Baada ya miezi kadhaa ya vuta nikuvute hatimaye Bodi ya Kimataifa ya Soka IFAB iliwaruhusu wanawake Waislamu kuvaa vazi la hijabu katika mashindano ya kimataifa ya mpira wa miguu. Uamuzi huo wa IFAB umekaribishwa kwa mikono miwili katika nchi za Kiislamu ambazo timu zao za wanawake za soka zimekuwa zikizuiwa kushiriki katika mashindano ya kimataifa ya soka kwa sababu ya vazi la staha la hijabu.
Shirikisho la Soka la Asia liliwasilisha ombi rasmi kwa IFAB likitaka wachezaji wa soka wa kike waruhusiwe kucheza mchezo huo katika mechi za kimataifa wakiwa na vazi la hijabu. IFAB iliafikiana na ombi hilo kimsingi lakini iliomba muda kwa ajili ya kuchunguza vizuizi vyote vinavyohusu suala hilo hususan vile vinavyohusiana na masuala ya kiafya na usalama wa wachezaji.
Ni vyema kukumbusha hapa kuwa Aprili mwaka huu Shirikisho la Soka Duniani FIFA lilikuwa limetangaza kuwa litapiga marufuku vazi la hijabu katika michezo ya Olimpiki ya mwaka huu mjini London.
Mwaka jana timu ya soka ya wanawake ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ilizuiwa kushiriki katika raundi ya pili ya kuwania tiketi ya michezo ya Olimpiki dhidi ya Jordan baada ya wachezaji wake kukataa kuvua vazi la Kiislamu la hijabu. Baada ya wachezaji soka wa kike wa Iran kukataa kuvua vazi la staha la hijabu FIFA iliitambua Iran kuwa imeshindwa magoli matatu kwa sifuri na kuiidhinisha Jordan kwa ajili ya raundi nyingine. Iran ambayo ilikuwa inaongoza kundi hilo ilikoseshwa fursa ya kushiriki katika michezo ya Olimpiki huko London kutokana na marufuku hiyo.
Uamuzi wa sasa wa IFAB wa kuwaruhusu wanawake wa Kiislamu kuvaa vazi la hijabu katika mashindano ya soka umechukuliwa baada ya hitilafu za zaidi ya mwaka mmoja juu ya kadhia hiyo.