Thursday, 16 August 2012 21:29
|
Geofrey Nyang'oro na Zaina Malongo
SERIKALI imeweka wazi kuwa hadi sasa hakuna majibu sahihi yanayoweza kuthibitisha kuwapo kwa ugonjwa wa
Ebola kwa kuwa hakuna maabara ya kupima ugonjwa huo.
Aidha hali hiyo imesababisha vimelea vya mtu aliyedaiwa kuwa na dalili za ugonjwa huo kupelekwa Uganda ambako kuna mabara zinazofanya kazi ya uchunguzi na kutambua ugonjwa huo.
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dk Hussein Mwinyi alisema hayo jijini Dar es Salaam jana alipokuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari waliotaka kujua hatua ilipofikia kuhusu ugonjwa wa Ebola.
Agost 5 mwaka huu maofisa wa afya walifika Hosptali Teule ya Wilaya ya Karagwe ya Nyakahanga na kumuona mgonjwa akiwa na baadhi ya dalili zinazofanana na ugonjwa wa Ebola na kuzipeleka Dar es Salaam kwa uchunguzi zaidi.
Akifafanua hilo Dk Mwinyi alisema hadi sasa hakuna majibu ya vipimo hivyo kwa kuwa vilipelekwa Uganda ambao wana maabara zinazothibitisha tatizo hilo.
Alifafanua kuwa hadi sasa bado majibu ya vipimo hivyo vya ugonjwa huo wa mlipuko havijarejea nchini lakini akawatoa hofu watanzania akisema hadi sasa hakuna kesi nyingine iliyoripotiwa.
“Nikweli hatujapata majibu ya vipimo vile,lakini hakuna sababu kwa watanzania kuwa na hofu kwani hakuna kesi nyingine ya mgonjwa iliyopatikana hadi sasa”alisema Dk Mwinyi.
Mwinyi alifafanua kuwa serikali kupitia wizara hiyo ya Afya inaendelea na mchakato wa kuelimisha jamii juu ya namna ya kukabiliana na ugonjwa huo ambao hauna dawa.
“Ugonjwa huu unaambukizwa na kirusi aina ya fangasi, vimelea hivyo vipo vingi na vinatofuatiana na ndio sababu tumepeleka Uganda kupima, lakini kwa kuwa tatizo hilo limekuwa likijirudia nchini tunaona haja ya sisi kuwa na kipimo hicho”alisema Mwinyi.
Wakati mtu mmoja akigundulika kuwa na dalili za ugonjwa huo wa Ebola, nchi jirani ya Uganda ulishatokea na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 100.Mwinyi alisisitiza kuwa serikali bado inafuatilia majibu hayo na kwamba pindi yatakapopatikana itayatoa kwa umma.
|
Follow Us Here