Ni jambo la heri kuona kila mmoja anatimiza wajibu na malengo yake ipasavyo ili kusukuma mbele gurudumu la Taifa letu.Baba wa Taifa Hayati Mwalimu J.K.Nyerere aliwahi kusema:yawezekana,timiza wajibu wako.TLS, UKIMYA WENU UNATUGHARIMU.
TLS (Tanganyika Law Society) ni Chama cha Mawakili cha Tanzania Bara(ambayo ndiyo iliyokuwa Tanganyika).Hii ni taasisi iliyoanzishwa kisheria mnamo mwaka 1954 kwa sheria ya ‘kikoloni’ ya Sheria ya Chama cha Mawakili wa Tanganyika,Sura Nambari 307 ya Sheria za Tanzania.Sheria hii iliundwa na Bunge la Kiingereza.Pamoja na mabadiliko ya hapa na pale yaliyofanywa kwenye Sheria hii,Mawakili wetu wamerithishwa Sheria hii-inawaongoza hadi leo.Ifahamike kuwa Chama hiki cha Mawakili hakihusishi kila Mwanasheria.Uanachama wake umeelezwa vyema chini ya kifungu cha 6 cha sheria husika.Pia kuna Sheria ya Mawakili,Sura ya 341 ya Sheria za Tanzania,pamoja na sheria ndogo na kanuni zilizoundwa kwayo, ambazo nazo zatumika pamoja katika kuwaongoza Mawakili hapa Tanzania. Ijumaa ya tarehe 17/12/2010, idadi ya Mawakili (wanachama wa Chama hiki) Tanzania ilioongezeka.Wapya zaidi ya 300 waliapishwa na Jaji Mkuu katika Sherehe maalumu zilizofanyika kwenye ukumbi wa Karimjee.
Chini ya kifungu cha 4 cha Sheria ya Chama cha Mawakili,chama kimepewa malengo tisa.Haya ndiyo yanaobeba maana halisi ya uwepo wa taasisi hii,nguvu zake na zaidi sana umuhimu wake.Malengo manne kati ya hayo yanagusa mojakwamoja ima wadau wa sheria au umma kwa ujumla.Malengo hayo manne yanaelezwa hapa ili makala hii ipate mshiko wake stahiki.Kwanza,Chama kina lengo la kuendeleza na kuimarisha viwango vya utendaji na mafunzo ya kada ya sheria.Pili,kuwezesha upatikanaji wa uelewa wa kisheria kwa wanachama wake na wengineo.Tatu,kuisaidia serikali na mahakama kwenye masuala yote yahusuyo Sheria za Bunge,utawala na utendaji wa sheria Tanzania.Na nne,kuulinda na kuusaidia umma wa Tanzania katika masuala yote yahusuyo sheria.
Kwa kutazama malengo hayo mema yaliyotolewa na Sheria kwa Chama cha Mawakili,ni wazi kuwa Jumuiya hii ya Mawakili ni ‘tegemezi’ sana kwa jamii nzima ya Tanzania.Chama hiki cha Mawakili kilitegemewa na wanasheria ambao ni lazima wajiunge na Shule ya Sheria ya Tanzania kwa ajili ya kupata mafunzo ya sheria kwa vitendo wawasaidie kuelewa vyema hatima yao.Mawakili walitegemewa kuwaeleza wanachama wao watarajiwa ni kwanini mafunzo hayo kwa vitendo ‘yameporwa’ kutoka kwenye mitaala yao ya Shahada ya kwanza ya sheria huku tasnia nyingine zote zikipata mafunzo hayo zikiwa vyuoni.Chama kilitegemewa kuwaambia wanachama watarajiwa juu ya wapi watapata fedha za kugharimia mafunzo yao hayo ya lazima ikiwa wengi wao,punde tu, walikuwa wanategemea Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu.Pia,wangewaambia kwanini Sheria mpya ya Shule ya Sheria ya Tanzania,2007 ‘imeipanda kichwani’ Sheria ya Mawakili hata bila kubadili sifa za mtu kuwa Wakili kama zinavyoidhinishwa chini ya kifungu cha 39 cha Sheria ya Mawakili,Sura Na.341.Chama kingefanya hivyo,kingekuwa kinatekeleza na kulifikia lengo la kwanza.Ukimya mkuu umetanda juu ya hili.Kwanini?
Sasa kuna suala la Katiba mpya.Kama ilivyotokea katika kipindi cha miaka ya 80, pale ambapo Chama hiki cha Mawakili kilisimama kidete na mstari wa mbele kuishinikiza Serikali kuweka Ibara zinazozungumzia Haki za Binadamu katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977.Serikali ‘ilisikiliza’ sauti ya Chama hiki na wadau wengineo na kukubali kuingiza Haki za Binadamu ndani ya Katiba yetu mwaka 1984 kupitia Sheria Nambari 15 ya mwaka huo.Sasa,Ibara za 12-30 za Katiba yetu zinatulinda! Tulitarajia kuwa Chama hiki kingerudia harakati zake au zinazofanana na zile za miaka ya 80 kufanikisha uundwaji wa Katiba mpya.Chakushangaza,Chama hiki cha Mawakili kimekuwa kimya mno.Ni mwanachama mmojammoja tu ndiye anayejitokeza kutoa maoni yake juu ya Katiba mpya.Tumewasikia akina Profesa Issa Gulamhussein Shivji,Profesa Abdala Safari,na Arold Sungusia ‘wakitoka kivyao’. Kwanini kusiwe na tamko la pamoja la kuonyesha msimamo wa Chama juu ya suala hili la Katiba mpya? Lengo la nne lililoelezwa hapo juu litafikiwaje?
Chama hiki cha Mawakili ni muhimu sana kwa watanzania wote.Sio tu kwa kuwapatia ‘watetezi’ kwenye kesi zao bali pia kuwafumbua macho na kuwasaidia kadiri ya uwezo wa kisheria kilichopewa.Watanzania wengi ni ‘majuha’ wa sheria.Wanatamani sana kusikia ufafanuzi wa kisheria wa mambo wanayoyasikia kila siku:Richmond,Meremeta,IPTL,Do wans,EPA,Kiwira,Buzwagi na mengineyo.Chama hiki kinawanyima uhondo-hakisemi ukweli.Wanachama wake wanabaki tu kuchangamkia nafasi za kuwatetea washtakiwa wa mambo kama haya na mengine wakisahau wajibu(malengo) wao.Wanabaki wakiwa ‘bize’ mahakamani kwa kesi ambazo kama wangeshiriki ipasavyo kutimiza wajibu wao kwa Taifa zisingekuwa hivyo zilivyo.
Ni wakati muafaka sasa kwa Chama hiki cha Mawakili kuvaa uhalisia wake-kurudi kwenye malengo yake.Majibu ya mateso ya wanasheria juu ya Shule ya Sheria ya Tanzania na mengineyo muhimu kwa umma wa Tanzania yanasubiriwa kwa hamu.Mabegi makubwa ya wanachama wa TLS sasa yabebe pia hoja murajabu juu ya mustakabali wa Taifa letu badala ya kubeba tu hati za mashtaka za wateja wao,Sheria zinazowaoongoza na kalamu.Pia,wasiwe ‘bize’ tu kuchukuliana hatua za kinidhamu.Ni muda wa TLS kusema na Serikali isikie.Umma utasikiliza.Utamuona mbaya nani.Utamshughulikia.TLS anzisheni Tanzania yenye neema na si hii ya kuhema.Ni ukweli usio kifani kuwa ukimya wa TLS unatugharimu.



Reply With Quote

Follow Us Here