ushahidi wake ni hafifu na ikibidi ni wa uongo.
Taaabu yangu ni kwamba kiti cha Spika kimeonyesha double standards ambazo watazania wote tunaendelea kuangalia kana kwamba tunaangalia ngumi za jogoo wawili wakipigana na kama vile sisi haituhusu.
Iwapo John Mnyika ataandikiwa barua, bais huo ni ushahidi tosha kwamba Spika amefanya amevunja katiba. Je, Spika kavunja katiba kwa namna gani?
Ibara ya 9(h) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inasema hivi: { Kwa hiyo, Mamlaka ya Nchi na vyombo vyake vyote vinawajibika kuelekeza sera na shughuli zake zote katika lengo la kuhakikisha kwamba aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, rushwa, uonevu au upendeleo zinaondolewa nchini }.
Ibara ya 13(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inasema hivi: {Watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki, bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria}.
Wakati humohumo katibani Ibara ya 13(2) inasema hivi: {Ni marufuku kwa sheria yoyote iliyotungwa na mamlaka yoyote katika Jamhuri ya Muungano kuweka sharti lolote ambalo ni la ubaguzi ama wa dhahiri au kwa taathira yake}.
Kama yapo mengine yanayotaja neno ubaguzi au upendeleo basi mtaonyesha lakini kwa hoja yangu hapa inanitosha. Sasa ubaguzi unaokatazwa na katiba unaigusaje issue hii ya ushahidi wa John Mnyika?
Ubaguzi ni kwamba Ofisi ya Spika wa bunge lilelile ameonyesha sura mbili kwa suala lilelile yaani kushughulikia ushahidi. Ni kweli kuwa kanuni hazitaji ni lini na kwa haraka gani Spika anatakiwa kushughulikia masuala haya ya kuuanika ushahidi au kuushughulikia.
Lakini hapa tumeona kuwa suala la ushahidi wa John Mnyika Spika hakusubiri hata masaa 48 yapite.
Hivyo, hii ni nafasi ya kulichukulia jambo hili kuwa ni la katiba. Kuna watu watakuja na hoja kwamba Bunge lina kinga. Hawa ni wale ambao hawajui maana ya kinga na hawajsoma utaratibu wa kinga au sheria ya kinga.
Hakuna mtu hapa nchini aliye juu ya katiba. Hakuna taasisi iliyo juu ya Katiba, siyo Ikulu au Ofisi ya Bunge, siyo Rais wan chi siyo Spika au Naibu Spika. Kinga ya bunge ni kinga kwa ajili ya kuendesha majadiliano maadamu majadiliano hayo hayavunji haki ya mtu yeyote duniani.
Bunge, mbunge, Spika, Naibu Spika wote hao waliapa kulinda katiba na si kuvunja hata kipengele kimoja.
Je, uvunjaji wa Katiba ni uhalifu wa aina gani? Kwa kiingereza wapo wanaouita “treason”. SIna hakika kama “Uhaini” ndilo neno sahihi kwa dhambi ya uvunjaji wa katiba.
Kuvunja katiba si lazima uvunje vipengele vyote. Na mara nyingi si rahisi kuvunja katiba yote maana hiyo sasa itakuwa si uvunjaji wa katiba bali hayo ni “Mapinduzi” kama mapinduzi yoyote duniani.
Kuvunjwa katiba ni pale kinapovunjwa kipengele kimoja au kadhaa vya katiba.
Kwa hoja hii ya John Mnyika, vipengele vyote vinavyozuia ubaguzi ndani ya Jamhuri yetu vimevunjwa. Hii sasa ni kesi ya kikatiba. Mahala pake ni mahakamani. John Mnyika akipata barua basi huo ndiyo mwanzo wa kulipeleka suala hilo Mahakamani.
Ninaweza kutaja mifani mingi ya mambo ya mabunge ya Commonwealth kufikishwa mahakamani lakini hata hapa Augustine Mrema alishawahi kupinga adhabu yake bungeni kwa kwenda mahakamani. Japo Mrema alishindwa kwenye kesi ile iliyoendeshwa na Jaji Katiti lakini Mahakama haikuzuia case ile eti tu kwa sababu ni jambo limetokea bungeni.
Hata msingi wa kesi ya Mrema ilijikita kwenye misingi ya Katiba kwamba pamoja na kutoridhika na adhabu ya kufungiwa ile adhabu ilikuwa inamnyima haki yake ya kikatiba kushiriki vikao vya Bunge. Pendekezo ambalo lilikataliwa na Jaji Katiti kwamba kuhudhuria vikao vya Bunge si haki ya kikatiba.
Hivyo, watanzania tuamke tulitizame jambo hili kwa muono huo na si kulalamika kama tumeishiwa hoja. Tunajadili katiba mpya na hivyo kesi kama hizi ni kipimo kwetu kuona kama kweli tunaelewa tunalojadili au la.
Hatuwezi kuendelea kuona Spika akivunja katiba kwa kutoa upendeleo na ubaguzi ambao umekatanzwa na vifungu tele vya katiba yetu. Sasa tujikite wote tulitizame kuwa ni jambo la katiba.
Wabunge wa CHADEMA watumie nafasi yao kulipeleka hili suala Mahakamani maana nis suala la kuvunjwa kwa katiba. Ushahidi upo mwingi tu kuonyesha Bunge ni taasisi inayoendekeza ubaguzi. Ukianzia na suala la Tundu Lissu ambapo Spika alilidanganya Bunge kuwa Tundu Lissu ni mshtakiwa wa mauaji. Kuna suala la kufikishwa kwa ushahidi wa Zitto Kabwe. Kuna suala la ushahidi kuhusu uongo wa Waziri Mkuu kuhusu mauaji ya Arusha hadi Lemma amepoteza ubunge.
CHADEMA wakienda mahakamani tutakuwa tumenyoosha adabu kwamba katiba si ya kuchezewachezewa kwa dhana ya kwamba kuna chama kina wabunge wengi na kinaweza kujivunia hilo kwa kudhani kiko juu ya katiba kwa sababu Rais, Spika, Naibu Spika wanatoka chama hicho.
Ninaamini wanasheria mliomo humu JF na kokote mnalijua hili kunizidi.
CHADEMA mkishindwa hapa basi inabidi watu tufungue macho na kuwakamia nyinyi wala si Anne Makinda au Job Ndugai. Mara nyingi mmekuwa mkitutangazia magazetini kuhusu upendeleo wa Spika na mnamuacha hivyohivyo wakati uwezo uko mikononi mwenu.
Mwaka jana Tundu Lissu alitutangazia kuwa amempeleka Spika Anne Makinda kwenye Kamati ya Kanuni za Bunge baada ya kuzuia swali lake kwa kisingizio kwamba ana kesi Mahakamani wakati Tundu Lissu hakuwa na kesi ya mauaji ya Tarime. Tukasubiri kwa hamu matokeo ya kesi ile maana tulijua hapa ndipo Spika Anne Makinda angekiona cha moto maana ushahidi wa hili ilikuwa wazi na asingekwepa kibano kile.
Lakini kwa mshangao wa watu kama mimi hadi leo hakuna lolote kuhusu suala lile kana kwamba Kamati ya Kanuni za Bunge haikumjadili Spika Makinda kwa kumpendelea Waziri Mkuu na kumzuia Tundu Lissu kujibu swali.
Hivyo ndivyo ninaona dawa inaweza kupatikana kwa masuala haya kwani tumechoshwa na marudio ya haya mambo.

Reply With Quote




Follow Us Here