Ujue ukweli wa kiapo cha mbunge, waziri
MWEZI uliopita ulizuka ubishi magazetini na kwenye vyombo mbalimbali vya mawasiliano ukihoji mantiki ya mbunge kuapa na kuanza uwaziri kabla hajaapa ubunge. Sina hakika kama ubishi ule sasa utahamia bungeni kujadili viapo vile.
Naanza kufafanua ninavyoelewa kwa kueleza historia ya ubunge.
Mfumo wa sasa wa Bunge uliundwa na kusimikwa na Simon De Montfort, tajiri aliyeitawala Uingereza kimabavu kwa muda.
Kabla yake, wafalme wa nchi hiyo walizoea kuwaita kwa msimu matajiri wa kwenye jamii (Lords) ili kusikia taarifa na ushauri wao.
De Montfort alipochukua madaraka, alibadili mtindo huo. Januari 20, 1265 aliwaita matajiri (Lords) lakini pia akaamua kila eneo lichague watakaokuja kuwawakilisha masikini (Commons).
De Montfort alifanya hivyo ili apendwe kuepusha chuki dhidi ya kitendo chake cha kumuondoa madarakani mfalme halali yaani Henry III.
Mfumo aliousimika De Montfort, japo ulirikebishwa kidogo, umedumu hadi leo. Ni mfumo wa Bunge kuwa na mikusanyiko miwili. Mkusanyiko wa kwanza umeendelea kujumuisha wanaoteuliwa na mfalme au malkia, ukijulikana kama “Upper House”.
Mkusanyiko wa pili ni wa watu waliochaguliwa na wananchi. Mkusanyiko huu huitwa “Lower House”.
“Lower House” inajulikana kwa majina kadhaa kama vile House of Commons (Uingereza), Bundestag (Ujerumani), House of Representatives (Marekani).
Wakati “Upper House” ina majina yafuatayo: House of Lords (Uingereza), Bundesrat (Ujerumani) na Senate (Marekani).
Mikusanyiko yote miwili kwa pamoja ndiyo huitwa Bunge (Parliament). Mtindo huu wa Bunge kuwa na mikusanyiko miwili huitwa “Bicameral”. Wakati mataifa yenye Bunge lenye mkusanyiko mmoja huitwa “Unicameral”.
Je, sisi tuna mabunge mawili (Bicameral) au moja (Unicameral)? Ni rahisi kujibu kuwa tuna Bunge la mkusanyiko mmoja tu, yaani ule wa kina John Mnyika, Anne Makinda na wenzao (National Assembly).
Lakini katiba haisemi hivyo. Katiba inasema kwamba yenyewe haikutungwa na Bunge kama hili, bali imetungwa bunge jingine tunaloliita “Bunge Maalumu,” au (Constituency Assembly).
Hivyo, katiba imetaja mabunge mawili, yaani “Bunge Maalum” (Constituency Assembly) na Bunge la Jamhuri (National Assembly).
Wanaosita kutamka kwamba tuna mabunge mawili (Bicameral), inabidi wasaidie kufafanua sababu zao kwani binafsi sioni ibara ya Katiba inayoonyesha kuwa lile “Bunge Maalumu” limefutwa.
Haitofautiani na kudhani kwamba Tanzania haina Mahakama Maalumu ya Katiba kwa sababu hatujawahi kuiona ikifanya kazi, wakati imetajwa kwenye ibara ya 125 hadi 128 ya Katiba.
Ni vizuri kueleza matukio yaliyotokea England Machi 2, 1629 na Januari 5, 1642 wakati wa utawala wa Mfalme Charles I wa England.
Machi 2, 1629, Charles I alinuia kuvunja bunge kwa sababu alishachoshwa na ubishi wabunge kubishia matakwa yake hasa matumizi ya pesa. Mtumishi wa mfalme ambaye hadi sasa anaitwa “Black Rod” akatumwa kuwafikishia wabunge taarifa hiyo.
Wabunge wa kikundi cha John Eliot walijua mtumishi sasa anakuja kuwaita ili bunge livunjwe. Wakajua Spika kwa woga wake akitoka kitini basi maamuzi yao yatakuwa batili yaani hakuna Bunge.
Hivyo, wabunge wakagawana majukumu. Wengine wakaenda kuubamiza mlango mbele ya yule mtumishi ili asiingie, na wengine wakakimbia hadi kwa Spika wakamshika kwa nguvu asiinuke kitini.
Mlango ukiwa umefungwa na Spika akiwa amebanwa pale kitini wenzao wakatumia mwanya huo kupitisha maazimio matatu waliyoyataka, kisha wakamwachia Spika wakatawanyika.
Januari 5, 1642 hali ikuwa ni tofauti, kwani Charles I hakutaka kuishia kumtuma mtumishi, bali pia aliamua sasa aingie kwa nguvu bungeni kuwakamata wabunge watano ambao ni vinara wa ubishi hasa John Pym.
Mtumishi wake alipofika mlangoni wabunge wakaubamiza lakini askari wa mfalme wakagonga na kuingia kwa nguvu. Charles I hakufanikiwa kuwakamata John Pym na wenzake kwani walishatoroka.
Kitendo cha Charles I kuvamia bungeni na kuvunja uhuru wa Bunge kilisababisha Waingereza wapigane vita vya wenyewe kwa wenyewe yaani askari wa Bunge na wa Mfalme.
Lakini kiliifanya hiyo Januari 5, 1642 iwe ndiyo siku ya mwisho kwa mfalme au malkia wa Uingereza kukanyaga kwenye mkusanyiko wa House of Commons. Hotuba za uzinduzi wa Bunge za malkia au mfalme huzitoa akiwa House of Lords.
Kitendo cha kuubamiza mlango hurudiwa hadi leo kila mara wabunge wanapoitwa kumsikiliza Mfalme au Malkia kule House of Lords. Waweza kukishuhudia kikifanywa mbele ya malkia Elizabeth II mwaka 2008 kwenye tovuti hii (www.youtube.com/watch?v=h1bJ8nY2pcc).
Kwanini kitendo cha kuubamiza mlango mbele ya mtumishi wa mfalme kinaadhimishwa kwa miaka 383 sasa.
Maana yake ni kwamba Bunge liko juu ya kila mtu hata kwa mkuu wa nchi yaani Mfalme au Malkia.
Hivyo, ni kazi ya Mkuu wa nchi kuwabembeleza wabunge kufungua mlango tena mara tatu ndipo awaombe kwa heshima na taadhima kuja kujiunga na wenzao kumsikiliza.
Hapa nchini, yapo mengi yanayohitajika ili mkusanyiko uwe ni kikao halali cha bunge. Ibara ya 146(2) ya Kanuni za Bunge inamtaka Spika avae joho lenye bendera ya Taifa akiwa kwenye shughuli za Bunge.
“Siwa” ni lile rungu linalobebwa na askari anayeongoza msafara wa Spika kuingia Bungeni. Hii “Siwa” ni ishara ya mamlaka ya Bunge.
“Siwa” isipokuwepo, basi mamlaka ya Bunge yanakosekana kwenye mkusanyiko uliokuwapo. Vikao vya kamati za Bunge hufanywa bila “Siwa”. Hivyo Kamati hizo si shughuli ya Bunge.
Nimerudia maneno “Shughuli za Bunge” hivyo nalazimika kuyafafanua. Ibara ya 89(2) ya Katiba inasema “Shughuli za Bunge” ni zile za ndani ya Bunge tu, na wala si za kamati, si za kamati ndogo wala si zile za Ofisi ya Bunge.
Maneno haya “Shughuli za Bunge” yanajirudia tena kwenye Ibara ya 68 inayomtaka mbunge kuapa kabla ya kuanza kushiriki “Shughuli za Bunge”.
Kwa mamlaka ya ibara ya 46A ya Katiba, Bunge lina uwezo wa kumshitaki Rais aliyeko madarakani. Utaratibu wa kumshtaki Rais unamtaka Spika kuunda Kamati Maalumu ya Uchunguzi wa Mashtaka dhidi ya Rais (Ib. 46A(4)). Mwenyekiti wa Kamati hii ni Jaji Mkuu wa Tanzania, na mjumbe mmoja ni Jaji Mkuu wa Zanzibar.
Kitendo cha Kamati ya Bunge kuongozwa na Jaji Mkuu, ni mfano mzuri kuonyesha kwamba Kamati si “Shughuli ya Bunge” na inaweza kuhudhuriwa na hata kuongozwa na asiye mbunge.
Sasa tujadili aina mbili za viapo yaani Kiapo cha Uaminifu na Kiapo cha Ofisi. Viongozi wakuu wa mihimili ile mitatu Bunge, Serikali na Mahakama huapa viapo vyote viwili wanapokabidhiwa zao. Inaelekea kwamba kile kinachoitwa Kiapo cha ofisi katiba haikitamki kama Kiapo cha ofisi. Badala yake yapo maneno mengi yasemayo (Kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi yake).
Wingi wa maneno haya umewachanganya hata wataalam hadi kusema labda hicho ’Kiapo kingine’ ndicho kile mawaziri wanachotakiwa kuapa siku wanayoingia Bungeni. Kwa kudhani hivyo hisia zilionekana zikihoji kwamba inawezekana ilikuwa ni makosa kuwaapisha wabunge kuwa mawaziri kabla ya hicho kiapo kingine.
Je, mtu anakuwa mbunge siku anapotangazwa au siku anapoapa? Mbunge akishatangazwa tayari ni mbunge, maana hakuna wa kutugeuza tusimpende.
Lakini, sheria yaani katiba inamfanya kuapa kwake bungeni kumpatie uhalali wa kushiriki “Shughuli za Bunge”.
Je, kwani lazima mbunge aende bungeni Dodoma? Mbona anaweza kubaki jimboni akawa anachimba visima au akanunua magari ya zahanati au akajenga shule kwa wanajimbo wake?
Tumeona kwamba shughuli inayofanyika bila lile rungu la Spika, si “Shughuli ya Bunge”. Kitendo cha mbunge kununua gari la zahanati au kusomesha yatima ni uhisani kama uhisani wowote. Si “Shughuli ya Bunge” kikatiba wala kihistoria duniani.
Mbunge akiendelea na huo uhisani wake, tena hata akadiriki kuigharimikia bajeti ya nchi nzima lakini asikanyage bungeni kwa mikutano mitatu mfululizo, basi atapoteza ubunge wake kwa uzembe yaani utoro kama walivyodai Zitto alipoanza kutosaini fomu za mahudurio bungeni.
Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Jaji Mkuu, Spika, Mbunge wote hawa wanaapa kiapo cha uaminifu kwa sababu wanautumikia umma kwa nyadhifa walizokabidhiwa.
Kwa nini mtu akiteuliwa kuwa Waziri anaapa tena kiapo cha uaminifu pale Ikulu wakati alishaapa bungeni?
Bungeni, mbunge anautumikia umma kwenye mhimili mmoja (Legislature). Wizarani, waziri anautumikia umma kwenye mhimili mwingine (Executive). Kule Mahakamani Jaji Mkuu anautumikia umma kwenye mhimili wa tatu (Judiciary).
Hivyo, mawaziri wale walioteuliwa hivi karibuni ubunge na uwaziri ndani ya saa 24 waliapa kiapo cha uaminifu, ili wautumikiea umma kwenye mhimili wa utendaji, yaani ule uwaziri wake.
Hivyo, tuwatarajie kuanzia keshokutwa waape kiapo cha uaminifu, lakini sasa kwenye mhimili wa uwakilishi.
Kwa nini mbunge haapi mara mbili pale bungeni kama Spika? Wala si kama Spika tu. Viongozi wakuu wengi wa ile mihimili mitatu huapa viapo hivi viwili.
Kwa nini sasa mbunge haapi kiapo cha ofisi? Kwani hana ofisi? Katiba imetaja majukumu ya viongozi watano : Rais (Ibara. 33-37), Makamu wa Rais (Ibara. 47-48), Waziri Mkuu (Ibara. 52), Waziri (Ibara. 58), Jaji Mkuu (Ibara. 119)}.
Katika ibara zote hizo 40, hakuna hata moja inayotaja majukumu au madaraka ya Mbunge. Badala yake, ibara ya 63 na 64 imetaja na kufafanua majukumu ya mkusanyiko mzima unaoitwa Bunge.
Kumbe, kila kinachotamkwa au kuulizwa au kuamriwa mle bungeni, kikipita bila kipingamizi basi katiba inatufundisha tutamke kwamba (“...Bunge limesema hivi...”) au (“...Bunge limeazimia hivi...”). Katiba inatufundisha hivyo hata kama mzungumzaji mkuu alikuwa ni mmoja tu kati ya wabunge wote zaidi ya 350.
Kwa maelezo haya mle bungeni panatakiwa uangalifu wa hali ya juu, kwani yanayojadiliwa, yanayoulizwa, yanayoamriwa pale ni ya bunge zima. Kama ni mafanikio yanakuwa ya Bunge zima. Kama ni lawama litupiwe Bunge zima.
Nawatakia heri wabunge wapya watakaoapa siku yoyote kuanzia keshokutwa. Pia nalitakia heri Bunge zima katika mjadala mzima wa bajeti.
*********************
Source: Tanzania Daima
Date: June 10, 2010 (Sunday)
Website: http://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=36836

Reply With Quote




Follow Us Here