Makamba amwinda Mengi
- Ahoji safari za mikoani
Mwandishi Wetu Aprili 22, 2009
Raia Mwema~Muungwana ni Vitendo
HUKU kukiwa na shinikizo la kutaka kumuondoa katika nafasi yake Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Yussuf Makamba, mwanasiasa huyo machachari, ametajwa sasa kumfuatilia Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni za IPP, Reginald Mengi.
Makamba ameelezwa kupendekeza ndani ya vikao vya chama hicho kuchunguzwa kwa uhusiano wa Mengi na wanasiasa waandamizi wa CCM wakiwamo wabunge, wengi wao wakiwa ni wale wanaofahamika kwa kuwa mstari wa mbele kupambana na ufisadi.
Habari za ndani ya vikao vya juu vya CCM vilivyofanyika Dar es Salaam mwishoni mwa wiki na baadaye mjini Dodoma, zinaeleza kwamba Makamba alitoa hoja hiyo katika vikao vya Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM na katika Kamati ya Maadili na Usalama ya chama hicho tawala.
Wakati Makamba akiwasilisha hoja hiyo, Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, alikuwa mmoja wa wageni wazito walioshiriki sherehe za miaka 75 ya kuzaliwa Waziri Mkuu Mstaafu na Mbunge wa Mtera, John Malecela, mahali ambapo anaelezwa kusifia juhudi za wabunge wanaopinga ufisadi.
Miongoni mwa wabunge ambao Makamba anahisi wanaivuruga CCM wakiungwa mkono na Mengi ni pamoja na Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela, ambaye pamoja na kupongezwa na Kikwete kupata zawadi ya mwanamke shujaa, alikuwa mmoja wa washiriki wa sherehe ya kuzaliwa mumewe mwishoni mwa wiki, jijini Dar es Salaam.
Pamoja na mambo mengine, Makamba anadaiwa kuhoji sababu ya Mengi kuingilia mambo ya CCM kwa kushirikiana na baadhi ya wanasiasa wa ndani ya chama hicho, hali ambayo Katibu Mkuu huyo wa CCM anaielezea ndani ya vikao kama inaashiria hatari kwa chama hicho siku za usoni.
Hatua ya Makamba kumgusa Mengi katika vikao rasmi vya chama, vimeelezwa kuwa sehemu ya mkakati maalumu wa kupunguza kasi kubwa ya mfanyabiashara huyo kuonekana akishirikiana na baadhi ya wabunge katika baadhi ya shughuli mbalimbali za kijamii, huku wakibainisha wazi kumuunga mkono Rais Kikwete.
Ingawa haijawekwa bayana lengo hasa la mapendekezo ya Makamba ni kuhoji pia hatua ya hivi karibuni ya Mengi kutoa misaada ya fedha kwa ajili ya kusaidia makundi mbalimbali ya kijamii kujiinua kiuchumi katika baadhi ya majimbo ya wabunge mbalimbali wa CCM bila kuyahusisha makao makuu ya chama hicho.
Mengi pia amekuwa mstari wa mbele katika vita ya ufisadi, vita ambayo inaungwa mkono na baadhi ya wabunge wa CCM akiwamo Anne Kilango - Malecela, ambaye hivi karibuni alitunukiwa Tuzo ya Mwanamke Jasiri na Serikali ya Marekani, kupitia ubalozi wake nchini.
Hata hivyo, habari zinaeleza kwamba hatua hiyo ya Makamba ni mkakati wa kujihami ama kulipiza kisasi kutoka kwa baadhi ya wanasiasa wakiwamo wabunge wanaopinga ufisadi ambao wamekuwa wakitaka kiongozi huyo kuondolewa katika nafasi yake kutokana na kushindwa kukisaidia chama hicho.
Tayari Makamba alitengwa katika kampeni za uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Mbeya Vijijini, ambako CCM ilishinda baada ya kuelezwa kwamba kiongozi huyo wa CCM alikuwa chanzo cha chama hicho kushindwa katika uchaguzi mdogo wa jimbo la Tarime.
Imefahamika kwamba sasa hata uchaguzi mdogo wa jimbo la Busanda, Makamba hatoshiriki kikamilifu, kukitolewa sababu kwamba ana majukumu mengi ya kitaifa na sababu nyingine za kiafya. CCM wanatarajiwa kumteua Lolesia Bukwimba, kuwania ubunge jimbo la Busanda.
Hayo yakiendelea, huko Mbeya, hali si shwari ndani ya chama hicho baada ya kuwapo mtafaruku miongono mwa viongozi wa CCM katika wilaya hiyo.
Katika moja ya matoleo yake, Raia Mwema ilikuwa na makala yenye kuelezea tahadhari iliyotolewa na wananchi wilayani Kyela kwa Rais Jakaya Kikwete kuhusu mwenendo wa kisiasa wilayani humo, sasa imedhihiri kwamba kilio cha wananchi wale kilikuwa ni cha kweli na kilipaswa kufanyiwa kazi na si kupuuzwa kama ilivyojidhihirisha.
Viongozi wa Chama cha Mapinduzi wilayani Kyela sasa wamefikia hatua inayoipeleka wilaya hiyo kwenye machafuko makubwa zaidi, kwani kitendo cha makatibu kata wanne wa Chama hicho kuwavamia viongozi wao wa Kamati ya Maadili ya Wilaya hiyo na kuwapiga wakitumia mateke na ngumi, kinazidi kuongeza chumvi kwenye kidonda.
Makatibu kata hao wanne wanaodaiwa kuwatwanga viongozi wao ni pamoja na Josephat Mwakajinga kutoka kata ya Kajunjumele, Grayson Mwaikambo wa kata ya Kyela mjini, Alex Mwaisombwa wa kata ya Lusungo na Ipyana Mwangunga ambaye ni Katibu Mwenezi wa kata ya Makwale
Hali ya kimazingira inaonyesha kuwa vurugu hizo zilimlenga zaidi Katibu wa Chama hicho wilayani Kyela, Maria Mwambanga ambaye kwa mujibu wa mjumbe mmoja wa Kamati ya Siasa ya Wilaya hiyo, inaelezwa kuwa wanataka kumuondoa kwa madai kuwa yuko upande wa Mbunge wa Jimbo hilo, Dk Harrison Mwakyembe.
Pamoja na madai hayo kuna taarifa vile vile kuwa Katibu huyo hatakiwi na baadhi ya viongozi wa chama hicho wilayani humo kwa madai kuwa hashindi ofisini na muda mwingi amekuwa akiutumia jijini Mbeya, hivyo kuunda genge la kumuondoa kwa nguvu.
Hata hivyo Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kyela, Japheth Mwakasumi anaelezea kushangazwa kwake na hatua ya makatibu kata hao kumvamia na kumpiga Mtendaji Mkuu wa Chama wilayani humo kwa madai yasiyo na kichwa wala miguu.
“Dhamira yao wanataka mtu anayepokea mawazo yao, hapo ndipo ninaposhindwa kuwaelewa kwani si unayaleta kwenye vikao, ni wazi kuwa there is someone behind, maana miongoni mwa madai yao ni kwamba Katibu ni mtu wa Mbunge, kwa kweli siwaelewi,” anaelezea kwa masikitiko Mwenyekiti huyo katika mahojiano maalumu na Raia Mwema.
Akizungumzia hali ya Katibu wake anasema sio nzuri na kwamba anaendelea na matibabu ikiwemo kupigwa picha.
“Wee unafanya mchezo midume mizima inamshambulia mwanamke, hapana tumefika pabaya kama siasa zenyewe ndio hizi za majungu yasiyo na kichwa wala miguu halafu mnamshambulia mwamamke asiye na hatia,” anazidi kushangaa Mwenyekiti huyo.
Aidha akizungumzia kinachoendelea ndani ya Chama hicho, Mwakasumi alisema kuwa Kamati ya Siasa ya Wilaya itaketi kesho Alhamis kulijadili suala hilo na kutoa maamuzi.
Hata hivyo, duru za ndani ya chama hicho wilayani humo zinabaisha kwamba vurugu hizo zilizosababisha Katibu huyo wa Wilaya kuumizwa vibaya, zinafadhiliwa na mmoja wa madiwani wilayani humo na kiongozi wa moja ya jumuiya za chama hicho mkoani Mbeya.
Ni wazi kwamba kwa taarifa hizo ni kwamba kuna kila dalili ya kuwepo kwa kambi mbili zenye mielekeo tofauti ya kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu mwakani.
Katika mahojiano na baadhi ya viongozi wa juu wa Chama hicho katika Wilaya ya Kyela pamoja na mkoani, wanazihusisha vurugu hizo moja kwa moja na harakati za kampeni za uchaguzi ujao mwakani na kwamba mbinu inayotumiwa na wafanya vurugu hao katika kukabiliana na Mbunge aliyepo haitofautiani na ile iliyotumika katika uchaguzi uliopita, kumtenganisha na uongozi wa juu wa chama hicho wilayani humo.
Katika mchakato wa kumpata mgombea ubunge wa Jimbo hilo kupitia CCM, viongozi wa juu wa wilaya wa Chama hicho hawakumtaka kabisa Mbunge wa sasa na badala yake waliegemea kwa Mbunge aliyekuwapo madarakani wakati ule, na hata Dk. Mwakyembe aliposhinda kwenye mchujo huo bado viongozi hao hawakumpa ushirikiano hivyo kutegemea zaidi nguvu ya wapiga kura ambako hadi sasa ndiko nguvu yake iliko.
Inaelezwa kuwa vurugu hizo za Jumamosi iliyopita zilitokea kwenye Kikao cha Kamati Maadili kilichoitishwa maalumu na kwa ajili ya kuwahoji baadhi ya makatibu kata, pamoja na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wa Wilaya hiyo, Visk Mahenge wanaotuhumiwa kuhusiana na vurugu zilizosababishwa na baadhi ya wajumbe wa Kikao cha Halmashauri Kuu ya Chama ya Wilaya hiyo Machi 31, mwaka huu.
Pamoja na tuhuma hiyo, Mwenyekiti wa Chama hicho Wilayani Kyela, Mwakasumi anaitaja tuhuma nyingine iliyokuwa wahojiwe makatibu hao ni kwa baadhi ya makatibu hao kudaiwa kuendesha kikao chenye mlengo wa kampeni za uchaguzi mwakani huku kikihusishwa na utoaji posho nje ya taratibu za chama hicho.
Wakizungumzia suala hilo la kampeni viongozi wa Chama hicho mkoani hapa walibaisha kuwa wanaelewa kuwepo kwa kampeni zinazoendelea chini kwa chini, lakini wakasisitiza haziwezi zikahalalishwa kuudharau uongozi uliopo madarakani kwani kwa kufanya hivyo ni kuruhusu vurugu na matumizi ya rushwa.
Mmoja wa viongozi wa chama hicho mkoani hapa alifikia hatua ya kusema, “Kinachonisikitisha ni hatua ya baadhi ya viongozi waandamizi wa serikali kuchochea vurugu ndani ya chama wilayani Kyela, Katibu anatekeleza wajibu wake kwa kufuata kanuni na taratibu za chama zilizopo, hawezi kutoshirikiana na Mbunge wa jimbo la wilaya yake, hata kama mbunge ni kutoka chama cha upinzani bado angeshirikiana naye, ila tu asingeruhusiwa (mbunge wa upinzani) kuingia kwenye vikao vyetu vya chama, lengo ni maendeleo kwa wananchi na sio watu binafsi.”
Moja ya matatizo yanayozikabili siasa za mkoa wa Mbeya ni kwa baadhi ya wanasiasa kuendelea kuishi katika ndoto za mtandao uliomwingiza madarakani Rais Jakaya Kikwete, wakiamini kwamba bado unazo nguvu zile zile za mwaka 2006 kurudi nyuma.
Pamoja Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya, Nawab Mulla kunukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari akielezea kuchukuliwa kwa hatua za nidhamu kwa waliosababisha vurugu hizo iwapo suala hilo litatuliwa nje ya mahakama, baadhi ya wanachama wameelezea kupingana naye katika hilo kwa maelezo kuwa Chama hicho siku hizi hakina uwezo huo wa kuwajibishana.
Wanautaja mgogoro ulioibuka kwenye kikao kimoja cha CCM Mkoa ambapo kiongozi mwanamke alitaka kumvalisha sidiria kiongozi mwenzake mwanaume kwa madai kwamba anaingilia mambo ya wanawake, lakini duru za kisiasa mkoani humo zikidai kuwa sababu hasa ni kutoungwa mkono kwenye kampeni zake kuwania uongozi wa juu wa chama hicho kwenye moja ya jumuiya zake.
Videos:Originally Posted by Invisible
[ame="http://www.youtube.com/watch?v=nj5RN-xHwlQ"]YouTube - Mengi s Press Conference on 23 April 2009 Part I[/ame]
[ame="http://www.youtube.com/watch?v=rDMD8nOBfEo"]YouTube - Mengi s Press Conference on 23 April 2009 Part II[/ame]




LinkBack URL
About LinkBacks

Reply With Quote




Bookmarks