Mbowe aanzisha safari ya 2010 kwa helikopta tena
na Mwandishi Wetu
MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe, leo anaanza awamu ya kwanza ya ziara ya kuzunguka mikoa 10 nchini, akitumia helikopta, kwa malengo ambayo yanaonyesha kuanza maandalizi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
Habari kutoka Mwanza ambako ndiko ziara hiyo inakoanzia zinaeleza kwamba, helikopta ambayo Mbowe ataitumia, iliwasili katika jiji hilo jana jioni ikitokea nchini Kenya.
Kwa mujibu wa habari hizo ambazo zilithibitishwa na Mbowe mwenyewe, ajenda kuu ya ziara hiyo ni kuwashukuru wananchi kwa namna walivyokiunga mkono chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana.
Hata hivyo, alipotakiwa kueleza iwapo ziara yake hiyo ilikuwa ikilenga kuanza kufanya maandalizi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, Mbowe hakuwa tayari kueleza moja kwa moja zaidi ya kusema tu kwamba; “lengo la chama chochote makini ni kuchukua madaraka ya dola.”
Taarifa rasmi kuhusu ziara hiyo iliyotolewa Dar es Salaam jana jioni na kutiwa saini na Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Shaib Akwilombe, ilisema dhumuni la kwanza la ziara hiyo ni kuwashukuru Watanzania waliokipigia kura chama hicho, kwenye uchaguzi wa mwaka jana.
Pamoja na hilo, Akwilombe katika taarifa yake hiyo alisema pia kwamba, atakapokuwa katika ziara hiyo, Mbowe atawashukuru wananchi kwa kufanikisha uchaguzi huo kwa njia ya amani, pamoja na kuwapo kwa mazingira magumu waliyokuwa nayo, ambayo hata hivyo taarifa hiyo haikuyafafanua.
Dhumuni jingine linalotajwa katika taarifa hiyo, ni kuwaandaa wananchi kujenga na kuimarisha chama hicho, kwa lengo la kuimarisha upinzani nchini, kama sehemu ya utekelezaji wa programu ya miaka mitano ya chama hicho yenye ujumbe unaosema ‘Tumaini Jipya’.
Aidha, alisema ziara hiyo ina lengo la kuhamasisha uwajibikaji wa viongozi na wananchi katika ngazi mbalimbali baada ya mwaka mmoja wa Serikali ya Awamu ya Nne, ili kuchochea demokrasia na maendeleo nchini.
Naibu huyo amesema, ziara ya mwenyekiti huyo itaanza leo wilayani Nansio kisiwani Ukerewe mkoani Mwanza, Shirati, Tarime na Musoma mjini, mkoani Mara.
Akiwa katika ziara hiyo ambayo itamchukua siku 10, Mbowe atakwenda pia katika mikoa ya Kagera, Mara, Kigoma, Shinyanga, Arusha, Manyara, Kilimanjaro, Tanga na Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, awamu ya pili ya ziara hiyo ya Mbowe ambaye hivi sasa anasoma masomo ya falsafa, siasa na historia katika Chuo Kikuu cha Hull nchini Uingereza na wakati huo huo akipata mafunzo mengine maalum ya uongozi huko huko Uingereza, itaanza katikati ya Mwezi Aprili mwakani.
Katika uchaguzi mkuu uliopita, Mbowe ambaye aligombea urais kwa mara ya kwanza, alishika nafasi ya tatu, akitanguliwa na Rais Jakaya Kikwete (CCM) na Prof. Ibrahim Lipumba (CUF), na chama chake kilipata viti vitano vya wabunge na kina wabunge sita wa viti maalum.

Reply With Quote


Follow Us Here