Rev. Kishoka
Samahani kwa kukuelewa vivyo sivyo.
Hayo mengine nimekupata, tuendelee kuyajadili kule kwenye "CHADEMA must reform"
Mtanzania wa kawaida anachojua tu ni kwamba waCHADEMA wanapinga ufisadi na kutetea rasilimali za Taifa; wanachojua ni Mbowe wa Helikopta anayekemea rushwa ya CCM kwa kuwaapiza, Zitto Kabwe aliyefukuzwa Bungeni kwa sababu ya Dili la Karamagi la Buzwagi, Dr Slaa ambaye ameshika pabaya Balali kwenye BOT na Tundu Lissu ambaye ameshirikiana na Slaa kutaja orodha ya mafisadi. Hizo ndio stori za vijiweni! Ukiwauliza kuhusu falsafa na itikadi hawayajui mambo hayo, changamoto ni CHADEMA kuweza kueleza zaidi sera zake mpaka watanzania wajue kwamba ni chama cha itikadi ya mrengo wa kati chini ya falsafa ya "Nguvu ya Umma", taratibu tutafika. Hatua ya kwanza ambayo tumeanza nayo ni kutoa mafunzo kwa viongozi wetu ngazi za chini, taratibu tutafika. Safari ya maili mia huanzia na moja!
Elimu ya bure tunayoipata hapa inapenya katika akili zetu na tunaitoa tunapokaa katika vikao vya chama ama vya ushirikiano wa vyama ama tunapoandaa rasimu ya nyaraka mbalimbali za kutoa mwelekeo. Tunaitumia pia tunavyopanda jukwaani kuhutubia wananchi ikiwemo huko vijijini. Kwa hiyo, chukulia kila unachoandika hapa kinasadia katika kujenga demokrasia na maendeleo nchini. Sisi ni watumishi na wawakilishi, vyama vya siasa ni taasisi za umma!
CHADEMA ina kurugenzi mbalimbali ambazo zinawataalamu wa fani mbalimbali, lakini hawa pekee hawawezi kutosha kusambaa maeneo mbalimbali nchini.
Tunahitaji wataalamu mbalimbali, hata kama wanakazi zao huo mawilayani ama kwenye taasisi mbalimbali watenge japo siku moja kwa mwezi huko walipo kujitolea utaalamu wao kwa ajili ya kusaidia mikakati ya kuleta demokrasia na maendeleo nchini. Vinginevyo, usomi wao utakuwa ni wa kibinafsi kama yule aliyechangiwa chakula chote kijijini avuke jangwa akalete chakula kwa waliobaki wenye njaa, huyo asiporudi ni msaliti! Kadhalika, wasomi wetu wakishindwa kuchukua japo muda mchache kukumbuka wajibu wao kwa wasiosoma na taifa kwa ujumla, nao ni wasaliti. Kama tunaweza kukaa kwenye pub masaa kadhaa tukipiga soga, tujue kuwa tunaweza kabisa kuwa na muda kwa ajili ya hii noble course tukitaka.
Wapinzani wanafanya nini kuchukua tuzo za siasa na ujamaa na kujitegemea? Tunafanya. Mimi na Profesa Baregu tulikuwa kwenye kamati ya kufanya mapitio ya itikadi ya CHADEMA kutenganisha bayana itikadi na falsafa ya CHADEMA katika muktadha wa malengo, sera za CHADEMA na mwelekeo wa Taifa kwa ujumla. Hatimaye katiba ikafanyiwa mabadiliko 2006- nimeweka kwenye "CHADEMA must reform" nakala ya Katiba ya CHADEMA- ukisoma 'itikadi ya CHADEMA ya mrengo wa kati" na falsafa ya CHADEMA ya "Nguvu ya umma" utaona kwamba imechota baadhi ya tunu za Ujamaa na kujitegemea ikachanganya na baadhi ya manufaa ya ubepari. Mchanyato uliopatikana utawezesha CHADEMA ikichukua dola- kuendesha nchi bila dola kuhodhi nyanja zote, lakini kuhakikisha pia uchumi unamilikiwa na wananchi waliowengi na si uchumi unaomilikiwa na kunufaisha kwa kiasi kikubwa tabaka la watu wachache ama wawekezaji kutoka nje chini ya ubepari wa kimataifa wa ukoloni mamboleo.
JJ
Follow Us Here