Bodi ya mikopo elimu ya juu yaja na vigezo vipya
2007-05-26 10:27:41
Na Mwandishi Wetu
Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELSB), imetangaza vigezo vipya vitakavyotumika kutoa mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu ambavyo vitazingatia uwezo wa kiuchumi wa waombaji.
Kwa mujibu wa tangazo la HELSB lililotolewa kwenye vyombo vya habari jijini Dar es Salaam jana, utaratibu huo mpya wa mikopo, utaanza kutumika mwaka wa masomo wa 2007/08.
Chini ya utaratibu huo, waombaji wamegawanywa katika makundi matano yaani A, B, C, D, E na F.
Taarifa hiyo imefafanua kuwa, wanafunzi katika A watapata asilimia 100 ya mkopo, B asilimia 80 na waombaji wa kundi C, watapewa asilimia 60.
Iliongeza kuwa, waombaji katika kundi D, watalipiwa kwa asilimia 40, E watapewa asilimia 20 na kundi F ambao hawatakopeshwa hata senti.
Wanafunzi watakaokubaliwa mikopo hiyo watalipiwa gharama kadhaa ikiwemo mafunzo, posho ya chakula, malazi, tahadhari, tiba, vitabu na mafunzo ya vitendo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kupewa mkopo kutategemea uchambuzi na mchujo utakaofanywa ili kuona hali ya kiuchumi ya mwombaji, wazazi ama walezi wake na hivyo mikopo itatofautiana kutoka mwanafunzi mmoja hadi mwingine.
Utaoaji wa mikopo utafanywa kwa kuchunguza waombaji kwa utaratibu utakaotolewa na HELSB ambao hata hivyo haukufafanuliwa.
Aidha, Bodi imewaonya waombaji watakaobainika kutoa taarifa za uongo ama kwa maandishi au mazungumzo ambayo yataathiri taratibu za maombi ya mkopo, kuwa watapewa adhabu ya kifungo cha miezi sita au kulipa faini ya Sh. milioni 1.5.
Kadhalika, ilisema iwapo mwombaji atakuwa amepewa mkopo kutokana na udanganyifu, Bodi itauzuia na kuufuta mara moja na mhusika kufikishwa mahakamani.
Hata hivyo, taarifa hiyo imesisitiza kuwa, utaratibu wa wanafunzi wa Kidato cha Sita waliofaulu Daraja la Kwanza kwa wanaume na Daraja la Kwanza na la Pili kwa wanawake, utaendelea kutumika katika utoaji wa mikopo hiyo.
Ilifafanua kuwa, kipaumbele kitatolewa kwa wanafunzi wanaosomea kozi za Tiba, Sayansi, Kilimo, Ualimu, Uhandisi na Teknolojia.
SOURCE: Nipashe
Follow Us Here