Ni katika harakati za kupambana na UKIMWI
Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya simu za mkononi ya Celtel Tanzania, imetoa sh. milioni 40 kwa Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili, Alhaj Ali Hassan Mwinyi, ikiwa ni udhamini wa kampuni hiyo ili ashiriki kupanda Mlima Kilimanjaro.....
Meneja Uhusiano wa Celtel Tanzania, Beatrice Mallya alisema Dar es Salaam jana kuwa Alhaj Mwinyi alikabidhiwa fedha hizo juzi mjini Moshi ikiwa ni mchango wa Celtel kumwezesha kushiriki Geita Kiliclimb Challenge kwa ajili ya kupambana na maambukizi ya maradhi ya UKIMWI nchini Tanzania.
Alisema Celtel kwa kushirikiana na kampuni ya mgodi wa madini ya dhahabu ya Geita, wamemwezesha Alhaj Mwinyi kupanda Mlima Kilimanjaro ili kutekeleza dhamira yake ya kupambana na UKIMWI. Alhaj Mwinyi alianza kupanda mlima huo juzi (Jumamosi).
Beatrice alisema Celtel ilianza kudhamini wapandaji Mlima Kilimanjaro kwa zaidi ya miaka minne iliyopita na itaendelea kudhamini kwa vile inaamini nguvu na juhudi zinazotumika kupanda mlima huo, zinaleta matumaini ya kupambana na UKIMWI.
"Tumefurahi zaidi kwamba mwaka huu Rais mstaafu, Alhaj Mwinyi anapanda Mlima Kilimanjaro kwa udhamini wa Celtel," alisema Beatrice na kubainisha kwamba kampuni hiyo pia mwaka huu inawakilishwa na Meneja wa Kitengo cha Fedha wa Celtel, Prisca Tembo kupanda mlima huo.
Akizungumza baada ya kukabidhiwa kitita hicho cha fedha, Alhaj Mwinyi mwenye umri wa miaka 83, alisema amepata msukumo wa kupanda Mlima Kilimanjaro ili kuendeleza juhudi zake katika mapambano dhidi ya UKIMWI, ikiwa ni njia mojawapo ya kuisaidia Tanzania na kutekeleza kauli mbiu ya Serikali kwamba Tanzania inawezekana bila UKIMWI.
"Lengo letu ni kuhakikisha jamii inaishi katika maisha salama bila kupata maambukizi ya UKIMWI kama tunavyoshauriwa na wataalamu, kuzingatia muongozo uliopo," alisema Alhaj Mwinyi.
Alisema alijisikia furaha na kuona fahari baada ya Ofisa Mwendeshaji Mkuu wa Celtel Afrika Mashariki, Bw. Bashar Arafeh kumweleza dhamira ya kampuni hiyo kumdhamini ili apande Mlima Kilimanjaro.
"Niliona ufahari! Nilikuwa na shauku ya kupanda Mlima Kilimanjaro mwaka huu, lakini ahadi kutoka kwa Bw. Bashar iliniongezea matumaini na morali ya kupanda Mlima Kilimanjaro, kwa lengo lile lile la kupambana na maambukizi ya UKIMWI kwa watu wetu na taifa letu," alisema Alhaj Mwinyi.
Alhaj Mwinyi aliishukuru Celtel kwa kumdhamini na mchango mkubwa ambao kampuni hiyo inatoa kusaidia jamii katika nyanja mbalimbali hasa elimu.
Global Publishers - Tanzania Newspapers

Reply With Quote
Follow Us Here